Uhamiaji yanasa wengine 25 usiku wa manane kwa makosa ya uhamiaji; wahusika wahaha!

Jamii Africa

Idara ya Uhamiaji nchini ikiendeleza wimbi la kukabiliana na uhamiaji haramu leo imewakamata watuhumiwa wengine 25 na inapanga kuwapeleka mahakamani ambapo wanaandaliwa utaratibu wa kurudishwa makwao na wale ambao wataweza kuombewa vibali vya kuishi au kufanya kazi Tanzania baada ya kulipa faini.

 

Wahamiaji hao walikamatwa usiku wa kuamkia leo kuanzia saa saba hivi baada ya ya idara hiyo kupokea taarifa za siri za kuwajulisha uwepo wa wa wahamiaji hao haramu. Wahamiaji 13 wa Kipakistani walikamatwa Kariakoo nyumbani kwa Mtanzania mwenye asili ya Pakistani Bw. Mohammed Raza (43).  Taarifa ambazo FikraPevu imezipata zinaonesha kuwa hii ni mara ya tatu kwa Bw. Raza kukutwa akiwa anahifadhi wahamiaji haramu.

 

Watuhumiwa wengine ni Wabangladesh 9  ambao walikamatwa huko Majohe, Ukonga njia ya kwenda Pugu. Watuhumiwa hao wa Kibangladesh walikamatwa katika nyuma ya mkazi mmoja aitwaye Farid Said Hussein ambaye ni dereva. Bw. Hussein ambaye ni Mtanzania amedai kuwa watu hao wanaletwa kwake na mtu aitwaye Hijaz na kuwa wanalipa Shilingi 6000 kwa siku kwa kichwa.

Mtu mwingine ambaye ametajwa kuwa anahusika na kuingizwa kwa wahamiaji hao nchini ni mkazi wa Namanga, Msasani aitwaye Sabira Bacho maarufu Anti Eididi ambaye ana asili ya Pakistani. Hata hivyo Bi Bacho ametoweka na anatafutwa na idara hiyo ila msaidizi wake ndio amekamatwa.

Wakati huo huo watuhumiwa wengine waliokamatwa na mfanyabiashra Jandu Singh jana wamepigwa faini kwa kuingia nchini bila kibali ambayo kila mmoja ametozwa shilingi milioni1.8 katika mahakama ya Kisutu huku taratibu nyingine za uhamiaji zikianza kutekelezwa. Watuhumiwa wengine waliokamatwa leo – hao 25 wanatarajiwa kufikishwa mahakama ya Kisutu siku ya Ijumaa.

Picha chini za tukio zima, majengo yaliyohusika. Mwenye kifua wazi ndiye Bw. Mohammed Raza – hana uhusiano na Mohamed Raza wa Zanzibar ambaye ni  kada wa CCM na mfanyabiashara maarufu.

FikraPevu itaendelea kukuletea hii “showdown” kati ya serikali na wahamiaji haramu kufuatia agizo la Waziri wa Mambo ya Ndani Bw. Shamsi Vuai Nahodha la kutaka idara hiyo ijioneshe kuwa inapambana na suala hilo ambalo limeonekana kuwa ni kero kubwa kwa Watanzania.

Na. M. M. Mwanakijiji na Waandishi wa Fikra Pevu

3 Comments

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *