Sumu ya Cyanide yatishia maisha ya wakazi Geita

David Azaria

AFYA za wakazi wa Mkoa wa Geita ziko hatarini kufuatia kuzagaa kwa sumu aina ya Sayanaidi(Cyanide), inayotumika kwa ajili ya uchenjuaji wa dhahabu katika migodi mbaimbali.

Kwa mujibu wa Uchunguzi uliofanywa na Mwandishi wa habari hizi mkoa wa Geita hususani wilaya ya Geita,matumizi ya sumu ya Cyanide imeongezeka kufuatia kuzagaa kwa migodi ya uchenjuaji wa dhahabu kila kona.

Aidha imegundulika kuwa migodi mingi ya uchenjuaji wa dhahabu inaendeshwa bila kuwa na vibali maalum kama sheria inavyotaka, huku ikitumia pia Sumu ya Cyanide bila kuwa na vibali wala wataalam!.

Mkoa wa Geita wenye wilaya Tano za Geita, Nyang’hwale, Chato, Bukombe na Mbogwe, una jumla ya migodi 21 ya uchenjuaji wa dhahabu, huku 19 ikiwa katika wilaya ya Geita.

Baadhi ya migodi ya uchenjuaji iliyoko Mkoani hapa ni pamoja na BC-Geita, Nyamigogo, Climate Control, Ntimaro, Gold Empire, Tryphone J Mpomvu, Mwagimagi, Mhama Co.Ltd, na Nyakagwe.

Uchunguzi umebaini kuwa asilimia 98 ya migodi hiyo inaendeshwa bila kuzingatia sheria ya migodi na hasa matumizi sahihi ya Cyanide,hali ambayo inadaiwa kutishia usalama wa Afya za wakazi wa maeneo husika kutokana na uharibifu wa Mazingira.

Kwa mfano uchunguzi umebaini kuwa zaidi ya Migodi 14 imezunguka mji wa Geita umbali wa kilomita tano,huku mitambo minne ya kuchuja sumu ya sayanaidi(Cyanide Leaching) ikiwa majumbani mwa watu katikati ya mji.

Baadhi ya watu wanadaiwa kufanya kazi ya kuchuja Cyanide majumbani mwao kwa kutumia madumu ya plastic (200lita drum) katika maeneo ya miji ya Geita, Nyarugusu, Kasamwa na Katoro pia mitambo midogo ya kukamatia dhahabu  ya kubeba kilo 25 hadi 50  za carbon majumbani.

Mgodi-1

PICHA: Baadhi ya wafanyakazi wakiweka mchanga wa dhahabu ndani ya mashimo yenye sumu ya Cyanide kwa ajili ya kuozesha kabla ya kukamua dhahabu

Ofisa Madini Mkazi kanda ya Geita Mhandisi Juma Sementa anathibitisha madai haya huku akidai kwamba idara ya madini imekuwa ktika mikakti mbalimbali ya kutoa elimu kwa wahusika ili kutambua madhara ya uendeshaji wa shughuli zao.

Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na kanuni zake inabainisha wazi taratibu za kuzingatia wakati wa uendeshaji wa shughuli za madini,kwa mfano kanuni ya namba 8 ya The Mining (Environmental Protection for Small Scale Mining), inazuia mchimbaji mdogo kutumia kemikali ya Cyanide kuchenjua madini pasipo kuruhusiwa na mkaguzi Mkuu wa Migodi.

Kifungu namba. 60 cha Sheria ya Madini kinaeleza  namna ya kuomba leseni ya uchenjuaji  na viambatanisho  vinavyotakiwa kuwasilishwa,ambapo kinazuia mtu yeyote kuanzisha ama kuendesha shughuli za uchenjuaji pasipokuwa na leseni(Processing Licence) ama kibali cha kutumia sayanidi(Cyanide Leaching Permitt).

Ofisa Madini Kanda ya Ziwa Mhandisi Salim Salim,anakiri kuwepo kwa hali hiyo na kubainisha kwamba wako katika hatua za mwisho za kufungia migodi yote ya uchenjuaji iliyobainika kufanya shughuli za uchenjuaji bila kuzingatia sheria.

Hata hivyo Mhandisi Salim anasema kabla ya kuchukua hatua hiyo Idara yake imelazika kutoa mafunzo maalum kwa wamiliki wa migodi hiyo ili kutambua umuhimu wa utunzaji wa mazingira ili kuepuka kusababisha madhara kwa jamii.

“Hili si tatizo la Geita pekee,ni tatizo kubwa sana kanda ya Ziwa, lakini Geita ni Kinara, kanda ya Ziwa kwa jumla wake kuna jumla ya Migodi 37 ya uchenjuaji wa dhahabu, lakini Geita inaongoza kwa kuwa na migodi 21, ikifuatiwa na Mwanza 9 na Mara 7…..’’ anasema Salim.

Anasema baada ya kutoa mafunzo hayo kwa wamiliki wa migodi hiyo kinachofuata sasa ni kuhakikisha kwamba wanafunga migodi yote ambayo haitafuata sheria,taratibu na kanuni za madini ili kunusuru afya za Wananchi wanosihi kuzunguka maeneo husika.

Migodi-2

PICHA: Mashimo yanayotumika kuozesha mchanga wa dhahabu kwa kutumia Cyanide, kama inavyofanywa katika migodi ya uchenjuaji wa Dhahabu. Migodi mingi ya aina hii imebainika kwamba haizingatii sheria ya madini ya mwaka 2010 katika matumizi ya Sumu aina ya Cyanide

Mhandisi Salim anasema idara ya madini iko katika mkakati kabambe wa kuifungia migodi yote inayodaiwa kuendeshwa bila kufuata sheria,lakini kabla ya kufanya hivyo wameamua kutoa elimu kwa wahusika ili kuondoa visingizio vinavyoweza kujitokeza wakati wa utekelezaji wa zoezi hilo.

Anasema wamiliki wa migodi hiyo wanatumia sumu kali aina ya Sayanaidi(Cynide),ambayo inahitaji uangalifu mkubwa katika matumizi yake,ili kuepusha madhara yanayoweza kutokea kwa binadamu.

Kwa mfano Mhandisi Salim anasema kuna baadhi ya wasimamizi wa miradi( Supervisors/Site Manager) hawajui madhara ya kemikali zilizopo kwenye maeneo yao ya kazi.

Anafafanua kuwa  wengi wao wamekuwa ni kama walinzi wa mali  na kuhakikisha kifusi kinasombwa,huku akiwaagiza wamiliki wa Miradi hiyo kuwateua Mameneja wanaofahamu madhara na mpangilio mzima wa uchenjuaji,na kufikisha uthibitisho wa barua na picha zao kwa wakaguzi wa Migodi walioko Jirani,ama katika ofisi za Madini zinazowahudumia.

Anasema ni wajibu wa wamiliki wa miradi kuhakikisha vifaa vya usalama na kujikinga kwa wafanyakazi(PPE) vinakuwepo tena vinavyofaa katika maeneo yao ya kazi,pamoja na kuweka utaratibu wa kukabiliana na majanga ya aina yeyote kama vile kuwasiliana wakati wa dharura ( mfano kuwa na king’ora ( audible siren).

Anapongeza Migodi ya Nyamigogo ulioko wilayani Nyang’hwale na BC-Geita ulioko wilayani Geita,kwa kufanya shughuli zao kwa kuzingatia sheria,Kanuni na Taratibu za madini,huku akitaka migodi mingine kujifunza kutoka kwa migodi hiyo.

Baadhi ya wamiliki wa migodi hiyo walisema umefika wakati asa kwa serikali kupitia Wizara ya Madini kuhakikisha kwamba inatoa elimu ya kutosha kwa wazawa ili waweze kumiliki Migodi mikubwa kama wanavyofanya kwa wawekezaji wakubwa kutoka nje ya nchi.

“Hata sisi watanzani kwa hapa tulipofikia tunao uwezo wa kuanza uchimbaji mkubwa madini kama ambavyo wanafanya wawekezaji kutoka nje ya nchi,kikubwa inachopaswa kufanywa na Wizara ni kutoa elimu pamoja na maeneo ya uchimbaji…..’’ alisema Baraka Ezekiel ambaye ni Mkurugenzi wa Kampuni ya MME inayomiliki migodi kadhaa katika mikoa ya Geita,Mara,Mwanza na Shinyanga.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mgodi wa BC-Geita Chacha Mwita aliitaka Wizara kutoa maelekezo kwa maofisa Mazingira wa wilaya ili waweze kujua namna ya kufanya kazi yao badala ya kuwauliza wamiliki wa Migodi hiyo kma ilivyo sasa pindi wanapofika kwao kwa ajili ya kupata vibali vya awali vya kuanzisha migodi yao.

Pia aliitaka Wizara ya Nishati na Madini kutengeneza vitalu vya miti inayonyonya sumu aina ya Cyanide ambayo inatumika kwa wingi katika Migodi hiyo,na kuisambaza kwa wachenjuaji badala ya wao kufanya kazi ya kuitafuta wenyewe hali inayowafanya wengine kushindwa kuitafuta.

Matumizi ya Cyanide yameongezeka kwa kasi kubwa katika wilaya ya Geita katika siku za hivi karibuni, ambapo ukiachilia mbali matumizi makubwa ya Zebaki ambayo nayo ni sumu hatari inayotumiwa na wachimbaji wadogo katika machimbo mbalimbali,kuongezeka kwa kasi kwa migodi ya uchenjuaji wa dhahabu inayotumia sumu tena kwenye makazi ya watu sasa kunatishia usalama wa watu na mali zao.

Inaelezwa kwamba kuna njia nyingi za namna ya mtu kupata sumu ya Cyanide ikiwemo kuvuta kwa njia ya hewa, kula kupitia chakula ikiwemo matunda na mbogamboga, ambapo kwa njia hiyo unaweza kuchukua muda mrefu kupoteza maisha,isipokuwa unapoilamba ama kunywa sumu hiyo unakufa papo hapo.

Dalili za mtu aliyetumia sumu ya Cyanide ni pamoja na kukosa hewa, mwili kuwa mdhaifu, Kuchanganyikiwa, Kifafa, kuumwa kichwa, kusinzia, kizunguzungu, Degedege na kupoteza fahamu.

2 Comments
  • Hey Devy,ulichoongea ni sahihi kabisa. Wengi wetu miongoni mwetu ambao ni wakazi wa Geita hawalijui hili,tunaofahamu ni wachache. Its me ur boy MAU of Police Geita. Big Up mwana!. Keep in touch!

  • Hey Devy,.U hv to discover other issues in GEITA which are deligate to us!Big Up mwana!. Keep in touch! Its ur boy MAU.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *