NSSF katika mgogoro na serikali Mwanza, wadharau maelekezo ya RC

Jamii Africa

MENEJA  wa Mfuko wa  Taifa  wa Hifadhi ya Jamiii (NSSF)  mkoani Mwanza, Elizabeth  Ngabo, anadaiwa kupuuza agizo lililotolewa na ofisi ya Mkuu wa Mkoa.

Habari za uhakika  zimeeleza kwamba , Meneja huyo bado hajachukua  hatua za kisheria dhidi  ya uongozi wa  kamapuni ya Kilumi Security  Services Ltd, kama alivyogizwa  kwanjia ya barua na Katibu wa Mkuu  wa Mkoa  wa Mwanza, Mathayo  F Maselle.

Inadawa kwamba Meneja  huyo anashirikiana na baadhi ya viongozi wa Kilumi Security Services Ltd jijini hapa; hatua  ambayo inachangia katika uvunjaji  wa sheria  za ajira.

“ Inavyonekana  ni kwamba Meneja  wa NSSF  ametutosa; kwani  tangu wakati huo hatujalipwa  mafao yetu na wala Meneja huyo  hajachukua hatua  dhidi  ya aliyekuwa mwajiri wetu, Kilumi  Security  Services,” alidai  aliyekuwa  mlinzi katika kampuni hiyo, Jeremiah   Nyamsongeca.
Anadai  kuwa baada ya kuachishwa kazi  alibaini kuwa  kampuni hiyo ilikuwa  haiwasilishi makato ya fedha katika mfuko wa NSSF; kitendo alichosema ni kinyume cha sheria.

Alidai pia kuwa yeye  pamoja na  na wenzake  hawana vitambulisho licha ya kwamba waliajiriwa kwenye kampuni hiyo kwa zaidi ya mwaka mmoja.
Nyamsongeca  ambaye  Februari  mwaka huu  alilalamikia  uongozi  wa NSSF  mkoani hapa kwa kushindwa  kuchukua hatua za kisheria dhidi  ya aliyekuwa mwajiri wake,  aidai kuwa bado anapigwa danadana.

“ Ninao  ushahidi  kwamba Meneja  wa NSSF  alishatumiwa barua yenye kumbukumbu namba EA112/205/01 iliyosainiwa na Katibu  wa Mkuu  wa Mkoa wa Mwanza, akiagizwa kuchukua hatua kwa mujibu wa sheria dhidi ya Kilumi  Security  Services” alidai  mlalamikaji huyo.

Alidai barua hiyo (nakala  tunayo) ya tarehe 14/2/2012 ilisema kuwa ofisi ya Mkuu wa Mkoa  wa Mwanza imechoshwa na malalamiko yasiyokoma dhidi ya kampuni ya Kilumi Security  Services.

Huku  akikabidhi nakala  ya barua hiyo kwa mwandishi wa habari hizi, Nyamsongeca  alidai  kuwa uongozi wa kampuni hiyo  unatamba kwamba kamwe ofisi ya NSSF  mkoa  haiwezi kuwafikisha mahakamani  wala kuwalazimisha kulipa  deni.

“ Taarifa  nilizonazo ni kwamba kampuni hiyo inadaiwa  zaidi ya shilingi  milioni kumi,” alidai.

Alipoulizwa, Meneja  wa NSSF  mkoa  wa Mwanza, Ngabo,  alikiri kupokea barua hiyo ingawa  hakuwa tayari kutoa ufafanuzi kwa madai  ya kutingwa na kazi nyingi ofisini kwake.

“ Ni kweli kuna malalamiko pamoja  na barua kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa kwamba Kilumi  Security  Services ambaye  ni mteja wetu inadaiwa makato ya fedha. Hata hivyo, bado ninaendelea kuwasiliana nao” alikiri  Meneja huyo.

Alisema  ofisi yake haijachukua  hatua  ya kufikisha kampuni hiyo mahakamani kutokana na kuepuka usumbufu pamoja na mlolongo wa kesi mahakamani.

“ Pamoja  na barua hii, Mhe Mkuu wa Mkoa anataka kuona hatua kali zinachukuliwa haraka iwezekanavyo ili pamoja na kupunguza malalamiko yasiyokuwa ya lazima lakini pia kuwatendea  wananchi hawa haki na hivyo kudumisha amani na utulivu katika Jamii,” inaagiza sehemu ya
barua  iliyoandikwa na Katibu wa Mkuu wa Mkoa.

Alipoulizwa kwa njia ya simu, Meneja  wa kampuni hiyo , Peter David, alikiri kuwepo  kwa  deni hilo huku  akisema suala hilo linashughulikiwa na Meneja wa NSSF mkoa  wa Mwanza.

” Ni kweli  malalamiko hayo yalishafikishwa  katika  ofisi ya  Mkuu wa mkoa; hata hivyo suala hilo linaendelea  kushughulikiwa na Meneja wa NSSF Mkoa” alidai.

Alidai  ofisi  yake inaendelea  na taratibu za malipo hayo na kwamba kudai na kudaiwa ni suala la kawaida katika biashara yoyote duniani.

Imeandaliwa na Juma Ng’oko, Mwanza

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *