Rais alidanganywa kuhusu umeme Songea?

Albano Midelo

RAIS Jakaya Kikwete mwezi Agosti 2009 alifanya ziara katika mkoa wa Ruvuma kwa lengo la kuangalia shughuli za kimaendeleo pamoja na changamoto zinazowakabili wananchi wa mkoa huo.

Siku ya kwanza ya ziara yake Rais wakati anapita barabarani akitokea uwanja wa ndege wa Songea wananchi walikuwa wakipiga kelele na kudai umeme huku wamewasha taa mchana  kutokana na hali halisi ya tatizo sugu la umeme katika mji wa Songea ambalo lilisababisha mji kuwa giza kutokana na mgawo mkali wa umeme ambao pia unazorotesha maendeleo ya mkoa wa Ruvuma.

Rais Kikwete

Rais Kikwete kwa namna ya pekee aliguswa  na alisikitishwa na kasi ndogo ya kushughulikia ufumbuzi wa tatizo la vipuri vya mashine za kufulia  umeme katika mji wa Songea hali liyosababisha kumwagiza meneja wa TANESCO mkoa wa Ruvuma injinia Monica Kebara  kufuatilia ili kujua vipuli vya mashine hizo vipo wapi na alitaka kupata ripoti ya vipuri hivyo na mwenendo  mzima wa matengenezo ili wananchi  wafahamu kila hatua.

Rais Kikwete hakuishia hapo,badala yake aliahidi kuileta mashine mpya ya kufua umeme ambayo aliamini ingeweza kumaliza tatizo la mgawo mkali wa umeme katika mji wa Songea makao makuu ya mkoa wa Ruvuma hivyo mgawo mkali wa umeme kubakia kuwa historia.

Jambo la kushangaza licha ya mashine mpya ya Rais Kikwete kufungwa na kuanza kutumika kuzalishia umeme katika mji wa Songea ,hali ya umeme katika mji wa Songea tangu mwaka 2009 hadi sasa inazidi kuwa mbaya ambapo maeneo mengi ya mji huo ni giza hadi siku tatu  kutokana na mgawo mkali wa umeme unaoendeleo kufanywa na TANESCO.

Matumaini ya Rais Kikwete kuhakikisha kuwa tatizo la umeme katika mji wa Songea litakuwa limemalizika tangu mwaka 2009 yamegonga ukuta  ,hali hiyo  imewafanya baadhi ya wananchi wa mji wa Songea kupoteza imani na kudai kuwa inawezekana mashine hiyo mpya ilitolewa katika mazingira ya kisiasa zaidi kuliko hali halisi kwa kuwa tatizo la ukosefu wa umeme wa uhakika limeongezeka.

Hamza Chenyewe ni mkazi wa Matarawe mjini Songea anadai kuwa TANESCO wameshindwa kumaliza tatizo sugu la umeme katika mji wa Songea na kusisitiza kuwa tatizo la umeme linaonekana kushughulikiwa kisiasa zaidi na kwamba tatizo la umeme  linachangia umasikini kwa wakazi wa Songea ambao wanashindwa kufanyakazi zao za kiuchumi kutokana na ukosefu wa umeme wa uhakika.

Chenyewe ambaye ni fundi seremala anasema ukosefu wa umeme unaleta kero kubwa kwa mafundi ambapo baadhi yao wameshitakiwa na kufikishwa mahakamani baada ya kushindwa kukamilisha matengenezo ya samani mbalimbali kwa wakati kutokana na kushindwa kukamilisha kazi za useremela ambazo haziwezi kufanyika bila umeme .

Adolf Kapinga meneja mstaafu wa kampuni ya Tanzania motors anasema ukosefu wa umeme wa uhakika umesababisha kuongezeka kwa ugumu wa maisha unaosababisha mfumko wa bei ambapo hivi sasa kwa mfano bei ya mchele mjini Songea imepanda kutoka shilingi 1000 hadi 2000 kwa kilo na kwamba gharama za vyakula kwenye mahoteli au mama lishe pia zimepanda mara dufu.

Agnes Mbonde mkazi wa Lizabon anasema kuwa ukosefu wa umeme hasa wakati wa usiku unasababisha kuongezeka kwa vibaka ambao wanapenda giza ili kufanya uharifu na kwamba wanawake ndiyo waathirika wakuu kutokana na ukosefu wa umeme wa uhakika katika mji wa Songea.

John Mtemi mfanyabiashara wa vifaa vya umeme mjini Songea anasema ukosefu wa umeme unasababisha biashara yake kuwa ngumu kwa kuwa wateja wake wanashindwa kujaribu vifaa wanavyokuwa wamevinunua hivyo kuamua kuacha kununua kuhofia kununua vifaa vibovu ambapo hivi sasa huduma zote na kila kitu kinachohusiana na umeme  kimepanda bei katika mji wa Songea.

“Wafanyabiashara na watu wenye uwezo wamenunua jenereta ndogo za kuzalishia umeme,ukipita kwenye mitaa mbalimbali ya mji wa Songea utaona utitiri wa jenereta,hii ni kutokana na wananchi sasa kukosa imani tena na umeme wa TANESCO ambao hauaminiki tena wala huwezi kufahamu lina umeme utawaka na lini utakatika hali ni mbaya’’,anasema Richard Shirima mfanyabiashara mjini Songea.

Uchunguzi umebaini kuwa ukosefu wa umeme pia unazorotesha vyombo vya habari vilivyopo mkoani Ruvuma kushindwa kusikilizwa na kuona na wananchi ambapo baadhi ya redio na luninga sasa ni miezi kadhaa havipo hewani hali ambayo inawakosesha wananchi haki yao ya kikatiba kupata habari .

Mwanaharakati Mohamed Kudeka mkazi wa Songea anatoa wito kwa serikali kuachana na umeme wa majenereta ambao matatizo yake yamekuwa yanajirudiarudia na kusababisha kero kubwa kwa wakazi wa mji wa Songea.

“Mchawi ni ugonjwa wa majenereta ambayo vipuli vyake vimechoka na kuchakaa,Rais angeambiwa ukweli kuhusu ukubwa wa tatizo la umeme angeweza kuleta mashine mpya yenye uwezo mkubwa,tumechoka na kero hii kama sio ubovu wa mashine utasikia mafuta ya kuendeshea mitambo yamekwisha TANESCO tuambieni ukweli’’,anasisitiza.

Kaimu meneja wa TANESCO mkoa wa Ruvuma Haruna Mwachula anadai kuwa ubovu wa mashine tatu  kati ya sita za kuzalishia umeme katika kituo cha TANESCO mjini Songea mkoani Ruvuma umesababisha mgawo mkali wa umeme kwa wakazi wa mji huo.

Mwachula anabainisha kuwa mashine tatu zinazozalisha umeme hivi sasa katika mji wa Songea zina uwezo wa kuzalisha megawati 2.2  ambapo mahitaji halisi ya umeme katika mji wa Songea ni megawati 4.5 .

“Umeme unaozalishwa hivi sasa ni karibu nusu ya mahitaji ya umeme katika mji wa Songea ,hali hii imesababisha kuwepo mgawo mkali wa umeme,hata hivyo mashine tatu ambazo ni mbovu vipuli vyake vimeagizwa na TANESCO makao makuu ‘’,anasema.

Anasisitiza kuwa mafundi wa TANESCO wanafanyakazi usiku na mchana ambapo tayari wamefanikiwa kufungua vipuli vyote vibovu kwenye mashine aina  ya katapila na  ABC  zenye uwezo wa kuzalisha megawati 3.2

Hata hivyo Mwachula anabainisha kuwa mashine mpya aina ya  ABC yenye uwezo wa kuzalisha megawati 1.6 ambayo ilitolewa kwa ahadi ya Rais Jakaya Kikwete tayari imefungwa na inafanyakazi ikisaidiwa na mashine mbili za zamani aina ya wartisila zenye uwezo wa kuzalisha kilowati 800.

“ Vipuli vipya vikiagizwa na Kazi ya kufunga vipuli katika mashine tatu ikikamilika itawezesha mashine zote kuzalisha umeme wa megawati 5.5 wakati mahitaji katika mji wa Songea ni megawati 4.5 hivyo kupatikana kwa  umeme wa ziada na tatizo la mgawo wa umeme kubakia kuwa historia’’,anadai kaimu meneja wa TANESCO mkoa wa Ruvuma.

Hii ni changamoto kwa TANESCO makao makuu kuhakikisha  kuwa vipuli vipya vya mashine za kufulia umeme vinaagizwa na kuletwa haraka ili kuondoa tatizo hili ambalo hadi sasa bado halijapata tiba sahihi ambayo ni Songea kuunganishwa kwenye grid ya Taifa au umeme mbadala wa madini ya makaa ya mawe na uranium ambayo yote yanapatikana kwa wingi mkoani Ruvuma.

 

 

 

 

 

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *