Halmashauri yachunguza ambulance kukodishwa kwa wagonjwa

Frank Leonard

HALMASHAURI ya Wilaya ya Iringa imeanza uchunguzi unaohusu kituo cha afya cha Idodi,  kukodisha gari lake la kubeba wagonjwa (ambulance) wakiwemo wajawazitro kwa Sh 20,000 hadi Sh 70,000.

Hivi karibuni baadhi ya wananchi wa kijiji hicho waliulalamikia utaratibu huo wakidai kwamba unawaumiza kiuchumi na kuwapotezea hadhi stahiki ya kupata huduma za afya.

Taarifa kutoka ofisi ya mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya hiyo iliyotolewa na Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Pudenciana Kisaka imesema uchunguzi kuhusiana na madai hayo ya wananchi umeanza mara moja.

Kisaka amewataka wananchi wa kijiji hicho na vingine vinavyotumia huduma ya gari hilo la wagonjwa kutoa taarifa za kweli kuhusu madai hayo.

IMG_5190
Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Iringa, Pudenciana Kisaka

Wakizungumza na gazeti hili hivikaribuni, wananchi hao walisema jambo linalosikitisha ni kuona hata wajawazito na watoto chini ya miaka mitano wanalazimika kutoa gharama hizo.

Mkazi mmoja wa kijiji hicho, Emanuel Mduda alisema wakati mke wake akijifungua mtoto wake wa pili alitumia Sh 70,000 kama gharama ya kumsafirisha hadi hospitali teule ya wilaya ya Iringa ya Tosamaganga.

“Alipokaribia kujifungua nilitumia saa moja kumfikisha katika zahanati ya Mapogoro iliyopo kilomita nane kutoka katika kijiji chetu; nilitumia usafiri wa baiskeli,” alisema.

Baada ya kumfikisha katika Zahanati hiyo, aliandikiwa rufaa ili apalekwe katika kituo cha afya cha Idodi kilichopo kilomita nane kutoka Mapogoro.

“Nilitumia Sh 20,000 kukodi ambalance hiyo na tulipofika Idodi mke wangu aliandikiwa rufaa tena ya kwenda hospitali teule ya wilaya ya Iringa ya Tosamaganga,” alisema.

Alisema alitumia Sh 50,000 kukodi gari hilo la wagonjwa kutoka Idodi hadi Tosamaganga na kuuliza dhana ya huduma bure kwa wajawazito na watoto ina maana gani.

Malalamiko ya Mduda yaliungwa mkono na Mwenyekiti wa kijiji cha Kitisi, Jonisia Pinda aliyesema huduma ya afya kwa wakazi zaidi ya 1,500 wa kijiji ni kero kubwa.

Hata hivyo alisema kijiji kimekamilisha ujenzi wa Zahanati yake ambayo haijaanza kufanya kazi kwasababu haina watoa huduma.

“Hivi sasa tunaendelea na ujenzi wa nyumba moja ya mganga; hata hivyo ujenzi wake umekwama kwasababu hatuna fedha,” alisema.

Ili kukamilisha ujenzi wa nyumba hiyo ya mganga, Mkurugenzi wa Kampuni ya Mkwawa Hunting Safari, Ahamed Huwel ameahidi kuchangia Sh Milioni tatu.

Huwel ambaye kampuni yake imepata kibali cha kuwekeza katika eno la Jumuiya ya Matumizi Bora ya Mali Hai Tarafa ya Idodi na Pawaga (MBOMIPA) alisema anaguswa na matatizo ya wananchi wa vijiji vinavyounda jumuiya hiyo inayopakana na hifadhi ya taifa ya Ruaha na ndio maana anawasaidia.

1 Comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *