Waendesha bodaboda wanachangia asilimia 13 ya mimba za utotoni nchini

Jamii Africa
  • Kuna uhusiano gani kati ya bodaboda na ongezeko la mimba za utotoni kwa wasichana wanaosafiri umbali mrefu kwenda shule?

Gazeti la The Guardian la Tanzania, linawaweka waendesha bodaboda kama kiini cha ongezeko la mimba za utotoni nchini Tanzania. Kwa mujibu wa tafiti zilizofanywa hivi karibuni, waendesha bodaboda wanachangia asilimia 13 ya mimba za utotoni nchini.

Matumizi ya bodaboda, ama pikipiki kwaajili ya biashara, yameongezeka sana nchini Tanzania hasa pale ambapo ni ngumu kupata usafiri mwingine. Umaarufu wake unasababishwa na upatikanaji mgumu wa usafiri pamoja na bei nafuu za pikipiki; na huwa zinaendeshwa na vijana wadogo waliotoka kumaliza tu elimu ya sekondari.

Kwa mujibu wa utafiti huo, wasichana wadogo, hasa wale wa vijijini, wako katika mazingira hatarishi zaidi kushawishika kingono kwasababu inawabidi kusafiri umbali mrefu kwenda shule. Gazeti la Financial Times linasema, baadhi ya wasichana huishi umbali wa hadi kilometa 15 kutoka shuleni, hivyo huwalazimu kupanda bodaboda badala za kutembea umbali huo.

Kwakuwa hawana fedha za kutosha kuwalipa waendesha bodaboda hao, huishia kulala nao kama njia ya malipo. Wanapopata ujauzito kwa jinsi hii, huishia kufukuzwa shuleni.

 

Swali hapa ni je, mimba ngapi za utotoni ambazo zinasababishwa na waendesha bodaboda nchini Tanzania?

PesaCheck imefanya uchunguzi na kubaini ya kwamba, madai ya kuwa waendesha bodaboda wanachangia ongezeko la mimba za utotoni Tanzania ni kweli kwa kiasi kikubwa kwa sababu zifuatazo:

Utafiti wa Taifa kuhusu Vichocheo na Madhara ya Ndoa za Utotoni nchini Tanzania, unafafanua kwamba wasichana kutoka kaya masikini ni kundi hatarishi kwasababu ya hali yao ya kiuchumi. Kukosa mahitaji yao ya msingi, kama kuweza kulipia usafiri, kunawafanya iwe rahisi kunyanyaswa kingono.

Ni ngumu kujua idadi kamili ya mimba zilizosababishwa na waendesha bodaboda. Lakini, kilicho bayana ni kwamba wasichana waishio vijijini nchini Tanzania ni kundi hatarishi la kunyanyaswa kingono na watu wanaohusika na usafiri sehemu mbalimbali nchini.

Watoto wengi hukumbana na changamoto mbalimbali wanapokuwa njiani kwenda na kutoka shule. Baadhi ya makondakta hukataa kuwachukua kwasababu wanalipa nauli ndogo. Safari ya kwenda na kutoka shule huwaweka watoto katika mazingira hatarishi. Ripoti ya “Ukatili Dhidi ya Watoto Tanzania” inaonyesha kwamba kati ya wasichana wanne waliotoa taarifa ya kufanyiwa ukatili wa kijinsia, mmoja kati yao ilimtokea akiwa anaenda shule, aidha kwa usafiri wa umma au akiwa anatembea.

Kwa mujibu wa Ripoti ya Ukatili Dhidi ya Watoto Tanzania (2011), msichana 1 kati ya 25 mwenye umri wa miaka 13 hadi 17 amewahi kupewa pesa au zawadi ili afanye ngono. Ripoti hii inaonyesha kwamba asilimia 23 ya wasichana wananyanyaswa kijinsia wakiwa wanaenda au kutoka shule.

Hivyo, madai ya kwamba waendesha bodaboda wanachangia ongezeko la mimba za utotoni nchini Tanzania ni kweli kwa kiasi kikubwa. Kuna ushahidi unaoonyesha kuwa wasichana wanaotoka kwenye kaya masikini, hasa walioko vijijini, wanapata shinikizo kubwa kulipia usafiri wao kingono. Kwa kuwanyanyasa wasichana hao, waendesha bodaboda huwaongezea ugumu ambao tayari wanao.

Matokeo yake, maamuzi ya kuwafukuza shule wasichana waliopata ujauzito huleta matokeo hasi. Kunawafanya wakose nafasi ya kupata elimu ambayo wangeihitaji kujikwamua na umasikini. Hivyo, huwaweka katika hali hatarishi zaidi.

 

Makala hii imeandikwa na PesaCheck Fellow Belinda Japhet, Mwandishi na Mshauri Mtaalamu wa maswala ya mawasiliano.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *