Siri iliyofichika mauaji ya wanandoa nchini

Jacob Mulikuza

Hivi karibuni tumeshuhudia matukio kadhaa ya vifo kwa wanandoa, aidha mume kumuua mke wake au mke kumuua mume wake.

Ni matukio ya kusikitisha ambayo yameripotiwa sehemu mbalimbali Tanzania ikiwemo Mkuranga, Pwani, Dodoma and Tabora. Mauaji haya yamezua maswali mengi huku kila mmoja akitoa tafsiri yake kwa namna anavyoiona hali.

Nimesikiliza maoni ya watu mbalimbali wakijaribu kudadavua ni kitu gani kimetokea mpaka vifo hivi vimetokea; maoni mengi yamekuwa ni kukosa hofu ya Mungu na wengine wakiamini ni nguvu za kishirikina.

Ningependa kutoa maelezo ya kitaalamu kwa nini matukio haya hutokea na nini kifanyike kuzuia aina hii ya matukio kutokea katika ndoa zetu.

Nianze kwa kusema taaluma yangu ni sayansi ya jamii ambayo nimejikita katika Saikolojia ya Binadamu (Human Psychology) na Ushauri Nasihi (Counseling). Naamini kwa taaluma hii niko sehemu sahihi kueleza tatizo hili.

Mauaji kwa wanandoa sio swala jipya duniani na pia linatokea kwa kiwango kikubwa kila mwaka. Dk. Aaron Ben-Zeeve katika kitabu chake In the Name of Love: Romantic Ideology and its Victims cha mwaka 2008 anaeleza kuwa takriban asilimia 40 ya wanawake huuawa na waume zao na asilimia 6 ya wanaume huuawa na wake zao kila mwaka duniani.

Takwimu hizo zinadhihirisha wazi kuwa tatizo kubwa liko kwa wanaume kuliko wanawake. Sababu zifuatazo zinaweza kueleza chanzo cha tatizo hili:

Niweke wazi kwamba, sababu za mauaji kutokea ni mchanganyiko wa mambo mengi kwa wakati mmoja, hivyo sababu nitakazozieleza hapa hazina maana ndiyo hizo tu bali zitatoa mwanga kwanini tatizo hutokea.

Nikianza kwasababu za kijamii, makuzi ya watoto wa kiume na watoto wa kike ni tofauti sana karibu jamii zote duniani. Jamii nyingi duniani humkuza mtoto wa kiume na kumfanya kujua yeye ni shujaa, mlinzi na kuwa yuko juu ya mwanamke.

Wanaume wengi tunajiona wajasiri, wenye nguvu na wanawake wako chini yetu hivyo tunaweza kufanya lolote kwao.

                                    Wanaume wengi tunajiona wajasiri, wenye nguvu na wanawake wako chini yetu

Makuzi haya ya jamii yanakwenda moja kwa moja kushawishi saikolojia ya mwanaume, hata katika ndoa. Mwanaume huonesha nguvu zake kwa mwanamke (Masculinity). Hivyo kunakuwa na mpaka baina ya mwanamke na mwanaume.

Hapa tunashuhudia matukio ya mara kwa mara ya wanaume kupiga wake zao kila kukicha. Hii halitokei bahati mbaya kwani makuzi ya jamii yameshawishi saikolojia ya mwanaume na kumfanya mwenye nguvu na anaweza kusahihisha kosa la mwanamke kwa kutumia nguvu na sio mjadala au mazungumzo.

Mjadala kwa wanaume ni dalili ya udhaifu na hii ni dalili ya kuwa na matatizo ya kisaikolojia.

Nitoe mfano mdogo tu, binti mwenye umri wa miaka 21 akitaka kwenda dukani usiku anaogopa sana, ila akisindikizwa na mtoto wa kiume mwenye umri wa miaka 7 anajisikia amani kabisa na uoga hutoweka.

Saikolojia hii inaruhusu amani kwenye mwili wako kwa kuwa tayari mapokeo ya jamii yamekuaminisha kuwa mwanaume ni mwenye nguvu na mlinzi.

Nikigeukia katika upande wa pili wa saikolojia unaochangia vifo kwa wanandoa. Binadamu wote tumeumbwa na nafsi mbili (personality) ambazo ni nafsi imara (strong personality) na nafsi dhaifu (weak personality).

Mtu mwenye nafsi imara ni yule anayeweza kupata msukosuko katika maisha, akaumia ila asikate tamaa akakubali mabadiliko na kuwa tayari kuishi nayo na kufanya vyema zaidi hapo mbele.

Lakini mtu mwenye nafsi dhaifu ni yule anayepitia msukosuko akaumia, akakata tama, akashindwa kuishi na mabadiliko na kuona hakuna namna ya kuendelea kuishi na mabadiliko hayo.

Wengi wetu tumepita huko na tunazidi kupita katika hizi nafsi mbili. Kwa maelezo hayo wanaume wengi wanaoishia kuwauwa wanawake zao mara nyingi wanakuwa na nafsi dhaifu ambazo huwaonyesha wako katika hali mbaya na hawawezi kutoka hapo walipo.

Wivu wa mapenzi ni sababu ya mauaji ya wanandoa

Nafsi hii hujidhihirisha kwa mapenzi waliyonayo kwa mwanamke husika kwamba ni mazito mno hivyo yanawapelekea wafanye vitu vya hatari.

Tafiti nyingi za saikolojia zinaonesha wale wanaowauwa wake zao husikika wakisema; nilimpenda sana huyu mwanamke kaniumiza, ama yeye ndio alikuwa nuru ya maisha yangu, kaififisha, ama wengine husema ni kwa sababu ya mapenzi ndio maana nimefanya haya.

Japo utetezi wa mapenzi hapo juu haukubaliki kisaikolojia ila tafiti zinaonesha nafsi dhaifu inayoandamwa na msongo wa mawazo wa muda mrefu humfanya mtu kupanga tukio la mauaji kwa kuwa haoni kama kuna njia mbadala zaidi ya kifo.

Kwa ufafanuzi zaidi, msongo wa mawazo (stress) hutokana na hali ya mazingira yanayokuzunguka kutokuendana na matarajio ya ubongo wako. Mfano, ulitegemea mpenzi wako ni mwaminifu (hali ya ubongo wako) ila ukamkuta na mtu mwingine (hali ya mazingira) hapo msongo wa mawazo hutokea kwani hakuna usawa baina ya ubongo na mazingira yako.

Kwa mantiki hii ni kwamba, kuweza kuwa na nafsi imara ni lazima tujifunze namna ya kufanya hivyo kwa kuwaona wataalamu wa saikolojia na ushauri nasahi. Ama wakati mwingine, kuzungumza na watu wenye uzoefu na jambo ambalo unalipitia kama vile wabobezi katika maswala ya ndoa, biashara, elimu na mengineyo.

Mantiki hapa ni kwamba, wakati mwanadamu anapokuwa na tatizo lazima apate suluhisho, sasa kwenye suluhisho hapo maamuzi ndipo hutofautiana kwa wengine huona ni mwisho wa dunia na wengine huona mwanga mwisho wa safari.

Nini kifanyike katika hali kama hii? Nitaeleza kwa uchache japo suluhisho linaweza kuwa la aina mbalimbali, ila kitaalamu ningeshauri tufanye hili:

Ndoa ni taasisi kama ilivyo taasisi nyingine, inahitaji ujuzi, uvumilivu, utashi na uelewa. Misukosuko ya ndoa ni mikubwa kwa kuwa inahusisha hisia hivyo hata namna ya kuitatua inahitaji hisia imara hususani nafsi imara kuweza kuliendea tatizo kwa umakini.

Kitu kikubwa ambacho tunaweza kufanya kama wanandoa, tujenge tabia endapo matatizo yanakuwa makubwa tuende kuwaona wataalamu wa ushauri nasahi ama wanasaikolojia ambao wamefunzwa namna ya kufanya kazi na msongo wa hisia (Emotional Stress).

Wataalamu hawa hutoa maelekezo ambayo yanaweza kumjenga mtu na kufanya nafsi dhaifu kuwa imara.

Kwa wale ambao wanaona ni gharama kwenda kwa wataalamu wa saikolojia na ushauri nasahi waende kwa wanandoa wakongwe waliokaa kwenye ndoa kwa muda mrefu wanaweza kuzungumza na kuweza kumfanya mtu aone kuna mwanga mwisho wa safari badala ya kukata tamaa na kuchukua maamuzi magumu ya kumuua mwenzi wako.

Nihitimishe kwa kusema, saikolojia ya mwanadamu yeyote yule inahitaji matunzo na matibabu ya mara kwa mara kama vile mwili wa binadamu unavyokwenda kwa tabibu kupimwa na kupatiwa dawa. Wengi wetu hupuuza umuhimu huu na mwishowe tunatenda mambo mabaya bila kujua tu wagonjwa.

1 Comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *