Marekani yatishwa na misaada, mikopo ya China inayotolewa Afrika

Jamii Africa

Katika kile kinachotajwa kuwa ni vita ya kiuchumi, Marekani imekosoa mfumo wa utoaji misaada na mikopo wa China kwa nchi za Afrika ikiwemo Tanzania ikidai kuwa unaongeza utegemezi  na  kudumza ukuaji wa demokrasia katika nchi hizo.

Tahadhari hiyo imetolewa na Waziri wa Mambo ya Nje,  Rex Tillerson amesema China inatumia rushwa na mikopo yenye masharti magumu kuzinyonya serikali za Afrika na kuziingiza kwenye madeni.

Akizungumza katika Chuo Kikuu cha George Mason kilichopo Virginia muda mfupi kabla ya kuanza ziara barani Afrika, Tillerson mesema tofauti na Marekani ambayo inahimiza ujenzi wa taasisi imara zinazozingatia demokrasia, utawala wa sheria, uwazi na usalama wan chi husika, China inakiuka misingi ya demokrasia kwa washirika wake.

Hotuba ya Tillerson ilirejea ushirikiano wa karibu wa China na Afrika uliodumu kwa zaidi ya muungo mmoja. Ambapo China imefadhili miradi mikubwa ya miundombinu, ujenzi wa reli na barabara katika nchi za Kenya na kuanzisha viwanda katika nchi za Lesotho, Namibia na Ethiopia. Pia uuzaji wa bidhaa zenye bei nafuu kwa Afrika nako kumetajwa kuua viwanda vya ndani.

Jiji la Beijing linaendesha program mbalimbali za elimu ambapo linawachukua viongozi wa Afrika, watumishi, wanafunzi na wafanyabiashara na kuwapeleka China kwa ajili ya kupewa mafunzo ya uongozi ili kujenga kizazi kipya za viongozi wa Afrika.

Tillerson ameikosoa program hiyo kuwa inalenga kuwajengea waafrika fikra za utawala wa kijamaa ambazo katika ulimwengu wa sasa hazina matokeo chanya kwa maendeleo ya dunia.

 

  

Tanzania nayo imo…

Tanzania nayo imetajwa kuwa miongoni mwa nchi barani Afrika ambayo imefungua milango kutoka China na kuonya kuwa misaada na mikopo ya nchi hiyo inaziweka rasilimali za taifa rehani ikizingatiwa kuwa  misaada  inaambatana masharti magumu ya kiuchumi na kisiasa.

Mwaka 2013 pekee China iliwekeza zaidi ya Dola bilioni 2.17 katika maeneo mbalimbali nchini Tanzania ikiwemo sekta za uzalishaji, uchukuzi, nishati, madini, usafiri, mawasiliano na utalii.

Miradi ambayo inatekelezwa kwa ushirikiano wa nchi hizo mbili ni pamoja na ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo, Kituo cha uzalishaji umeme wa gesi cha Kinyerezi ambacho kiko katika hatua ya III na IV na kinagharimu Dola bilioni 1.

Pia mahusiano ya kibiashara pia yameimarika hasa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita ambapo mwaka 2011 na 2012 biashara ilikuwa ni Dola bilioni 2.1 na bilioni 2.5, na inakisiwa biashara baina ya mataifa hayo mawili itaongezeka zaidi miaka ijayo.

Katika soko la ujenzi,zaidi ya asilimia 70 ya miradi ya barabara na madaraja imejengwa na makampuni ya China. Ni teknolojia yao iliyotukuka na bei nzuri inayolingana na mahitaji ya Watanzania ndio inayofanya makampuni kupata zabuni nchini. Kutokana na hali hiyo kampuni hizo zimeisaidia Tanzania kuokoa zaidi ya asilimia 20 ya miradi yote ya uwekezaji.

Wachambuzi wa uchumi kwa nyakati tofauti, wameitaka Tanzania kutathmini faida na hasara za misaada kutoka China ili kulinda uhuru na rasilimali za nchi.  .

NCHI 10 ZINAZOONGOZA KUPOKEA MISAADA KUTOKA CHINA

 

 

Tatizo liko wapi?

Misaada ya China imekuwa ikilaumiwa kwa kuhimiza tawala za kiimla,ujenzi wa barabara zisizo na viwango na kutumia wafanyakazi kutoka China kujenga miundombinu ili kurahisisha upatikanaji wa mafuta, madini na rasilimali zingine kwa ajili ya viwanda vyake vilivyopo China.

January mwaka huu, kulizuka tetesi kuwa China iliiba taarifa muhimu za kikao cha Wakuu wa nchi za Afrika ambacho kilikuwa kinafanyika katika jengo la Makao Makuu ya Umoja wa Afrika (AU) nchini Ethiopia. Jengo hilo lilitolewa na China kama zawadi kwa bara hilo mwaka 2012.

“Uwekezaji wa China hauna umuhimu wa kutatua changamoto ya miundombinu ya Afrika, lakini mfumo wake umesababisha madeni na  tatizo la ajira”, alisema Tillerson. “Ukijumuisha msukumo wa kisiasa na fedha inahatarisha raslimali za Afrika na uthabiti wa kiuchumi na kisiasa”.

Tillerson ameanza ziara ya kikazi katika nchi za Afrika anakusudia kuweka wazi sera za Mambo ya Nje za Marekani na msimamo wa rais Donald Trump kwa nchi hizo. Anatembelea nchi za Ethiopia, Djibouti, Kenya, Chad na Nigeria ambapo atazungumzia masuala ya ugaidi, utawala bora, biashara na uwekezaji.

Pia ameahidi kuendeleza  program zilizoanzishwa na George Bush na Barack Obama ambazo ‘Power Afrika’, Mfuko wa kudhibiti UKIMWI (PEPFAR) na  mradi wa uongozi YALI.

 Marekani itatoa Dola milioni 533 kwa ajili ya msaada wa Chakula na afya kwa nchi za Somalia, Sudan Kusini, Ethipia, na nchi za  Afrika ya Magharibi na Kati zinazozungunga ziwa Chad.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *