Vigogo wa Wazazi CCM wagombana hadharani kabla ya Kikwete kufika

Jamii Africa

MAANDALIZI  ya sherehe za maadhimisho ya miaka 35 tangu kuzaliwa kwa Chama Cha Mapinduzi(CCM) yameingia dosari baada ya Makamu Mwenyekiti wa Jumuia  ya Wazazi wa  chama hicho ngazi ya Taifa, Dogo  Mbarouk ,  kugombana hadharani  na  mwenyekiti wa Jumuia hiyo ngazi ya mkoa  wa Mwanza, Ezekiel  Bahebe.

Maandalizi  hayo yameingiwa dosari  siku chache kabla Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete  akitarajiwa  kuwasili jijini hapa  wakati wowote leo  kwa ajili ya sherehe za miaka 35  ya kuzaliwa  kwa CCM.

Chanzo  cha habari   kutoka  ndani  ya  Jumuia  hiyo  zimeliambia FikraPevu kuwa  ugomvi huo  uliibuka Februali Mosi mwaka huu, majira ya mchana  katika  ofisi ya jumuiya hiyo mkoa  wa Mwanza.

Habari zinasema  vurugu hizo zilitokea muda mfupi baada ya  Dogo kuwasili jijini hapa  kwa  ajili  ya maandalizi ya kilele  cha maadhimisho ya  miaka 35  ya kuzaliwa cha Chama Cha Mapinduzi; sherehe ambazo  mwaka huu zitafanyika kitaifa mkoani hapa.

“ Ugomvi huo  ulitokea  baina ya viongozi hao  baada  ya Dogo kufoka kwamba  kwa nini miradi ya Jumuia ya wazazi mkoani  Mwanza inasuasua;  kitendo ambacho mwenyekiti  wa Jumuia ya wazazi  mkoani hapa  (Ezekiel Bahebe) alikipinga  kwa madai kwamba Dogo anaingilia majukumu ya mkoa” chanzo cha  habari kilidai  kwa sharti la kutotajwa jina gazetini.

Chanzo chetu cha habari  kinadai  kuwa Bahebe  alimweleza Dogo  pasipo uoga wowote  kuwa  kwa  wadhifa wake, hapaswi kuhoji  juu ya miradi ya  mkoa na kwamba  kufanya hivyo ni kuvuka mipaka  ya majukumu yake.
Inadaiwa kwamba  Dogo ambaye yuko mkoani hapa  kwa ajili ya maandalizi ya sherehe za maadhimisho ya  miaka 35 tangu  kuzaliwa kwa CCM,  alikutana na kikwazo  hicho baada ya kusomewa  taarifa fupi ya Jumuia.

Kwa  mujibu wa habari, taarifa hiyo iliyosomwa na Katibu wa Jumuia ya wazazi wa CCM  mkoani hapa, Habiba  Haji,  mbele ya Makamu  mwenyekiti huyo  ilidai utekelezaji wa baadhi ya miradi ndani ya Jumuia hiyo umekwama kutokana  na  ukata.

Alipoulizwa, Bahebe  alisema” Taratibu ziko wazi kwamba  ipo mipaka  katika majukumu ya kiongozi wa Taifa na Mkoa; lakini hata hivyo ninaomba  ukamuulize katibu wangu  kuhusu  kilichotokea jana “

Alikiri  pia  kwamba  Dogo  yuko mkoani hapa  ikiwa  ni sehemu ya maandalizi  ya sherehe za maadhimisho ya miaka 35 ya kuzaliwa kwa  CCM.

“ Ni  kweli  jana( yaani juzi Februali Mosi)  tulikuwa  na kikao na Makamu  Mwenyekiti; mwenyekiti wangu wa mkoa , Ezekiel  Bahebe  alikuwepo  na walihitilafiana kidogo tu  na Makamu  mwenyekiti wa  Jumuia ngazi ya  Taifa” alikiri  Katibu wa Jumuia hiyo ngazi ya mkoa  wa  Mwanza, Habiba Haji.

Alikiri kwamba hitilafu hiyo ilitokana na  kusuasua  kwa utekelezaji wa miradi ya Jumuia  ngazi ya mkoa.
Ingawa  hakuwa tayari   kutoa ufafanuzi  juu ya suala hilo,  Katibu huyo alikiri kwamba  utekelezaji wa baadhi ya  miradi ya Jumuia  hiyo  unasuasua  kutokana na kukosekana  kwa fedha.

“ Hata hivyo, Dogo  anatarajiwa   kutembelea  miradi yetu iliyoko  katika wilaya ya Geita na baadaye atatembelea   mradi wetu wa shule ya sekondari Bulima  ambapo  atapata fursa ya  kuzungumza na wazazi kabla ya Februali 5 ” alisema Katibu huyo.

Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Jakaya Kikwete  kesho Jumapili anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika  maadhimisho ya miaka 35  tangu kuzaliwa kwa  chama hicho, Februali 5 mwaka 1977, siku ambayo mwaka huu imeangukia katika siku ya kuzaliwa kwa zmt

Taarifa hii imendaliwa na Juma   Ng’oko, Mwanza 

1 Comment
  • Hivi kama viongozi kama akina Bahebe wanaoonesha kuwa wanajua misingi, kanuni na miiko ya chama kwa kuzuia Dogo asihoji kuhusu miradi ya jumuia ya wazazi Mwanza, kwanini UELEWA huo na misimamo hiyo wasiitumie kuondoa ubadhilifu na uongozi mbovu unaopigiwa kelele na wanachama na watu wengi ulioko kwenye chama hicho?

    kwanini umuhimu wa kufuata taratibu na miiko ya chama unatumika kwa masuala manyonge tu?

    kwa nini hawa wazee wasivae ujasiri wakasafisha chama kwa ngazi zote?

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *