Mageuzi sekta ya usafiri wa anga, utalii kukuza pato la nchi

Jamii Africa

Tanzania ni miongoni mwa nchi za Afrika yenye vivutio vingi vya utalii lakini kutokuwepo kwa sekta imara ya usafiri wa anga kumeifanya sekta ya utalii kukosa mapato. 

Sekta ya Utalii inachangia sehemu kubwa ya Pato la Taifa na kuzalisha ajira kila mwaka  lakini inaelezwa kuwa sekta hiyo inaweza kukua ikiwa usafiri wa ndege ambazo zinaingia na kutoka nchi utaimarishwa ili kuendana na mahitaji ya watumiaji ambao wanatoka katika nchi zilizoendelea.

Akitoa hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii (2017/2018), Prof. Jumanne Maghembe alisema sekta ya Utalii ni kichocheo cha ukuaji wa uchumi hasa katika sekta za kilimo, mawasiliano, miundombinu, usafirishaji, burudani na uzalishaji wa bidhaa na huduma kwa watalii.

“Aidha katika mwaka 2016/2017 watu laki tano waliajiriwa katika sekta ya Utalii na wengine milioni moja walijiajiri wenyewe katika sekta hiyo. Vilevile sekta ilichangia asilimia 17 ya Pato la Taifa na kulipatia Taifa asilimia 25 ya fedha za kigeni”, alisema Prof. Maghembe.

Licha ya sekta hiyo kuwa na mchango mkubwa katika maendeleo bado mchango wake haulingani na idadi ya vivutio vilivyopo ambavyo havijafikiwa kwasababu ya changamoto za miundombinu ya barabara na usafiri wa ndege.

Usafiri wa anga unaratibiwa na Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) ambalo kwa muda mrefu limekuwa likijiendesha kwa hasara na kukabiliwa na madeni mengi ambayo yamelifanya shirika hilo kutohimili ushindani wa mashirika mengine ambayo yanatawala soko la usafiri nchini.

Mkaguzi  Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Prof. Mussa Assad akiwasilisha hotuba yake Bungeni mwaka 2016 alisema “moja ya changamoto zinazoikabili Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) ni uhaba wa fedha. Changamoto ambayo imelikabili Shirika hili kwa miaka mingi sasa. Kutokana na taarifa za fedha ambazo hazijakaguliwa, nimegundua kuwa shirika limekuwa likipata hasara kwa miaka 9 mfululizo”,

“Mapato ya shirika yamekuwa yakishuka  mwaka hadi mwaka tangu mwa ka 2007. Mfano; kati ya mwaka 2008 na 2013, mapato ya Shirika yalishuka kwa kiwango kikubwa”.

Mlima Kilimanjaro uliopo Kaskazini mwa Tanzania

Ili kulinusuru Shirika hilo, serikali imeamua kulipa madeni yote ya ATCL na kwa sasa amenunua ndege mbili zenye uwezo wa kubeba watu 75 na iko mbioni kuagiza ndege zingine ambazo zinatarajia kuingia nchini mwaka ujao.

Msemaji wa Serikali, Dkt. Hassan Abbasi  emesema Ndege aina ya Q400 ambayo ilitarajiwa kuwasili Julai mwaka huu itawasili Julai mwaka ujao ikiwa ni ndege ya tatu kununuliwa na serikali ya awamu ya tano inayolenga kulifufua shirika la Ndege Tanzania (ATCL).

“Tunanunua ndege nne… kwasababu moja ya malalamiko makubwa sana huko nyuma ilikuwa ni lawama kuhusu shirika letu la ndege kwamba huwezi kuwa na nchi yenye vivutio vyote hivi vya utalii lakini hukuna shirika imara la ndege.

“Kwa hiyo tumeanza hizo juhudi na mimi nasema kufikia mwakani ndege zote za awamu hii tulizoziagiza zitakuja nchini na ndege hiyo uliyoitaja itakuja nchini, iko katika majaribio si kama baiskeli unaweza kufunga tairi na kuanza kutumia,” amesema Dk Abbasi na kusisitiza kuwa,

“Kuna viwango vya kimataifa kufikiwa, ila ninachosema kwa sasa inafanyiwa ukaguzi itakapokamilika itakuja nchini ila kufikia Juni mwakani zile ndege zote. Ile kubwa Boeing 787 yenye uwezo wa kubeba abiria 262 itakuwa imewasili ifikapo Julai mwakani.”.

Kauli hiyo ya Msemaji wa serikali inakinzana na hoja aliyotoa Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu ambaye aliibia mjadala wa kuchelewa kufika kwa ndege hizo akidai kuwa zimezuiliwa nchini Canada kwasababu Tanzania inadaiwa fidia ya Tsh bilioni 87 na kampuni ya ‘Stirling Civil Engineering Limited’ ya Montreal, Canada.

Fidia hiyo inatokana na hatua ya kukiuka mkataba wa ujenzi wa barabara ya Wazo Hill hadi Bagamoyo. Kampuni iliitaka Mahakama nchini Canada kuzuia mali zote za Tanzania zilizomo nchini humo mpaka deni lote lilipwe. Licha ya kucheleweshwa kwa ndege hizo ambazo zitatua katika viwanja mbalimbali duniani, ujio wake utachochea sekta ya utalii na kuiweka Tanzania kwenye ramani ya dunia na kuvutia watalii wengi.

Mchango wa Usafiri wa Ndege kwenye sekta ya Utalii

Kulingana na ripoti ya Baraza la Usafiri na Utalii Duniani (2017) inaeleza kuwa sekta ya utalii ina mchango mkubwa katika maendeleo ya  dunia, ambapo inachangia asilimia 10 (Dola za Kimarekani trilioni 2.2) ya uchumi wa dunia. Pia imetoa ajira milioni 108 duniani kote na inakadiriwa ifikapo 2024 itakuwa imeajiri watu milioni 126.

 Mafanikio ya sekta ya utalii yanachagizwa na uwepo wa usafiri wa ndege, ambapo zaidi ya 54% ya watalii wa kimataifa wanasafiri kwa kutumia ndege. Kwa Afrika inakadiliwa watu milioni 5.8 wameajiriwa katika maeneo ya kupokea wageni kutoka nchi za Magharibi ambao wanatumia ndege. Mwaka 2014, sekta hiyo ilichangia Dola bilioni 46 za Pato la nchi za Afrika.

Hata hivyo, uboreshaji wa miundombinu ya viwanja vya ndege ili kuongeza wigo wa watalii wa kimataifa kutembelea vivutio vilivyomo nchini.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *