Tusipoandika historia yetu, tusije laumu ikipotoshwa!

Michael Dalali

Wengi wangependa kujua/kusoma wasifu rasmi “biography/autobiography” wa wanasiasa kama Benjamin Mkapa, Dkt. Salim A. Salim (moja ya wanadiplomasia nguli ambaye alipata kuiongoza Umoja wa Afrika katika miaka ya 1989 hadi 2001 kama Katibu Mkuu na pia kuwahi kuwa Waziri Mkuu katika serikali ya Mwalimu Nyerere), wafanyabiashara kama Said Salim Bakhressa, Reginald Mengi, wanazuoni kama Profesa Issa Shivji, Haroub Othman. Wanamichezo kama Filbert Bayi, Leodgar Tenga, n.k. ili kufahamu kwa undani wameweza kufika pale walipofika na kuwa na mchango mkubwa mpaka sasa kwa taifa.

==================================================

Uandishi umekuwa ukipungua siku hata siku katika jamii yetu ya Tanzania, lakini haimaanishi hakuna vya kuandikwa, hakuna mafunzo ya kuwekwa katika kumbukumbu kwa ajili ya vizazi vya sasa na vijavyo! Ni uchaguzi tu ambao wengi wenye taarifa kuamua kutoandika historia ambapo madhara ya uamuzi huu ni makubwa kuliko tabu ya kupitia mchakato wa uandishi.

Ni kweli si kila mmoja ana karama ya uandishi lakini kwa ukuaji wa teknolojia na maendeleo katika tasnia ya uandishi, hata asiye mwandishi anaweza kuandika iwe yeye mwenyewe moja kwa moja au kushiriki katika uandishi pasi kuandika.

Tukiangalia kwa haraka tunaweza kuhoji kwanini hakuna wasifu rasmi “biography/autobiography” za kutosha za watendaji mbalimbali waliopata kushika ofisi za umma hasa ngazi za juu na kutoa mchango mkubwa katika jamii yetu mpaka sasa. Lazima tujiulize, kwani ni kwa kupitia maandiko kama hayo ndipo baadhi ya visa na mikasa ambayo kwao wameipitia inaweza kuwa funzo maridhawa kwa vizazi vya sasa na vijavyo. Kwani ni thamani kuu kujifunza katika yale wengine walianguka au kuyamudu vyema kuliko kusubiri yatukumbe tena ndipo tupate fundisho!

Ni kwa namna gani, mathalani, majaji waliopata kutumikia mhimili wa mahakama kwa muda mrefu na katika safari ndefu mfano wengine walioanzia toka uhakimu ngazi za wilaya mpaka kufikia ngazi hizo za juu kabisa katika mhimili huo wa sheria safari yao ikawa funzo na yenye kuhamasisha hasa kwa wanaoanza fani hiyo. Kwa ukosefu wa maandiko kama hayo, wengi (hasa kizazi cha sasa) wanaweza hisi wanayoyapitia ni mapya au kuyumbishwa na pia na misukumo mbalimbali. Kuna umuhimu mkubwa wa maandiko haya.

Maandiko haya pia hayapaswi kusubiri hadi muda wa kustaafu au uzeeni. Kuna machache ambayo hata vijana wa sasa wameyapitia katika utendaji wao katika fani mbalimbali ambayo yanaweza kabisa kuwa chachu kwa maendeleo na kupiga hatua katika utendaji endapo yangeliandikwa vyema.

Katika mjadala ambao nilipata kuuibua katika mtandao wa kijamii wa ‘Twitter’, wengi wa wachangiaji walionyesha uhitaji sana wa kuandikwa kwa yale ambayo watu wameyapitia au kukumbana nayo katika utumishi au utendaji kazi wao. Na baadhi walidiriki kuonyesha kiu yao ya kutamani kusoma vitabu vyenye kuelezea misimamo safari walizopitia katika taaluma nk baadhi ya watendaji wa kiserikali, watumishi wa umma, wafanyabiashara, wanasiasa nk. Mifano michache ya kiu ya wachangiaji ilikuwa ni kupata bahati ya kusoma wasifu rasmi “biography/autobiography” wa wanasiasa kama Benjamin Mkapa, (aliyepata kuwa Rais wa Tanzania katika serikali ya awamu ya tatu), Dkt. Salim A. Salim (moja ya wanadiplomasia nguli ambaye alipata kuiongoza Umoja wa Afrika katika miaka ya 1989 hadi 2001 kama Katibu Mkuu na pia kuwahi kuwa Waziri Mkuu katika serikali ya Mwalimu Nyerere), wafanyabiashara kama Said Salim Bakhressa, Reginald Mengi, wanazuoni kama Profesa Issa Shivji, Haroub Othman. Wanamichezo kama Filbert Bayi, Leodgar Tenga, n.k. Haya ni kwa uchache tu, ambayo ni kiu kwa wengi kufahamu kwa undani wameweza kufika pale walipofika na kuwa na mchango mkubwa mpaka sasa kwa taifa. Ni kwa njia zipi, ipi ni misimamo yao katika baadhi ya masuala na nini ndoto zao kwa Taifa letu.

-wewe-

Makundi haya yanakwenda mbali pia kwa wale ambao bado wapo katika utumishi wao kwa sasa, mathalani wanasiasa vijana kama; Zitto Kabwe, Halima Mdee, John Mnyika, January Makamba ambao kwa hivi karibuni wamekuwa na mvuto na hamasa kwa vijana wengi katika upande huo. Huku kusanifu pia maisha ya wajasiriamali vijana wenye kumiliki makampuni na kuendesha biashara mathalani Mohammed Dewji. Lakini pia wapo wenye kuhamasisha kutokana na mafanikio ambayo wamepiga katika taaluma na kazi zao kama vile Suzan Mashibe kwenye shughuli za anga, Julie Makani katika sekta ya afya. Ni muhimu kuandika historia sahihi ili isije ikaandikwa ndivyo sivyo!

Tumeshuhudia uandishi kama huo ukifanywa kwa wanasiasa machachari wanaochipukia nchi nyingine mfano Afrika Kusini ambako mwandishi Fiona Forde aliandika kitabu juu ya mwanasiasa Julius Malema; “An Inconvenient Youth – Julius Malema and the new ANC”.

Katika kuhakikisha historia haipotei wala kufutika, kuna wengi walishiriki katika ujenzi wa taifa na katika nyanja mbalimbali na kupitia utendaji wao hata kama hawakuwa maarufu sana ila kuna maamuzi waliyopata kuyachukua yatadumu kuwa funzo vizazi kwa vizazi. Bila ya kuwa makini na mafunzo haya tunakuwa jamii inayorudia makosa yale yale kwa nyakati tofauti.

Tuchukulie mfano katika eneo la usafirishaji wa majini ambalo katika miaka ya karibuni tumeshuhudia ajali za kutisha zenye kuangamiza wananchi wengi. Lakini baadhi ya matukio haya yamekuwa yakichangiwa na uzembe. Uzembe ambao miaka kadhaa nyuma ulishakemewa na kwa nyakati zile ambazo tahadhari ilipuuzwa madhara yalijitokeza. Hakuna uandishi wa vitabu wenye kutunza kumbukumbu hizi na uchambuzi wa kina. Nyaraka nyingi za tume ambazo zinaundwa zinaishia kupata vumbi katika makabati na kuliwa na mchwa. Lakini tungalichapa katika mifumo ya vitabu na kufikika kwa wingi na mwananchi yeyote anayetaka kupata maarifa kutokana nayo tungaliweza kupiga hatua.

Katika kuzama kwa meli au vivuko tunaweza pia kukumbuka sakata mathalani la kuzama kwa kivuko cha Kilombero. Kuzama huko kwa kivuko kulitokea kama ajali lakini inaweza kuwa ni moja ya ajali ambazo ni tarajiwa kwani tayari uamuzi wa kununua kivuko hicho ulipingwa vikali na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Miundombinu kwa wakati huo Marehemu Odira Ongara kwa madai kwamba kivuko kile kilikuwa chakavu na kisingeweza kukidhi vigezo vya manunuzi na hata matumizi na kuamua kutokutia sahihi ununuzi wa kivuko hicho. Uamuzi huu ulipuuzwa na kivuko kikanunuliwa kwa uidhinishaji wa viongozi wengine wa juu zaidi, chini ya waziri Mustapha Nyang’anyi na hatimaye maafa ya kuzama na kuua watu ndilo likawa zao. Kuzama huko na maafa hayo vilizua mjadala mkali sana baadaye. Lakini kwa ufinyu wa kuandika na kusoma, haya yamekuwa yakijirudia, makosa yaleyale yamezidi kutusababishia maafa kwa taifa.

Mfano wa eneo moja la sekta ya usafirishaji wa maji ni chembe tu katika mengi ambayo yameshajitokeza kwenye sekta nyingine ambapo yamekuwa yakijirudia kila uchao pasi kuwa na funzo kwa kizazi cha sasa wala kile kijacho.

Moja ya hatua muhimu kuelekea maendeleo endelevu na ustawi wa taifa lolote ni pamoja na kuthubutu kuandika na kusoma.

Jukumu hili la kuweka kumbukumbu katika maandishi ni la kila mmoja ambaye amepitia mengi ambayo yanaweza kuwa funzo kwa wengine iwe mazuri au mabaya awe ana uwezo wa kiuandishi au lah, kwani kwa wale ambao hawana uwezo wa kiuandishi au muda wa kuwekeza katika kuandika, wanaweza kabisa kushirikiana na wanahabari ambao kwao uandishi ni sehemu ya kazi yenye kuwapatia kipato. Ndiyo inawezekana kabisa, kwani katika nchi nyingi duniani, waandishi wa habari wamekuwa wakitumia fursa ya kuwa karibu na vyanzo vya taarifa mbalimbali kuandika maandiko kama vitabu aidha kwa niaba ya watu ambao wamepitia visa hivyo, au wametenda masuala yenye kuhitaji kuwekwa katika kumbukumbu au pia kuandika tu masuala nyeti kwa kina kwa ajili ya sasa na vizazi vijavyo.

Tunaweza kujiuliza kwa kina kuna sababu gani kwa waandishi wa habari hususani wa makala ambao kwa muda mrefu wameandika na kuchambua masuala ya rushwa katika sekta ya nishati na madini yaani kusanifu mikataba mibovu ambayo imeingia katika historia ya nchi yetu kama ile ya Richmond au Dowans kutokuwa na vitabu juu ya hayo? Ni kwanini tunaruhusu haya yote ambayo tumeyashuhudia yapotee kwenye vichwa vyetu pasi kuandikwa na kuwa funzo kwa vizazi vya sasa (hususan kwa nchi nyingine) na vizazi vijavyo? Kuna sababu yoyote yenye tija katika hili? Au tutashangazwa pale ambapo wataibuka waandishi toka nchi nyingine na kuandikia juu ya hayo kisha tukahamasika na kukimbilia kuyasoma?

Kuna nyakati zenye mafunzo mengi ya kisiasa ambayo endapo yakiachwa yapite pasi kuandikwa vizuri tunaikatili historia yetu, tukichukua mfano mambo ambayo kundi kama vile G55 ambalo lilikuwapo na kusimamia ajenda nyingi za kisiasa kama vile suala la muungano na nafasi ya Tanganyika. Huko walikuwapo wanasiasa na wabunge kama vile Njelu Kasaka, Jenerali Ulimwengu, hawa wote wapo. Mengi waliyopitia ni tija sana katika hali ya kisiasa sasa na hata baadae. Ni funzo sana kwa wanasiasa wa sasa na hata wa baadae. Tunahitaji sana maandiko yao!

Tunaweza kujiuliza kwa wale ambao walipitia michakato ya kisiasa mathalani kushiriki kwa kina na ukaribu chaguzi kama vile za mwaka 2005 na kushuhudia mikakati ya lile kundi lisemwalo la “wanamtandao” wana sababu gani kutoandika mafunzo yale? Ni woga? Au kwa wale ambao walishiriki kwa kina kampeni na michuano ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 na hasa kampeni za upinzani za Dkt. Wilibrod Slaa ambaye alikuwa moja ya mwanasiasa mwenye kugusa mioyo ya wananchi kutoandika tena kwa kiuchambuzi juu ya yaliyojiri kwa kina? Ni woga?

Au tunaweza kujiuliza: Kwanini hakuna uthubutu wa kuandika vitabu juu ya vyama vyetu ambavyo vinaendesha siasa nchini mathalani vyama kama CHADEMA au CUF kwa upande wa upinzani na kile chama tawala cha CCM? Kusanifu ukuaji wake, kuimarika na hata misukosuko ambayo imeshapitia?

Maana jamii yetu inapenda kusoma hayo, na ndiyo maana tunaona baadhi ya wananchi wamekuwa wakinunua vitabu juu ya namna ambavyo siasa za Kenya zimekuwa zikiendeshwa mathalani vitabu kama “Politics of Betrayal” (Siasa ya Usaliti) cha Joe Khamis au kile cha “Peeling back the Mask” cha Miguna Miguna. Hivyo ni miongoni mwa vitabu vya jirani wenzetu ambao wamekuwa wakiandika yale ambayo wanapitia na kuwa funzo kwa sasa na baadae. Achilia mbali nchi zilizoendelea kama vile Marekani ambako baadhi wamekuwa wakisoma vitabu vingi juu ya namna siasa zimeendeshwa mathalani namna Rais wa sasa, Barrack Obama amekuwa akiendesha kampeni zake na hatimaye ushindi katika vitabu maarufu kama kile cha “Audacity to win” cha aliyekuwa meneja wa kampeni za rais huyo Barrack Obama kwa mwaka 2008 bwana David Plouffe.

Hatuwezi kupiga hatua kimaendeleo endapo hata masuala ambayo yapo katika uwezo wetu hatuyatekelezi na kuyapa kipaumbele! Tunasaliti kuandika historia yetu wenyewe hivyo ni fursa baadaye kwa kila yeyote yule anayeweza kunena juu ya hilo kuja na kile anachopenda kisikike. Ukweli hasa wa mambo unapotea na kuachwa upotoshaji uote mizizi!

5 Comments
  • Kaka mdogo Michael, hongera kwa makala nzuri. Cha kuongezea hapa ni kuwa tatizo sio kuandika tu bali kuna tatizo lingine la kutokupenda kusoma vitu serious miongoni mwa watanzania

    Tanzania ya leo haivutii sana mtu kuandika vitabu kwani wasomaji achilia mbali wanunuzi ni wachache mno. Na katika hili ninamfano hai mmoja wa kitabu kizuri chenye mambo mazito lakini sokoni hakijanunuliwa inavyotakiwa nacho ni cha RAI YA GENERALI ULIMWENGU.

    Kuna uhitaji mkubwa wa kuanza kuwahamasisha watoto wetu kujenga tabia ya kupenda kusoma. Na ili kufaniisha hili kunahitajika juhudi zaidi ya za mwalimu na mzazi.

    Mfano kwa Tanzania ya leo kunahitajika kuanzishwa kwa mashindano ya kusoma na kuandika nsha kama yalivyo ya bongo star search, Dume Condom n.k. Kukitokea mashindano kama haya naamini idadi ya watanzania wapenda kusoma na kuandika itaongezeka sana.

  • Nashukuru sana Ndugu Chrispin kwa kuisoma makala yangu na kuchukua wasaa kunipa mrejesho. Ni faraja sana kwa mwandishi yeyote kupokea mrejesho wa kazi yake.

    Ni kweli usemayo kuwa kusoma nako ni tatizo kubwa Tanzania (iwe nje ya mfumo wa kielimu na hata katika mfumo wa kielimu). Naamini si kama swali la "kuku au yai kipi kinaanza". Ninaamini lazima vyote viwepo; uandishi na usomaji kwani vinategemeana kama vile ule msemo wa Shabarn Robert; "lila na fila havitangamani".

    Tunapaswa kuchochea uandishi. Tunapaswa kuchochea usomaji kwa nguvu zetu zote ili kuwa na taifa makini na imara.

  • hongera kwa makala yako nzuri, lipo tatizo la waandishi wa habari na waandishi kutumika katika siasa sasa wanaona wakiandika historia ya fulani hususani ya mwanasiasa watamkuza kisiasa hili ni tatizo, pia waandishi wengi ni wavivu wa kufanya utafiti wanapenda habari nyepesi tu kwa mfano fulani kahama ccm kaenda chadema au fulani kahama chadema kaenda ccm huyo ataandikwa mpaka historia yake. waandshi pokeeni changamoto hiyo.

  • Nashukuru Kaswalala, una hoja. Na lengo hasa la makala ni kututia shime sote (wanahabari na wale ambao si wanahabari) kushiriki kikamilifu katika kuhakikisha tunakuwa na maandiko kwa vizazi vya sasa na hata vizazi vijavyo katika nyanja mbalimbali.

  • saluti kwako.nashindwa hata nisemaje ila tunashida hizi

    ubunifu katika utungaji na ufanyaji wa kazi zao

    bila kusahau uvivu wa Tanzania sas hapo usiwatoe waalimu

    kwasababu walikuwa wanafunzi na ndo wale wale ambao hawakusoma vitabu…nahisi mikakati endelevu, sapoti ya serikali na msukumo wa nafsi ni vitu muhim ili kujitoa katika hili… for change

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *