Ubakaji, ulawiti watoto usifumbiwe macho Kinondoni

Jamii Africa

Na Daniel Samson

Kulingana Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 sehemu ya pili (II) inatoa wajibu na majukumu ya mzazi katika kumlea mtoto ambapo inaeleza kuwa “Kila mzazi atakuwa na wajibu na majukumu yaliyowekwa ama na sheria au vinginevyo kwa mtoto wake ambayo yatajumuisha wajibu wa kumlinda mtoto dhidi ya utelekezwaji, ubaguzi, vurugu, unyanyasaji, madhara ya kimwili na kiakili na ukandamizaji”

Ni tofauti na matakwa ya sheria, wako baadhi ya wazazi ambao wanawafanyia watoto wao ukatili wa aina mbalimbali na kukiuka jukumu la msingi la kuwalinda na kuwatengenezea mstakabali mzuri wa maisha.

Lucy (4) (jina hilo sio halisi) ni miongoni mwa watoto wengi duniani ambao wamefanyiwa ukatili wa kijinsia na watu ambao wanapaswa kuwalinda na kuhakikisha wanakuwa na furaha wakati wote.

Lucy alibakwa na baba yake mzazi aliyetambulika kwa jina la Clement (40) (jina la pili tumelihifadhia). Tukio hilo lilitokea kata ya Bunju B wilaya ya Kinondoni ambapo alimsababishia maumivu makali sehemu zake za siri.

“Baba aliniingiza vidole huku chini, amekuwa akinifanyia muda mrefu. Aliniingiza chumbani akanilaza kitandani na kufungua zipu na kutoa dudu”,amesema Lucy na kuongeza kuwa baba yake alimuingilia nyumbani kwao Bunju B ambako wanaishi kwenye nyumba ya kupanga.

Akihojiwa na mwandishi wa makala haya Lucy amesema baba yake alimkataza kuwa asimuambie mtu yoyote lakini maumivu yalipozidi alimwambia mama yake aitwaye Beatrice (jina la pili tunalihifadhi kwa ajili ya usalama)

Beatrice anasema aligundua kuwa mtoto wake ameingiliwa wakati akimuogesha ambapo alikuwa akilalamika kwamba anapata maumivu sehemu za siri.

“Nilimuuliza tatizo nini lakini hakuniambia akabaki analia na kuonyesha sehemu zake za siri”, amesema Beatrice na kuongeza kuwa alimuita mama Vena ambaye wanaishi pamoja katika nyumba yao ambapo walimchunguza na kukuta ameharibiwa sehemu zake za siri.

“Nikampandisha juu ya kiti nikwambia wapi panauma? Ebu nionyeshe akapanua miguu. Nikamuuliza mbona uko hivi kuna tatizo gani huku mbona kuna damu, kulikuwa na michubuko, maana kulikuwa kwekundu kote…”, Amesema Mama Vena.

“Nikamuuliza  mbona uko hivi umefanyaje? Akaniambia baba amefanya hivi, baba alifungua zipu akatoa dudu akaingia huku”, amebainisha Mama Vena.

Anasema usiku huo huo, aliambatana na Beatrice hadi kwa kaka yake (Clement) ambaye anaishi mtaa wa Idara ya Maji kata ya Bunju B ili wasaidiwe kumkamata mtuhumiwa. Walifanya kikao ambapo walianza kumtafuta Clement ambaye tayari alikuwa ameondoka nyumbani baada ya kutekeleza unyama huo.

Familia hiyo haikutaka kulifikisha suala hilo kwenye vyombo vya dola na ili kumnusuru mtuhumiwa. Inaelezwa kuwa msimamo huo wa familia ulipata nguvu kwasababu Beatrice, mke wa Clement ilikataa kumfikisha mme wake polisi kwa kuhofia kukosa matunzo.

Mama Vena anasema siku tatu baada ya tukio hilo alitoa taarifa kwenye ofisi ya serikali ya mtaa wa Idara ya Maji na kutaka suala hilo lifikishwe polisi.

 Lucy aliyefanyiwa udhalilishaji wa kingono na baba yake mzazi

 

 Kesi yafikishwa Polisi

Kutokana na shinikizo la majirani, Beatrice, aliripoti tukio hilo kwenye kituo cha Polisi cha Mabwepande ambako huko jalada la kesi ya ubakaji lilifunguliwa Novemba pili 2017.

Beatrice alipewa Fomu ya Polisi (PF3) ambapo alimpeleka mtoto huyo hadi hospitali ya Mwananyamala iliyopo Wilaya ya Kinondoni kwa ajili ya vipimo.  Alionana na daktari na Lucy alifanyiwa vipimo viwili, cha Maambukizi ya virusi vya UKIMWI na kile cha kuingiliwa kimwili.

Majibu ya daktari  yalionyesha dhahiri kuwa mtoto huyo amenajisiwa na sehemu zake za siri zimeharibiwa na majibu ya kipimo cha maambukizi ya UKIMWI yamefanywa kuwa siri ili kutoharibu upelelezi wa kesi hiyo ambayo iko polisi.

Siku hiyo hiyo aliwasilisha majibu hayo kwa Mkuu wa Kituo Cha Polisi Cha Mabwepande, ambapo majibu yalipokelewa kwa ajili ya ushahidi. Upelelezi wa tukio hilo unaendelea ili kumkamata mtuhumiwa Clement ambaye alitoroka kusikojulikana baada ya kupata taarifa kuwa anatafutwa na polisi.

 

 Ukubwa wa Tatizo la ubakaji

Katika kuangazia ukubwa wa tatizo la ubakaji katika Manispaa ya kinondoni, Chama Cha Wanahabari Wanawake  (TAMWA), kimeshirikiana na mwanadishi wa makala haya ili kuibua na hatimaye kutoa suluhu juu ya njia sahihi ya kukomesha vitendo hivi.

Kwa mujibu wa takwimu za Jeshi la Polisi Tanzania (2016) zinaonyesha kuwa katika kipindi cha miezi saba ya kwanza ya mwaka 2016 yaani kuanzia Januari hadi Julai, Kinondoni ambayo Kipolisi ni Mkoa ilikuwa inaongoza kwa kuwa na kesi 187 za ubakaji katika kipindi hicho huku ikifuatiwa na Mbeya (177), Morogoro (160),  Pwani (159), Temeke (139) na Ilala (109).

Pia Takwimu za Jeshi hilo zinaonyesha kuwa matukio ya ubakaji nchini Tanzania yameongezeka kutoka 6,985 mwaka 2016 na kufikia matukio 7,460 mwaka 2017 na ongezeko hilo ni asilimia 6.8.  Makosa ya kunajisi yalikuwa 16 kwa mwaka 2016 na yaliongezeka hadi kufikia 25 mwaka uliofuata

Kinondoni inatajwa kuwa na matukio mengi ya ubakaji kwa sababu kuna mwamko wa watu kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia ikiwemo kuwaripoti  watuhumiwa wa vitendo hivyo ili wachukuliwe hatua za kisheria.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Ali Hapi ameitaka jamii kushirikiana na vyombo vya dola kwa kutoa taarifa sahihi za matukio ya ubakaji, “ Jeshi la Polisi limejipanga ili kila aliyepatikana na hatia ya ubakaji achukuliwe hatua”.

 

Ustawi wa Jamii

Mshauri na Mtaalamu wa Saikolojia kutoka Taasisi ya Ustawi wa Jamii Tanzania, Zainabu Rashidi amesema ubakaji una athari nyingi kwa watoto ambapo zinaweza kuendelea hadi ukubwani.

Amesema mtoto aliyebakwa hujiona duni na mpweke na hufikia hatua ya kujitenga na kuogopa kucheza na wenzake kwa sababu jamii humnyooshea kidole ambapo hujiona mwenye hatia.

“Athari kubwa ni kwamba mtoto anakuwa mnyonge, mpweke na anakosa hamu ya kushiriki na wenzake katika mambo mengine kwa sababu vitendo vya ubakaji katika jamii vinatafsiriwa kama aibu na unyonge. Na haijalishi mtoto amebakwa na nani? Jamii huanza kumnyoshea kidole kwamba Yule mtoto alibakwa”,  amesema Mtaalamu huyo na kuongeza kuwa,

“Anapokuwa mtu mzima anaendeleza tabia ambazo ni mbaya, anaweza kufanya vitendo vya kikatili, kulipiza kisasi, kumchoma mtoto mikono na mwingine anaweza kufikia hatua ya kuchanganyikiwa”.

Ameitaka jamii kujenga utamaduni wa kutoa taarifa na kuwasaidia waathirika wa ubakaji kwa kuwapeleka Ustawi wa Jamii ili wapate tiba ya kisaikolojia na kurejea katika hali ya kawaida.

                                            Beatrice, mama wa Lucy  aliyebakwa na baba yake mzazi

 

Msimamo wa Serikali dhidi ya Ukatili

Serikali kupitia Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt Faustine Ndungulile ameitaka jamii kutoyafumbia macho matukio ya ubakaji aidha inapaswa kutoa taarifa ili watuhumiwa wachukuliwe hatua za kisheria.

“Kupaza sauti katika kupinga ukatili wa kijinsia na kuondokana na utamaduni wa kukaa kimya dhidi ya vitendo vya kikatili na madhara yake yanamgusa kila mmoja katika ngazi tofauti”, amesema Dkt. Ndungulile.

Hata hivyo, Serikali imezifanyia maboresho Sera na Sheria ikiwemo  Sheria ya Elimu sura 353 ambayo inatoa adhabu ya kifungo kisichopungua miaka 30 kwa mtu yeyote atakayembaka na kumpa mimba mwanafunzi wa shule ya Msingi au Sekondari.

Pia Serikali imeanza utekelezaji wa Mpango Kazi wa Taifa wa kutokomeza Ukatili dhidi ya wanawake na watoto unaojumuisha sekta zote zinazohusu wanawake na watoto kwa lengo kuzuia aina zote za ukatili.

 

 Nini Kifanyike?

Ili kupunguza au kuyamaliza matukio haya, jamii inapaswa kuacha tabia ya kuwalinda wabakaji lakini wanatakiwa kuwafikisha kwenye vyombo vya dola ili wachukuliwe hatua za kisheria.

Pia kuboresha sheria na sera ikiwemo Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 ambayo inatoa mwanya kwa watoto kuolewa katika umri mdogo. Mabadiliko hayo yaambatane na mikakati ya kitaifa ya kuwalinda watoto dhidi ya vitendo vyote vya ukatili ukiwemo ubakaji na ulawiti.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *