Bunda walalamikia miundombinu ya Zahanati yao

Frank Leonard

WATOA huduma wa zahanati ya Bunda, wilayani Bunda mkoani Mara wameilalamikia miundombinu mibovu ya kituo hicho kwamba inaathiri utoaji huduma.

DSC08315
Zahanati ya Bunda

“Ofisi ya mganga inatumika pia kuhifadhi dawa, chumba cha mapokezi na sindano havina madirisha” Mganga Msaidizi Victoria Awino alisema.

Alisema Zahanati hiyo yenye watoa huduma watano tu pamoja na kuelemewa na mzigo wa wateja wengi, haina nyumba hata moja ya mtumishi.

Alisema kwa wastani zahanati hiyo inahudumia wateja 30 na 40 kila siku, jambo linalosababisha wafanye kazi baada ya muda wa kazi na siku za mapumziko.

Akizungumzia huduma ya afya ya uzazi, Awino alisema kwa mwaka jana pekee ilitoa huduma kwa wajawazito 1,692 na kati yao 32 walikuwa na maambukizi ya virusi vya Ukimwi (VVU).

“Wengi wa wajawazito hao walikuja na waume zao wakati wakihudhuria kliniki kwasababu walitakiwa kwa pamoja kupima maambukizi ya virusi vya Ukimwi,” alisema.

Hata hivyo alisema vitendanishi vya kupima VVU vinapunguza hamasa ya akina baba kuhudhuria kliniki na waume zao.

“Tunaomba serikali ijitahidi sana kufikisha vitendanishi hivyo kwa wakati ili kuboresha huduma ya afya ya uzazi kwa mama, mtoto na baba,” alisema.

Katika kutekeleza sera ya afya ya mwaka 2007 inayotaka makundi maalumu wakiwemo wajawazito na watoto chini ya miaka mitano wapate huduma bure, Awino alisema vifaa kama beseni la kuogea, sabuni na mipira ya kuzalia hutakiwa kununuliwa na wahusika.

“Vinavyopatikana mara chache na kutolewa bure katika zahanati hii ni pamoja na mipira ya kuvaa mikononi, dawa za kuzuia damu, bomba za sindano na mkunga,” alisema.

Pamoja na kutoa huduma kwa wajawazito, Awino alisema huduma ya kuzalisha wajawazito hao hufanywa kwa dharula zahanati katika hiyo kwasababu hushauriwa waende hospitali teule ya wilaya ya Bunda (BDDH).

Muuguzi Mkuu wa Wilaya ya Bunda, Aderaida Masige alisema katika kuboresha huduma, serikali iko mbioni kuitanua zahanati hiyo ili iwe na hadhi ya kituo cha afya.

“Na kituo pekee cha afya cha serikali cha Manyamanyama kilichopo mjini Bunda kimekuwa hospitali ya wilaya na ili kufikia hadhi hiyo, miundombinu yake inaendelea kuboreshwa,” alisema.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *