Miundombinu ya maji Mwanza sasa kuboreshwa, mita mpya kufungwa

Jamii Africa

Mamlaka ya  Majisafi na Majitaka Jijini Mwanza(Mwauwasa)  inatekeleza mradi  utakaogharimu   Euro 900,000  kwa ajili ya  kuboresha miundombinu, ikiwemo  ufungaji wa mita kubwa ya kisasa  itakayosaidia kupunguza  upotevu wa maji  yanayozalishwa  na mamlaka hiyo.

Taarifa hiyo ilitolewa Jijini Mwanza na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka hiyo , Mhandisi Mashaka Sitta, wakati  akizungumza na waandishi wa  habari ofisini  kwake.

“ Tatizo  lipo, ingawa kusema kweli linaendelea kupungua; isitoshe muda siyo mrefu  tatizo  hilo litabaikia  historia mara baada ya kukamilikakwa mradi mkubwa ambao utagharimu Euro 900,000,” alisema Mhandisi Sitta  na kuongeza;

“Kupitia mradi huo, Mwauwasa itanunua mita  za kisasa  kwa ajili ya kudhibiti  upotevu wa maji”.

Kaimu Mkurugenzi  huyo alisema  fedha hizo  zitatumikika katika ununuzi wa vifaa ikiwa ni pamoja  na mita za kisasa pamoja na magari kwa ajili ya usafiri wa  wataalamu   watakaotekeleza mradi huo.

Alisema  kupitia  mradi huo, Mwauwasa  inatarajia kufunga mita  moja kubwa  ya kieliktroniki   katika ofisi ya makao makuu ya mamlaka, ikiwa ni njia mojawapo ya  kudhibiti  tatizo  sugu la upotevu wa maji.

Alisema mita hiyo iitwayo bulk (bulk  metre)  ina  uwezo  wa kutoa taarifa  juu  ya upotevu wa maji katika  mita ndogondogo zilizounganishwa  kwenye mtandao wa mamlaka.

Mhandisi huyo  alisema kwa kutumia  mita hiyo, mamlaka itakuwa  na ushahidi ambao  utaiwezesha Mamlaka  kuchukua hatua dhidi ya visababishi  vya upotevu wa maji ya bomba jijini hapa.

“ Uholanzi   imekubali kutusaidia fedha  kupitia EU ( Jumuia ya nchi  za  Ulaya). Kwa  ajili hiyo, ndio  watakuwa consultant (washauri),” alisema  Sitta.

Kwa  mujibu wa Sitta,  tayari  washauri hao wapo   Jijini  hapa kwa ajili ya kuendelea  na awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mradi huo.

Alisema  mradi  huo utaanza kutekelezwa  ifikapo  Aprili  mwaka huu na kwamba unatarajiwa  kukamilika baada ya miaka miwili.

Hata  hivyo, alisema   kwa sasa upotevu wa maji  yanayozalishwa na mamlaka hiyo umepungua kutoka  wastani wa asilimia 48  kufikia mwishoni mwa mwaka jana  hadi asilimia  41.6  Januari  mwaka huu.

Alisema  upungufu huo  umetokana  kuimarika  kwa usimamizi katika kitengo cha  usomaji mita pamoja na udhibiti wa vitendo vya kujiunganishia mita  za maji kiujanja ujanja.

Alisema  lengo la mamlaka  hiyo ni  kuhakikisha upotevu wa maji unazidi kupungua hadi asilimia 38 ifikapo Juni mwaka huu.

“ Mitambo  yetu ina uwezo wa kuzalisha  maji  ya kiwango cha mita za ujazo 108  kwa siku, ingawa   hadi sasa tunazalisha mita  za ujazo 72,000  tu kwa siku.  Tofauti  hii inatokana na ukweli kwamba bado tunakabiliwa na changamoto  kwamba   maeneo mengine jijiji bado hayajafikiwa na mtandao wa maji,” alisema.

Alisema  hali hiyo  inasababishwa na jiografia ya Jiji  la Mwanza, ikiwa  ni pamoja na miamba,milima  pamoja na ukosefu wa fedha kwa ajili ya kutengeneza  njia ya  kupitishia mabomba ya maji.

Imeandikwa na  Juma Ng’oko, Mwanza                   

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *