BENKI YA DUNIA: Tanzania iko chini ya wastani wa urahisi wa kiuchumi wa kuanzisha biashara

Jamii Africa

Ripoti mpya iliyotolewa na Benki ya Dunia (WB) imesema urahisi wa kuanzisha biashara nchini Tanzania uko chini ya wastani unaotakiwa na nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara, sababu  inayokwamisha ukuaji wa sekta binafsi na uchumi wa wananchi.

Ripoti hiyo ambayo imetolewa mapema mwaka huu  ni matokeo ya utafiti kupitia mradi wa ‘Doing Business’  katika nchi 190 duniani kwa mwaka 2017 na kuchambua takwimu za sheria na sera zinazosimamia sekta ya biashara ambapo imeielezea Tanzania kama nchi ambayo inayokabiliwa na changamoto mbalimbali za kimchakato katika uanzishaji wa biashara.

Tanzania iko nafasi ya 162 sawa na asilimia 73.03 kati ya nchi 190 duniani ambapo kiwango hicho kiko chini ya wastani wa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara cha asilimia 76.82. Tanzania inaungana na nchi  za Malawi na Botswana ambazo ziko kwenye kundi moja la nchi zilizo chini ya mstari wa ‘frontier score’

Kwa mujibu wa ripoti hiyo asilimia 100 ni sawa na ‘Frontier score’ alama inayotambulisha nchi zenye utendaji mzuri zaidi kwenye uchumi hasa urahisi wa  kufanya biashara.  Upangaji wa kuupa nafasi uchumi wa nchi katika urahisi wa kuanzisha biashara unapatikana kwa kuangalia umbali wake kufikia ‘Frontier scores’ambapo ni kiwango bora cha kuanzisha biashara.

 

URAHISI WA KUANZISHA BIASHARA KWA NCHI ZA AFRIKA

 

Frontier scores hutofautiana kulingana na kanda  na kiwango cha ukuaji wa uchumi na hali ya kisiasa ya nchi husika.

Ripoti hiyo inabainisha kuwa katika nchi 5 za Afrika Mashariki, Tanzania bado haina mwelekeo mzuri wa urahisi wa kuanzisha biashara ambapo imeshika nafasi  4 kwa kupata asilimia 73.03 ikifuatiwa na  Uganda. Burundi ndio nchi yenye mazingira rahisi ya kiuchumi ya kuanzisha biashara ikiwa na 91.94% ikifuatiwa na Rwanda (87.62%) pamoja na Kenya (83.20).

Wastani wa  nchi za Afrika Mashariki kwa mazingira rahisi ya kiuchumi ya kuanzisha biashara ni 81.62%. kwa muktadha huo Tanzania na Uganda ziko chini ya wastani unaohitajika huku Kenya, Burundi na Rwanda zikiwa juu ya wastani unaotakiwa.

Utafiti ulitumia njia mbalimbali kupata matokeo ambapo uliweka viashiria vya urahisi wa kuanzisha biashara vikiwemo; muda, gharama, mtaji na mchakato wa kupata vibali vya biashara.

Kulingana na vigezo hivyo, Tanzania imeangushwa na ongezeko la ada ya usajili inayotozwa kwenye ardhi na makazi ambako biashara mpya zinafunguliwa. Pia ukiritimba wa upatikanaji wa leseni  na   mlundikano wa kodi kwa wafanyabiashara na kodi mpya inayokatwa kwenye mishahara ya wafanyakazi.

Ili kutimiza malengo ya mradi huo, utafiti huo uliangazia mambo mengine muhimu  ikiwemo  mtaji  wa kuanzisha  biashara,  vibali vya ujenzi, kupata umeme, hati ya ardhi na nyumba, mikopo, ulinzi kwa wawekezaji, ulipaji  kodi, biashara nje ya mipaka, utekelezaji wa mikataba na ufilisi wa mali.

Kwa upande wa dunia, New Zeland  imekuwa nchi ya kwanza miongoni mwa nchi 10 zenye urahisi wa kufanya biashara, ikufuatiwa na Singapore pamoja na Denmark.

URAHISI WA KUANZISHA BIASHARA KWA NCHI ZA AFRIKA YA MASHARIKI

 

Lakini nchi za Somalia, Congo DRC, Afghanistan, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Libya, Yemen, Sudan ya Kusini, Venezuela na Eritrea zimewekwa kwenye kundi la nchi 10 za mwisho ambazo sio rahisi kufanya biashara. Sababu kubwa ni vita vya wenyewe kwa wenyewe vinavyochochewa na makundi ya waasi wasioridhishwa na mwenendo wa siasa za nchi husika.

Mapendekezo ya ripoti hiyo kwa Tanzania ni kuboresha mfumo wa upatikanaji wa hati za ardhi na majengo ya kufanyia biashara ili kuvutia wawekezaji wengi kwa muda mfupi  na kupunguza gharama  na mchakato wa kupata vibali vya biashara. Pia kulegeza masharti ya ulipaji kodi kwa sekta binafsi.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *