Polisi wapora maiti walioua kwa risasi mgodini Tarime

Jamii Africa

JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Tarime na Rorya Mkoani Mara, kupitia askari wake wa FFU limelazimika kutumia nguvu pamoja na kuwatisha kwa silaha wananchi na waombolezaji wa marehemu, Mgosi Magasi Chacha (30), aliyekufa baada ya kupigwa risasi ya moto na polisi wanaolinda mgodi wa North Mara uliopo Wilayani hapa.

Sehemu ya mgodi wa dhahabu wa North Mara, unaomilikiwa na African Barrick Golds

Katika tukio hilo la leo Jumatano saa 5:10 asubuhi, polisi wakiwa kwenye magari manne huku wakiwa wamebeba silaha ikiwamo bunduki aina ya SMG, mabomu ya machozi na marungu, waliwasili kwenye hospitali ya wilaya ya Tarime kuchukuwa mwili wa marehemu Chacha kwa nguvu ili kwenda kuuzika baada ya kuwakamata baadhi ya viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) waliokuwa katika msiba huo.

Mgodi wa North Mara unamilikiwa na kampuni kubwa ya uchimbaji madini duniani ya Barrick Gold, na umekuwa katika mgogoro na wenyeji wa eneo hilo mara kwa mara hali inayosababisha kuwapo kwa matukio yanayohatarisha amani mara kwa mara.

Wakati polisi hao wa FFU waliokuwa wametanda aneo kubwa la hospitali hiyo wakitaka kuchukua mwili wa marehemu, mamia ya wananchi, ndugu wa marehemu akiwemo mkewe (jina lake halikupatikana), pamoja na viongozi wa Chadema wilaya ya Tarime, waliwazuia polisi kuuchukuwa mwili huo, wakitaka lazima taratibu za kisheria zifuatwe na si vinginevyo.

Baada ya viongozi hao wa Chadema, wananchi, ndugu na jamaa wa marehemu Chacha kuchachamaa, mke wa marehemu alikuwa akilia kwa uchungu huku akiwa amekaa karibu na mlango wa chumba cha kuhifadhia maiti, akikataa polisi kuchukuliwa mwili wa mumewe kwenda kuuzika bila ndugu na yeye kuridhia, lakini askari kanzu mmoja wa kiume alionekana kuanza kumburuza mke huyo wa marehemu kwa lengo la kumtoa eneo hilo ili polisi wachukuwe mwili huo.

Wakati mke huyo wa marehemu akiburuzwa na mmoja wa askari polisi aliyekuwa akitii amri ya mkubwa wake wa kazi (majina hayakupatikana), mwanamke huyo alikataa katakata kuondoka, lakini polisi nao walionekana kumlazimisha hadi baadhi ya nguo zake alizokuwa amejifunga zikidondoka kisha baadhi ya maeneo ya mwili wake juu ya kiuno yakiwa yanaonekana nje, jambo ambalo lilioelezwa na walioshuhudia  kama ni udhalilishaji.

Mwandishi wa habari hizi alishuhudia vurugu hizo, baina ya polisi na ndugu wa marehemu, ambapo polisi walilazimika kuweka chemba risasi za moto katika bunduki zao za SMG, baada ya kuona wametaka kuzidiwa nguvu, ambapo waliwakamata na kuwaweka ndani mwenyekiti wa Chadema wilayani Tarime, Lucas Ngoto.

Viongozi wengine wa Chadema waliokamatwa na polisi katika tukio hilo ni, Katibu wa Chadema wilaya hiyo, Mroni Mwita pamoja na diwani wa Kata ya Sabasaba, Christopher Chometa, huku mwenyekiti wa Baraza la Vijana Chadema (Bavicha), wilaya ya Tarime, Chacha Heche akiponea chupuchupu kukamatwa kwa madai ya kutaka kuzuia mwili huo wa marehemu usiondolewe hospitalini hapo kwenda kuzikwa.

Marehemu Chacha mkazi wa Kijiji cha Nkende ambaye alikuwa mwendesha pikipiki wilayani Tarime, aliuawa Juni 4 mwaka huu majira ya saa 1:45 asubuhi, kwa kupigwa risasi ubavuni kisha kutokea tumboni na askari polisi wanaolinda mgodi huo wa North Mara, unaomilikiwa na kampuni ya Barrick, na kwamba jeshi la polisi Kanda maalumu ya Tarime na Rorya imethibitisha askari wake kumuua raia huyo, bila kutaja sababu ya mauaji hayo.

Hata hivyo, baada ya vuta nikuvute hiyo iliyodumu takribani dakika 45, hatimaye polisi walifanikiwa kuuchukuwa mwili huo wa marehemu Chacha na kuuondoa nao hospitalini hapo ukiwa chini ya ulinzi mkali wa polisi, na kwamba magari yaliyokuwepo eneo hilo yakiwa yamesheheni askari ni PT 2036, PT 1873, PT 1863, T 754 BLF pamoja na pikipiki moja ya doria, huku gari la halmashauri ya wilaya hiyo SM 5241 ndilo lililotumika kuubeba mwili huo wa marehemu.

Taarifa ya jeshi la polisi Kanda hiyo maalumu, iliyotolewa na Kaimu Kamanda wa Kanda hiyo ya Kipolisi, Sebastian Zacharia-SSP ilieleza kwamba awali marehemu alijeruhiwa kwa risasi tumboni na askari polisi, kwa madai ya kumkata panga mguu wa kushoto mlinzi mmoja wa mgodi huo, Winchlaus Petro (26).

“Kabla mauti kumkuta alijeruhiwa kwa kupigwa risasi tumboni na askari polisi waliokuwa doria eneo hilo la mgodi. Marehemu alianza kumshambulia askari kwa panga na kuikata silaha ya askari huyo mara mbili hata baada ya kuonywa kwa kupiga risasi hewani wakati wa kukamatwa”, ilisema sehemu ya taarifa hiyo ya polisi yenye kurasa moja.

Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo ya wilaya ya Tarime, Nagga Marco ilisema, uchunguzi wake umebaini marehemu Chacha alipigwa risasi ubavuni karibu na mgongo, kisha risasi hiyo ikatokea tumboni.

Kwa upande wao familia na ndugu wa marehemu huyo, akiwemo baba yake mkubwa, Charles Matiko waliieleza FikraPevu kwamba, nguvu iliyotumiwa na polisi kuchukuwa mwili wa kijana wao ni ya kinyama, kwani familia ilikuwa haijaridhia kuchukuliwa kwa marehemu kutokana na ukweli kwamba mipango ya maziko ilikuwa haijakamilika.

Mauaji ya watu eneo hilo la mgodi wa Nyamongo, yanaelezwa kushamiri, ambapo inadaiwa mwaka jana vijana wapatao watano waliuawa kwa kupigwa risasi na polisi, Mei 7 mwaka huu kijana mwingine aliyetajwa kwa jina moja la Mwikwabe aliauawa eneo hilo la mgodi, na kwamba Juni 4 mwaka huu marehemu Chacha aliuawa pia kwa kupigwa risasi ya moto na askari polisi wanaolinda mgodi huo wa North Mara ambao unamilikiwa na kampuni ya kigeni ya Barrick.

Habari imeandaliwa na Sitta Tumma, Tarime

10 Comments
  • Baada ya Polisi kufanikiwa kuondoka mwili huo wa Chacha toka hospitalini, marehemu alienda kuzikwa na Jeshi la Polisi, Halmashauri, au Ndugu, jamaa na rafiki zake?

  • Stori hii inajaribu kuleta karibu matatizo yanayotokana na kutoelewana kati ya wawekezaji na wananchi (mpokeaji). Sasa swala ni ambayo sijaiona ni kwani huyu kijana alipigwa risasi. Je alikuwa mhalifu? alikuwa mtetea haki ya wachache ( wanyonge)?

  • Tunakoelekea ni kubaya.

    Kama polisi wanashindwa kutuliza ghasia kwa njia ambayo si ya kinyama! Mmmh…

  • Cku yao itafika wala haipo mbali na mgodi watafaidi wazawa polen kwa yaliyowakuta

  • Inasikitisha sana kama wewe ni mtanzania lakini uwezi kunufaika na kile kilichopo nchini kwako, poleni sana nduguzani mliopatwa na msiba wa kijana mwenzetu, may holmight god rest his soul in coolest place Amen.

  • kama tumefikia hapo…miaka michache baadae kama hatutokuwa makini na kubadilika….tanzania haitokuwa tofauti na DRC

  • Polisisiem hawa siku zao zinahesabika. Hakiyamama wakati wao utakapofika risasi zao zitageuka kuwa maji na sisi raia tutawakamata kwa mikono yetu na kuwapimia dozi yao. Kiungo kimoja kimoja cha miilini mwao kitacharangwa kwa ustadi mkubwa kabla ya kuvikusanyia katika uchanja maalum kisha kuitia kiberiti. Pambaf zao!!!!

  • Mtatuuwa lakini mwisho wenu unakaribia!! RIP Mgosi.

    Tunaomba mawakili wakujitolea kusaidia mjane huyu kupata haki zake.

  • Hili tukio linasikitisha sana, kwa wapenda amani hii si dalili njema!!

    Mimi ninashindwa kuelewa, hizi nguvu kubwa zitaendelea kutumika mpaka lini? Serikali ina wataalam wa conflict resolution hivi kweli wanashindwa kukaa na jamii na huyu mwekazaji na kutafuta suluhisho la kudumu juu ya tatizo hili? Mimi napata wasiwasi sana juu ya amani ya sehemu husika na Tanzania kwa ujumla.

    Ninaendelea kusikitika juu ya tukio lenyewe, huyo maiti atazikwa kiserikali au amehamishiwa kwingine wakati taratibu za usalama na mazishi vikiandaliwa??

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *