‘UBESHI’: Safari ya Vijana Kuifikia Almasi Mwadui-Shinyanga

David Azaria

MAJUZI nilikuwa katika utafiti wa namna gani Madini ya Almas yanayopatikana katika Mji Mdogo wa Maganzo Wilayani Kishapu mkoani Shinyanga umewanufaisha wananchi wanaozunguka Mgodi wa Almasi wa Mwadui.

Eneo la Maganzo linaelezwa kuwa na Almasi lukuki ambayo inachimbwa hadi ndani ya nyumba za watu,lakini maisha ya wananchi wa eneo hilo hayafanani na maelezo yanayotolewa kuhusiana na historian a eneo hilo,napengine unaweza kusema kwamba maisha yao hayaendani na Almasi inayochimbwa kwenye eneo hilo.

Ukipita katika maeneo mengi ya wakazi wa maeneo ya vijiji vinavyozunguka mgodi huo utakumbana na mashimo makubwa yaliyochimbwa wakati wa kutafuta Almasi,lakini wa kwa sasa wanasema mashimo hayo hayana mali tena,namahali pekee ambapo kunaonekana kuwa na Almasi nyingi ni eneo la mgodi.

Kwenye maeneo mengine tofauti na kwenye mgodi ni lazima utakuta ni makazi ya watu,na kinachofanyika ni kwamba Almasi ikiibuka katika eneo la makazi ya mtu kinachofanyika ni kuweka uzio na shughuli za uchimbaji kuendelea ndani.

Safari yangu ya kwenda Maganzo inaanzia Jijini Mwanza ambapo majira ya saa 2 asubuhi nikiwa na Gari Dogo aina ya Noah nawasili Maganzo majira ya saa 4:30.

Baada ya kufika Maganzo natafuta nyumba ya kulala wageni ambazo kimsingi si nyingi sana ni za kuhesabu,moja,mbili,tatu,nne,tano,ambazo zote ziko pembezoni mwa barabara kuu ya Mwanza-Shinyanga katikati ya Mji huo.

Vijana wanaonekana ni wengi katika mji huu,ni wenye umri wa kati ya miaka 15-35,muda mwingi wanaonekana kutembea makundi makundi,lakini hata kama wameketi basi watakuwa ni makundi makundi.

Ni vijana ambao ukiwaangalia unabaini moja kwa moja kwamba wanaishi katika maisha ambayo si mazuri,ni watu wa kutangatanga wasijue ni wapi mahali pa kwenda na hasa pa kufanya kazi walau kwa ajili tu ya kujipatia kipato cha kuendesha maisha yake.

Wanaonekana ni watu waliokata tamaa ya maisha,na kilichobaki ni maisha ya kubangaiza tu,na ndiyo maana sasa kazi yao kubwa ni kuingia ndani ya Mgodi wa Williamson Diomond!,huko ndani si kwamba wakiingia lazima wapate,kuna kupata au kukosa.

Si hivyo tu.huko ndani kuna mbwa wakali,kuna walinzi,kuna polisi,kuna kila aina ya ulinzi ambapo mwisho wa siku ukikamatwa,hali yako inakuwa tete,kuna kuuawa ama kujeruhiwa vibaya kama si kupewa kilema cha maisha pale unapokuwa umenusuru roho yako.

Ukitizama kwa harakaharaka wakazi wa mji huu maendeleo yao si ya juu sana,yanaonekana ni ya wastani,lakini wanakabiliwa na tatizo kubwa la Njaa,wanapoishi ni pembezoni tu mwa mgodi wa Mwadui ambapo kunazalishwa Madini ya Almasi ndilo eneo pekee linalotoa madini haya hapa nchini na katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Kiukweli maisha waliyo nayo si sawa na Almasi inayozalishwa kutoka katika eneo hilo walipo ambapo ni makazi yao,na hasa ikizingatiwa kwamba Almasi imeanza kuzalishwa kwenye eneo hilo tangu miaka ya 50,wakati huo wakiwepo wakoloni,lakini na wananchi wakiwepo kwenye eneo hilo ambao kimsingi hasa ndio waliogundua uwepo wa Almasi.

Kisha majira ya saa 10 jioni najimwaga mitaani na kupita katika makundi kadha wa kadha nikijaribu kuperuzi maisha ya wakazi wa eneo hilo kwa ujumla,moja linalonishangaza ni kwamba pamoja na kwamba katika mji wa Maganzo kuna watu wa kutosha lakini ukiwa mgeni ni rahisi kutambulika.

Moja ya mambo yanayonivutia ni maneno mawili ya UBESHI na NG’ANA ambayo ni vigumu dakika tano kupita bila kulisikia likitamkwa na baadhi ya wakazi wa eneo hilo na hasa vijana wenye umri kati ya miaka 15-35.
1
Baadhi ya vijana wakichenjua mchanga wenye Madini ya Almasi katika kijiji cha Maganzo.

Vijana wenye umri huu ni wengi katika mji wa Maganzo ambapo nalazimika kuketi kwenye moja ya vijiwe vya kahawa katikati ya mji huo na kuanza kusikiliza maongezi yanayoendelea kwa watu waliokuwa kwenye kijiwe hicho.

Neno UBESHI linazungumzwa sana naamua kutoa fedha taslimu shilingi 2000 na kuweka mezani huku nikimuomba mzee kuhakikisha wale wote walioko kwenye kijiwe hicho wanatumia fedha hiyo kwa kunywa kahawa.

Najikuta napata marafiki ghafla kwenye kijiwe hicho akiwemo mzee huyo ambaye ni maarufu kwa jina la Mzee Ally na hapo Napata nafasi ya kupenyeza swali langu juu ya maana halisi ya neno UBESHI,cha ajabu kila mmoja aliyepo pale anataka kunijibu.

Mzee Ally anasema UBESHI ni neno linalotumiwa na vijana wanaokwenda kuiba mchanga wa Almasi ndani ya mgodi wa Mwadui na kwenda kuosha na kupata Almasi ambayo wanakwenda kuuza na kupata fedha za kujikumu.

Anasema neno hilo lilianza kutumiwa kwenye miaka ya 1960 baada ya kuwa wakazi wa eneo hilo wanazuiwa kuingia ndani ya mgodi huo wakati huo ulinzi ukiwa chini ya askari wa Kikoloni,ambao walikuwa wanawakamata wezi wa mchanga huo na kuwafikisha kwenye mahakama ambayo moja iko hapo Maganzo na nyingine iko kwenye kijiji cha Mwadui-Lohumbo (Utemini).

“Tulikuwa tunakamatwa sana,kwa sababu hata mimi nilikuwa ‘M-BESHI’ na niliwahi kukamatwa mara nyingi tu na askari wa kikoloni lakini hatukuacha kwa sababu tulikuwa hatufungwi mara nyingi tulikuwa tunapatiwa adhabu ama kucharazwa viboko…..’’anasema Mzee huyo na kuongeza kuwa hakuna mzee hata mmoja ambaye ni mzaliwa wa eneo hilo ambaye hakupitia UBESHI.

Anaongeza “Baada ya kuona hivyo na kwa sababu tulikuwa mara nyingi tunakaa na wapelelezi ambao ni walinzi waliokuwa wakivaa kiraia na kukaa na sisi mitaani,tuliamua kubuni majina ya kutumia ili iwe vigumu kwa askari kubaini tunachokizungumza hata kama yupo…’’.

Anasema waliamua kutumia neno UBESHI linalotokana na Ndege mmoja aitwaye Kipanga anayenyakua vifaranga ama hata ndege wenzake kama amezubaa na kumla,na pia wakamua kuiita alamasi NG’ANA ili kuficha uhalisia wake.

“Kwa hiyo kuanzia hapo tuikuwa na uwezo wa kupanga mikakati yetu hata mbele ya askari juu ya namna ya kwenda kuiba mchanga wa Almasi Mgodini,bila hata wao kutustukia,na tulifanikiwa sana na jina hilo limedumu hadi sasa na kuonekanan kama ndio majina halisi…’’ anasema na kuongeza.

“Ndiyo maana hapa ukiuliza Neno Almasi kwa mfano wale wafanyabiashara huwezi kupata,isipokuwa unatumia neno NG’ANA….’’.

Anasema ilikuwa ni vigumu sana kwa walinzi wa kikoloni kubaini mipango waliyokuwa wakifanya namna ya kwenda kuiba mchanga wa Almasi ndani ya mgodi huo,na walikuwa wakifanikiwa,pamoja na kwamba kulikuwa na ulinzi madhubuti na hasa ulinzi wa kutumia Mbwa.

“Mbwa walikuwa wanatuuma sana wakitukamata,lakini ndiyo hivyo tena tulikuwa hatuna namna ya kufanya,kwa sababu mji huu wa mganzo umejengwa kwa Almasi,sisi sio wakulima,bali kazi yetu kubwa ni kuchimba Almasi,tulikuwa tunachimba hata humu katikati ya mji wakati wowote unasikia almsi imelipuka…’’ anaeleza.

Mgodi wa Almasi wa Mwadui umezungukwa na jumla ya vijiji vinane,ambavyo ni Mwadui-Lohumbo(Utemini),Idukilo,Maganzo,Uchambi,Bulima,Sanjo,Magala,na Nyenze.

Katika vijiji hivi ukiangalia kwa makini pamoja na kwamba vingine viko umbali wa kilomita tano kutoka ulipo Mgodi,lakini hakuna kitu kipya ambacho unaweza kukiona kama msaada kwa wakazi wa eneo husika.

Kwenye vijiji hivyo njaa imetawala kwa wananchi,kuna matatizo ya mambukizi ya virusi vya ukimwi na makundi mbalimbali yanataabika na ugonjwa huo na hasa kwa kukosa chakula pamoja na kwamba wanatumia dawa za kuongeza nguvu ambazo kimsingi mtumiaji wake anapaswa kupata lishe bora.

Mfano mzuri ni katika kijiji cha Mwadui-Lohumbo ambapo kikundi cha watu wanaoishi na virusi vya ukimwi wanataabika kwa njaa kutokana na kukosa chakula,njaa imekumba maeneo mengi ya wilaya ya Kishapu ikiwemo eneo hilo maarufu kama Maganzo lenye vijiji vinane.

Wakati Fulani waliwahi kuahidiwa kupatiwa fedha kwa ajili ya kuanzisha ufugaji wa kuku kutoka TASAF kwa lengo la kuwafanya kupata fedha za kujikimu ikiwa ni pamoja na kuwawezesha kupata nauli kwa ajili ya kufuata dawa za kufubaza virusi vya Ukimwi hata hivyo ahadi hiyo bado haijatekelezeka,wanaambiwa fedha hakuna!.
3
Baadhi ya vijana wakiwa na Koreo wakielekea ndani ya mgodi wa Mwadui kuchota mchanga wa Almasi.

Kija Kidagaswa ni mmoja wa vijana katika mji huo wa Maganzo ambaye anasema kwamba maisha wanayoishi katika eneo hilo ni ya shida kutokana na kukosa ajira katika Mgodi wa Almasi wa Mwadui,hali ambayo imekuwa ikisababisha walazimike kuingia kwenye mgodi huo kwa njia ya wizi ili kujipatia mchanga wa dhahabu.

“Mle ndani ya mgodi tunaingia sana tu kwa ajili ya kuchukua mchanga wa dhahabu,hatuna kazi,hawataki kutuajiri na hatuna biashara wala kazi ya kutingizia kipato,ndiyo mana tunalazimika kuingia humo na kuiba mchanga wa dhahabu…….’’ Anasema Kidagaswa.

Anaongeza“Sio kwamba tunaingia kirahisi humo ndani,kuna uzio,kuna mbwa,kuna walinzi wa kila aina,polisi,Mgambo,na hata wale wa Makampuni mengine ya ulinzi,lakini tunapambana nao hivyo hivyo tu……,tukipata mchanga tunakwenda kuosha tukipata almasi tunauza,tukikosa tunarudu tena…..’’.

Sera ya Madini ya Mwaka ya mwaka 1977 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2007 inasema moja ya kazi kubwa ya Idara hiyo ni Kuandaa na kusimamia utekelezaji wa mikakati itakayohakikisha uchimbaji mdogo unakua na kutoa ajira kwa Watanzania wengi.

Pia sera hiyo inasema itandaa miongozo kwa ajili ya uchimbaji mdogo, kuisimamia na kutathmini utekelezaji wake pamoja na Kutayarisha mikakati ya kusaidia uchimbaji mdogo ili kuleta maendeleo endelevu.

Katika eneo la Maganzo hakuna hata moja lililofanyika kwa ajili ya wachimbaji wadogo kwa mujibu wa sera hiyo,katika eneo hilo karibu kila eneo hadi katika makazi ya watu kuna Almasi ambayo hulipuka wakati wowote,lakini wananchi hawaruhusiwi kuichimba,hata kama ikilipukia kwenye eneo la nyumba yako.

Lakini baadhi ya wananchi wamekuwa wakichimba ndani ya nyumba zao kwa njia ya wizi na kuhakikisha kwamba hakuna mtu anayefahamu kwamba katika nyumba Fulani kuna uchimbaji wa almasi unafanyika.

Kibaya zaidi hakuna ajira kwa wakazi wa eneo hilo,na kama wapo basi ni wale wenye vibarua ndani ya kampuni hiyo,kwa mfano katika kijiji cha Mwadui-Lohumbo ambacho kiko umbali wa kilomita tatu kutoka ulipo mgodi hakuna hata kijana mmoja ambaye amepata ajira katika mgodi huo,kijiji hicho kinakadiriwa kuwa na vijana zaidi ya 100 wenye umri kati ya miaka 15-30.
2
Mmoja wa Vijana akionyesha Chekecheo la kukamatia madini aina ya Almasi Maganzo Mkoani Shinyanga.

Hata hivyo vijana pamoja na baadhi ya wakazi wa Maganzo wanasema wamestushwa na kauli ya hivi karibuni ya Mkuu wa wilaya ya Kishapu Wilson Nkambaku,ambaye ametoa agizo la kuwataka vijana kuacha tabia ya kuingia ndani ya mgodi huo kwa shughuli ya kuiba mchanga wa Almasi.

Hivi karibuni katika mkutano wake wa hadhara katika Badhi ya vijiji vinavyozunguka mgodi huo kwenye ziara yake Mkuu wa wilaya hiyo,alisema wimbi la watu kuvamia mgodi huo hususani vijana na kuiba Mchanga wa Almasi limekuwa kubwa na hivyo kutishia usalama wa mgodi huo.

Akaagiza watu wote watakaokamatwa wakiwa wamevamia ndani ya mgodi huo wafikishwe mahakamani na kufunguliwa mashitaka.

Uchunguzi umebaini kuwa vijana wengi wanaokamatwa ndani ya mgodi huo wamekuwa wakifikishwa mahakamani na kuhukumiwa kulipa faini ya shilingi 15,000 jambo ambalo linadaiwa kwamba limekuwa haliwatishi vijana hao.

Kwao faini hiyo wanaona ni jambo la kawaida sana,na ndiyo maana wanaendelea kuingia ndani ya mgodi huo na kuiba mchanga wa dhahabu.

“Faini ni ndogo,tunachofanya ni kuhakikisha kwamba unaingia na haukamatwi,kwa sababu ukiingia na ukafanikiwa kupata mchanga mzuri,unapata hadi shilingi 500,000/=,kwa hiyo kulipa faini ya shilingi 15,000 sio kitu chochote….’’.anasema Makoye Magadula.

Anaongeza “Hii kazi sisi tumekuwa tumeikuta inafanywa na wazazi wetu ndio waliotufundisha kwa sababu ndio maisha yao ya kila siku,hata sisi hatuwezi kuiacha,tutaendelea kuifanya kwa sbaabu hatuna ajira….’’.

Inadaiwa kwamba Katika ziara ya Mkuu huyo wa wilaya katika vijiji vinavyozunguka Mgodi huo,aliwaonya vijana ambao wamekuwa na tabia ya kuvamia mgodi huo na kuiba mchanga wa dhahabu,ambapo katika kijiji cha
Maganzo alikumbana na upinzani mkali kutoka kwa marika yote.

Hali hiyo ilisababisha mkutano wake kuvurugika,lakini akatoka na kuonya kwamba serikali itawashughulikia wale wote watakaobainika kuingia ndani ya mgodi huo kwa lengo la kuiba mchanga huo,lakini wazee nao wakamuapia kwenye mkutano huo,”Ubeshi uliasisiwa na babu zetu,tumerithi na tutauendeleza kwa sababu vijana wetu hawapati ajira’’.

Mzee Makoye Lufungulo kwa upande wake anasema wamestushwa na kauli ya Mkuu huyo wa wilaya ya kupiga marufuku ‘ubeshi’,huku akithibitisha kwamba hiyo ndiyo ajira pekee ya vijana katika eneo hilo vinginevyo wanakaribisha matatizo mengine.

“Suala la ubeshi sio la kutolea maamuzi mazito kama hayo….,ni jambo ambalo linahitaji watu kukaa chini na kutambua kiini na kuona namna ya kutafuta ufumbuzi wake,lakini kwa stahili hii ya kutoleana Amri,ni ngumu sana……’’ anasema Mzee Lufungulo.

Anasema yeye mwenyewe amefanya kazi ya ‘Ubeshi’ katika kipindi chote cha miaka 70 aliyo nayo hadi sasa,na ndiyo shughuli pekee iliyomfanya kusomesha watoto wake,na hata sasa kazi yao ni hiyo na ndiyo inayowasaidia kuendesha maisha yao ya kila siku.

“Suala la ‘Ubeshi’hata marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alikuwa analijua,aliwahi kuja hapa na akashuhudia na hapo ndipo alipowaeleza wakoloni kwamba ili kuondokana na hali hiyo ni lazima watoe Ajira kwa vijana ama wananchi wa eneo hilo wakati huo sisi tulikuwa vijana tukifanya kazi hiyo ya Ubeshi…..’’ anasema Mzee Lufungulo.

Anasema katika eneo hilo hakuna kiongozi yeyote ambaye anaweza kuzuia suala la ‘Ubeshi’ ndani ya mgodi huo wa Mwadui,isipokuwa jambo pekee ni uongozi wa mgodi huo kuhakikisha kwamba unaweka utaratibu wa kuajiri wakazi wa eneo hilo hususani vijana ambao wanaonekana kuwa wengi zaidi.

Wengi wa Wazee wa eneo hilo wanasema kwa vyovyote vile hali ilivyo hivi sasa kuna hatari na Mgodi huo kuvamiwa na wananchi kwa lengo la kujichukulia mali(Almasi),kwa sababu inavyoonekana uvumilivu umewatosha.

“Kwa muda mrefu sasa tumeahidiwa kwamba tutapatiwa maeneo ya uchimbaji ili na sisi tuchimbe kwa ajili ya kuendesha maisha yetu,lakini tunashangaa Mgodi umepewa eneo kubwa la kuchimba Almasi,pamoja na makampuni mengine ya watu Binafsi yamekuwa yakija hapa na kupata maeneo ya uchimbaji lakini sisi tukikosa….’’ Anasema Mzee Lufungulo.

Anaongeza “Kibaya zaidi kuna maeneo ambayo yalikuwa makazi ya wananchi ambao nao walikuwa wanaishi na kuchimba kwa ajili ya kuendesha maisha yao,lakini yote hayo yamechukuliwa na makampuni ya watu binafsi bila hata kuwalipa wahusika fidia ya mali zao….’’.

Makampuni yanayoendesha shughuli za uchimbaji wa Almasi katika eneo la Maganzo ni Williamson Dimond,pamoja na El Hilali,ambalo ni kampuni ya mtu binafsi ambayo yote kwa pamoja yanalalamikiwa kwamba yamekuwa hayatoi msaada kwa wakazi wanaozunguka kwenye eneo hilo,huku mengine yakiwa hayajawalipa wananchi fidia ya mali zao.

Kwa vyovyote vile zinahitajika juhudi za haraka katika kuhakikisha kwamba migogoro kati ya makampuni ya uwekezaji katika eneo hilo yanamaliza kero zilizopo kati yao na wananchi wa eneo husika,ili kuepusha vurugu zinazoweza kuja kujitokeza hapo badaye kama zilizojitokeza huko Mkoani Mtwara,pamoja na Tarime Mkoani Mara.

1 Comment
  • Tatizo la 'UBESHI'si dogo kama mkuu wa wilaya afikirivyo, nimesomea hapo Shy-bush na vijana walikuwa wanaingia mgodini wengine wakitokea shuleni.

    Kusema ukweli kuna watu wenye vipato vikubwa wapo nyuma ya hii biashara na wengi wao ni watu walio serikalini ama wako karibu na dola. Hawa ndio wanunuzi wa hiyo almasi na wanawafadhiri vijana na huwakomboa mara tu wakamatwapo.

    Mbaya zaidi wafanyakazi wa mgodini wanahusika kwa karibu sana kuratibu shughuli husika.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *