Hofu ya Usalama kwa wafanyakazi GGM Yatanda

David Azaria

SIKU chache baada ya moto kuzuka ndani ya mgodi wa Geita (GGM) na kuteketeza mali zenye thamani ya zaidi ya shilingi Bilioni 25,hofu kubwa ya kupoteza maisha imeibuka kwa uongozi na wafanyakazi wa mgodi huo.

Uchunguzi umebaini kuwa baada ya kutokea kwa tukio la moto,lilitokea jaribio la mmoja wa maofisa wa mgodi huo katika Idara ya Utumishi kunusurika kuteketezwa kwa moto ndani ya ofisi yake baada ya kukuta ametegeshewa ‘bomu’ petroli kwenye chombo cha kuhifadhia taka.

Imedaiwa kuwa siku hiyo mtu ambaye bado hajafahamika aliingia ndani ya ofisi ya ofisa huyo na kuweka dumu lenye mafuta ya petrol lenye ujazo wa lita moja na nusu,na kisha kuiweka ndani ya ndoo ndogo ya kihifadhi uchafu na badaye klifunika dumu hilo kwa makaratasi na kuwasha moto.

Mkurugenzi wa mgodi huo Garry Davies alithibitisha kwamba moto huo mkubwa ambao chanzo chake bado hakijafahamika,unadaiwa kuwa huenda ukawa umesababisha hasara ya zaidi ya shilingi Bilioni 25.

“Ni tukio la ajabu,limetustua sana,bado hatujui chanzo chake,lakini tutafanya uchunguzi kubaini chanzo cha moto,kwa sababu ni nadra sana kwenye maeneo kama haya yetu moto wa aina hii kutokea….’’ Alisema Davies wakati akitoa taarifa kwa mkuu wa mkoa wa Geita Said Magalula.

1

Hizi ni Bohari mbili zilizosheheni vifaa mbalimbali mali ya mgodi wa GGM zikiteketea kwa moto.

Mkuu wa Mkoa wa Geita Magalula alilitaka jeshi la polisi kufanya uchunguzi wa kina ili kubaini chanzo cha tukio hilo,ili kuepusha madhara mengine makubwa kama hayo kutokea tena.

Kwa mujibu wa uchunguzi wa Gazeti hili bohari hizo mbili zilizoteketea kwa moto zilikuwa na vifaa mbalimbali kwa ajili ya shughuli za mgodi,na kwamba hali hiyo imesababisha kuoungua kwa uzalishaji kutokana na baadhi ya vifaa kutokuwepo.

Mmoja wa maofisa wa ngazi ya juu wa mgodi huo ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini alitaja baadhi ya vifaa vilivyoteketea kwa moto kwamba ni sare za aina mbalimbali za wafanyakazi,vipuri vya mitambo mbalimbali vya uchimbaji,pamojana vifaa vingine vya umeme.

“Hasara ni kubwa sana,bado hatujajua hasa hasara kamili lakini kama taarifa ya Mkurugenzi wa mgodi ilivyoeleza ndivyo hivyo,tunatarajia kupata taarifa kamili ya hasara baada ya uchunguzi wa wataalamu kutoka ndani nan je ya nchi itakapomaliza kazi yake…..’’ alisema Ofisa huyo.
2
Haya ni Magari ya zimamoto ya mgodi yakijaribu kuzima moto,bila mafanikio

MINONG’ONO

Habari zilizopatikana kutoka kwa baadhi ya wafanyakazi wa mgodi huo zimeeleza kuwa kumekuwepo na minong’ono ya tukio hilo kuhusishwa na ‘ugaidi’ kutokana na hasa mazingira ya tukio zima kwa ujumla.

‘Ndiyo maana unaona uongozi wa mgodi umeomba wachunguzi wa kimataifa kuja kufanya uchunguzi wa tukio hilo,ili kuondoa wasiwasi kwa uongozi pamoja na wafanyakazi wa mgodi…’’ alisema mmoja wa wafanyakazi ambaye aliomba jina lake kuhifadhiwa.

Hata hivyo baadhi ya wafanyakazi wamedai kuwa huenda mchezo mzima wa tukio hilo utakuwa umefanywa na baadhi ya wafanyakazi ambao wanaona kwamba wamekuwa hawatendewi haki na uongzozi wa mgodi.

Taarifa zinaeleza kwamba kwa muda sasa kumekuwepo na minong’ono miongoni mwa wafanyakazi ambapo inadaiwa kuwa wafanyakazi wamegawanywa katika madaraja matatu tofauti.
3
Haya Baadhi ya mashimo makubwa yanayochimbwa dhahabu katika mgodi wa Geita

“Humu ndabi sasa hivi hali si shwari sana,wafanyakazi wamewekwa kimadaraja,kuna daraja la juu,la kati na la chini,na kibaya zaidi kuna wanaoongezwa mishahara na wengine ambao hawajaongezwa….’’ Alisema mfanyakazi mwingine na kuongeza.

“Kwa mfano sasa hivi kuna wafanyakazi wengi sana ambao wanaacha kazi na kukimbilia kwenye migodi mingine na hasa iliyoko nje ya nchi….sasa hili linweza likawa pengine haliwafurahishi wafanyakazi wakaamua kufanya tukio kama hilo….’’.

WACHUNGUZI WA NJE WAWASILI

Taarifa za uhakika kutoka ndani ya uongozi wa mgodi huo zimeeleza kuwa tayari wachunguzi kadhaa kutoka nje ya bara la Afrika pamoja na afrika yenyewe kama vile Afrika kusini wamewasili na kufanya uchunguzi juu ya tukio hilo.

Awamu ya kwanza ya wachunguzi kutoka nje ya Tanzania,barani Afrika na nje ya Afrika wameondoka katikati ya wiki hii,na taarifa zinaeleza kwamba awamu ya pili inatarajiwa kuingia mwishoni mwa wiki hii kuendelea na uchunguzi.

“Baada ya uchunguzi kukamilika pande zote zitakutakana na kufanya tathmini ya chanzo ch moto pamoja na hasara iliyotokea,na kisha baadaye itatoa taarifa rasmi kwa uongozi wa mgodi…..’’ kilisema chanzo chetu kutoka ndani ya mgodi huo.

Kamanda wa Polisi Mkoani Geita Leonard Paul alithibitisha kuwepo kwa tukio hilo na kuongeza kwamba wakati vyombo mbalimbali vya ndani nan je ya nchi vikiendelea na uchunguzi,nalo jeshi la polisi itafanya uchunguzi wake kwa sababu ni jukumu lake kufanya hivyo.

2 Comments
  • Doh!!..maskini GGM!!..

    Uchunguzi ufanywe na chanzo kiwekwe bayana. Hii itasaidia kuweza kuepukana na majanga kama haya kwa siku za usoni. Vyombo vya habari navyo vitujuze kwa usahihi bila kuficha ficha ni nini hasa kilijiri kwenye Bohari za GGM?…mpaka moto uzuke namna hiyo?..nijuavyo mimi kwenye Migodi wafanyakazi wote huwa wana mafunzo ya hali ya juu ya kutambua, na kudhibiti Hatari mbalimbali MOTO ikiwa ni mojawapo. Pia huwa maeneo yote ya Migodi yanakuwa na Vifaa madhubuti vya kudhibiti MOTO.

    Kulikoni GGM??..

  • mgawanyo wa mabeberu, mabepari na watwana katika mapato ya rasilimali ya taifa huku mabeberu na mabepari wa kingeni wakiwanyanyasa watwana ambao ni wazawa jambo linalojenga chuki kati yao na inaweza kusababisha ujuma

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *