Mgogoro wa ardhi Mwanza wapelekwa kwa Waziri

Jamii Africa

MIGOGORO  wa ardhi  inazidi kuwa  kero kubwa miongoni mwa wakazi wa Jiji la Mwanza ambapo wiki  jana ( Mei 6) zaidi ya wananchi 100 kutoka mtaa  wa Sumba ‘B’ katika wilaya ya Ilemela Jijini hapa  waliamua  kuandamana  hadi ofisini kwa Mkuu  wa Mkoa, Abbas Kandoro ili aweze kuwasaidia.

Aidha, baada ya kukoswa  majibu  waliyokuwa  wakiyatarajia  wananchi  hao  wameamua kuandika  barua kwenda kwa  Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi.

Viongozi  wa  kamati  maalumu iliyoundwa na wananchi hao  wameiambia FikraPevu kwamba mgogoro huo  ulianza tangu mwaka 2008, baada ya maafisa  wa ardhi katika sekretarieti ya mkoa wa Mwanza kuanza zoezi la upimaji na uthaminishaji pasipo kuwashirikisha wakazi wa mtaa huo .

” Ni kweli  tuliandamana June 6 mwaka huu majira ya asubuhi; kutoka  mtaa wa Sumba ‘B’ hadi  katika eneo la ofisi za Mkuu  wa Mkoa” alisema mwenyekiti wa kamati  iliyoundwa, Ramadhani Mohamed  wakati  alipofika katika ofisi za geti hili  mwanzoni mwa wiki hii.

Mohamed alisema  huduma waliyopewa  na Mkuu  wa Mkoa haikuwaridhisha kwa vile  waliambiwa  amewasiliana na Mkuu  wa Wilaya ya Ilemela ili aweze kutoa majibu  sahihi  kuhusiana  na mgogoro.

Jiji la Mwanza
Jiji la Mwanza pichani

” Jambo  jingine ambalo linatushangaza  sisi ni kwamba awali tuliambiwa kuwa wanapima viwanja kwa ajili ya makazi ya pamoja na eneo la wazi kwa magari ya  wafanyakazi wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa, lakini tunashangaa upimaji wa viwanja umefanyika na tayari  Wachina  wameanza kufika na kuoneshwa viwanja” aliongeza  Mwenyekiti  wa kamati  maalumu iliyoundwa na wakazi hao kwa ajili ya ufuatiliaji,  Ramadhan Mohamed .

Alisema  upimaji  na uuzaji wa viwanja  katika eneo hilo  umeghubikwa na utapeli kwa vile hata stakabadhi zilizotolewa  kwa  ya  kugarimia  malipo ya fidia ya na kupimiwa viwanja hazina nembo ya serikali .

Alizitaja baadhi ya hatua  zilizofikiwa na kamati yake katika kutatua mgogoro huo  ni pamoja na kuitisha vikao  kwa ajili kukutana na watuhumiwa na kwamba kila mara wahusika.

” Mheshimiwa Waziri, sisi wananchi hatutaki kumwaga damu tunakuomba uje mwenyewe ili uweze kuujua na kuutatua mgogoro huu; kwani  mara kadhaa tumefuatilia hadi kwa Mkuu  wa Mkoa bila mafanikio” inasema sehemu ya barua hiyo (nakala tunayo).

Wananchi hao wanamuomba Waziri  kutoa  majibu yake  kabla  wao hawajafikia hatua ya kujichukulia  sheria mkononi.

” Ni matumaini yetu kuwa tutapata jawabu kutoka kwako kabla ya maamuzi ya wananchi, nyaraka zilizopo nyuma ya barua hii ni baadhi tu ya wananchi wanaopinga ifisadi huu”  wanaendelea  kudai  wananchi hao kupitia barua hiyo ambayo  pia nakala yake imetumwa kwa Mkuu wa mkoa  wa Mwanza.

Wananchi hao wanadai  katika  barua hiyo yenye kichwa cha habari ‘mgogoro wa ardhi’ kwamba wametapeliwa maafisa kutoka ofisi ya Mkuu  wa Mkoa  kwa vile hawakushirikishwa  kabla ya zoezi la upimaji  na uuzaji wa viwanja vyao  kuanza.

Kwa  mujibu  wa barua  hiyo ambayo imepewa  kumbukumbu namba 2/yenye vikao 10/2008/2011, Afisa ardhi  kutoka  ofisi ya Mkuu  wa Mkoa  wa Mwanza ambaye ametajwa kwa jina moja la Tegambwa  na mwenzake  aliyetajwa kwa jina moja la Beni pamoja na mwenyekiti wa serikali ya mtaa huo, Yusto Mleka,  ndio chanzo cha mgogoro huo.

Barua  hiyo iliyoandikwa Mei 6 mwaka huu inadai kuwa ardhi yao imeporwa na maafisa ardhi wa mkoa wa Mwanza pasipokuwepo na mihtasari  yoyote  inayoonesha ushirikishwaji na wananchi hao.

Alizitaja baadhi ya hatua  zilizofikiwa na kamati yake katika kutatua mgogoro huo  ni pamoja na kuitisha vikao  kwa ajili kukutana na watuhumiwa na kwamba kila mara wahusika hukacha kwa kisingizio  cha kuwa na kazi nyingi za kiofisi.

Mkuu  wa Mkoa, Abbas Kandoro  amekiri  kwa njia ya simu juu ya kukutana na wananchi hao.

Alikiri pia kwamba suala hilo  limedumu kwa muda  mrefu sasa na kwamba amelikabidhi  katika ofisi ya Mkuu  wa Wilaya kwa  kwaa ajili ya kushughulikiwa.

” Ni kweli mgogoro huo ninautambua, na nilikutana na wawakilishi wa wananchi hao siku ya Ijumaa iliyopita; kwa ufupi ni kwamba nimelikabidhi  suala hilo  katika ofisi ya Mkuu wa Wilaya  ili litafutiwe ufumbuzi” alikiri  Kandoro.

Mwenyekiti wa serikali ya kijiji hicho, Yusto Mleka  alikiri  kwa njia ya simu kuhusu kuutambua mgogoro huo ingawa alikanusha  kuwa yeye  hana uhusiano wowote na maafisa ardhi kutoka ofisi ya Mkuu  wa Mkoa.

Alifafanua kuwa mgogoro huo ulianza kabla yeye hajachaguliwa kuwa mwenyekiti wa mtaa huo.

Diwani  wa kata hiyo, Margareth  Chenyenge (CHADEMA)  amekiri kuwepo kwa mgogoro huo  na kuongeza kwamba  umeanza kusababisha hofu  na uvunjifu wa amani  ndani ya mtaa huo.

Alisema  tayari  ameanza kufanya  vikao na wakazi wa mtaa huo  kwa ajili ya kupata ufumbuzi.

Hata  hivyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, Wilson Kabwe aliliambia   gazeti hili kwamba yeye hana taarifa kuwepo kwa mgogoro huu.

Habari hii imeletwa na mwandishi wetu Juma Ng’oko aliyeko mkoani Mwanza

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *