Polisi ivunjwe kwa kushindwa uchunguzi sumu ya Mwakyembe-wito

Jamii Africa

WAKATI Mbunge wa Kyela na Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk. Harrison Mwakyembe, analishutumu Jeshi la Polisi kwa kutotimiza wajibu kuhusiana na mambo mbalimbali ikiwamo uchunguzi kuhusu kudhuriwa na sumu, baadhi ya Watanzania wametaka polisi ivunjwe na kundwa upya.

Baadhi ya Watanzania hao waliotoa maoni yao kufuatia taarifa iliyotolewa na Dk. Mwakyembe, ikibeza na kushangazwa na majibu yaliyotolewa na polisi kupitia Mkurugenzi wa Upelelezi wa Jinai (DCI), Robert Manumba, aliyewaambia waandishi wa habari kwamba “Mwakyembe hakupewa sumu.”

Miongoni mwa wachangiaji hao wametoa maoni yao katika mtandao wa Jamiiforums na wengine katika mitandao mingine ikiwamo tovuti ya gazeti la serikali la Habari Leo lililochapisha habari ikimnukuu DCI Manumba kuzungumzia afya ya Dk. Mwakyembe.

Dk. Harrison Mwakyembe

“Ukiona vyombo vya usalama vinacheza na maisha ya raia wake ujue nchi imefika mahali pabaya sana ni suala la muda tu kabla wananchi hawajafikia hatua ya kudai haki zao. Tanzania kupitia Bunge waunde tume yenye lengo la kulifumua jeshi la polisi na kuliunda upya ili liweze kututendea haki Watanzania. Ni aibu kubwa viongozi wakuu wa jeshi la polisi kukubali kutumika kijinga na wanasiasa

ambao wana laana ya Watanzania.

 

DCI Robert Manumba

“Ni matumani yangu viongozi wa dini, asasi za kiraia watapaza sauti zao ili wale wote waliohusika kwa namna moja au nyingine na uovu huu wanafikishwa mahakamani haraka bila kuchelewa,” anasema Mchangiaji wa muda mrefu katika mtandao wa Jamiiiforums (JF) anayejiita Ngongo.

Mchangiaji mwingine wa JF anayejitambulisha kwa jina la Only83, yeye alianza kwa kumlaumu Dk. Mwakyembe kwa kuendelea kuwa ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ambacho kinaendelea kumnyanyasa na kutomsaidia.

“Ninachomlaumu Dk. Mwakyembe ni kuendelea kukaa CCM na kwenye serikali yake wakati wanaendelea kumfanyia vituko…hivi kama wana nia ya dhati ya kumsaidia kwanini wawe na kauli mbili mbili? Hii ni hatari kwa usalama wake. Anapaswa kutambua anapambana na genge kubwa na la hatari. Nashangaa kwa uwezo wake wa elimu na kuchambua mambo anashindwaje kugundua mfumo huu unaomzunguka,” anasema mchangiaji huyo na kuendelea;

“Lakini nadhani polisi na vyombo vya usalama visipuuze hizi habari na kutoa matamko rahisi kama ya DCI Manumba ni kitu kinachoshangaza na kusikitisha. Na hii imekuwa kama mazoea kwa serikali na viongozi wake ni wepesi kutoa majibu rahisi kwa matatizo magumu. Mfano halisi ni huu wa mgomo wa madaktari,Waziri anatoa kauli nyepesi bungeni wakati watu wanakufa. Hii tabia inapaswa kuachwa.”

Mchangiaji katika mtandao wa Habari Leo, yeye alisema;

“Inashangaza kusikia jeshi la polisi kutoa majibu mepesi kiasi hicho wakati malalamiko ya awali ya Dr. Mwakyembe kuhusu njama za kuuwawa na kutaja majina ya watu mpaka gari la polisi na mganga wao wa kienyeji hayajashughulikiwa na hakuna dalili yoyote ya kushughulikiwa na tumeona baadhi ya wanaolalamikiwa wamehamishiwa mikoani ili kuziba ukweli wa kile kinacholalamikiwa. Hatuna jeshi bali tuna kampuni ya mafisadi.”

Mchangiaji mwingine alisema polisi wapo kwa ajili ya kupokea maelekezo tu na siyo kusimamia sheria za nchi akiwafananisha na kompyuta inayosubiri kupewa amri na mtumiaji.

“Tumeshuhudia kesi ngapi zikifutwa pasipo kuwa na sababu, EPA ilipotea mikononi mwa polisi na mahakama, ndio hivyo kwa kupokea maelekezo toka kwa watu fulani ambao ndio wanaoandika katika compyuta,” anasema mchangiaji anayejiita Mizambwa.

Oti Kate yeye anasema, “Mimi nina wasi wasi na uelewa na utayari wa huyu ‘Kayumba’ (Manumba)  katika kujibu maswali.  Katika kujibu swali amesema hivi; Kutokana na uchunguzi wa kipolisi ulioshirikisha Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, hakuna ushahidi juu ya hilo”. ….. baadae  anasema  kazi ya Polisi sio kuchunguza maradhi bali kuchunguza tuhuma, sasa hiyo kushirikisha wizara ya Afya si ndiko wangejua anasumbuliwa na nini? Hapo tayari wizara ya Afya imesha-ridhia kutoa ushirikiano so pamoja na kilichomsibu huyu muheshimiwa…………..dah!”

Katika taarifa yake Jumamosi Februari 18, 2012, Dk. Mwakyembe amesema amekerwa na taarifa ya DCI Manumba kuhusiana na afya yake na kwamba polisi hawajawa na nia ya dhati kuchunguza yanayomsibu.

Taarifa kamili ya Dk. Mwakyembe hii hapa:

“Nimelazimika leo Jumamosi, tarehe 18 Februari, 2012 kutoa taarifa hii kwa vyombo vya habari kufuatia mkutano wa DCI Robert Manumba na waandishi wa habari jana (17/02/12) kuongelea, pamoja na mambo mengine, hali yangu ya afya na kuhitimisha, kienyejienyeji tu kuwa “sikunyweshwa sumu” ila naumwa tu ugonjwa wa ngozi bila kufafanua ugonjwa huo wa ngozi umesababishwa na nini!

“Napenda nisisitize mapema kabisa kuwa msimamo huo wa Jeshi la Polisi umenikera sana katika hali niliyonayo ya ugonjwa, kwanza kwa kuingilia mchakato wa matibabu yangu na uchunguzi wa kina kuhusu kiini chake unaoendelea hospitali ya Apollo nchini India ambako bado sijahitimisha matibabu yangu; pili kwa ufinyu wa uelewa unaojitokeza bayana kwenye tamko la Jeshi la Polisi unaosisitiza kuwa “sikunyweshwa sumu” wakati sumu si lazima unyweshwe ili ikudhuru, inaweza kudhuru hata kwa kugusishwa tu;

“Na tatu kwa Jeshi la Polisi kujiingiza kwenye suala ambalo kwa takriban mwaka mzima halijawahi kuwa na dhamira ya dhati ya kulielewa au kulichunguza mbali na kulifanyia mzaha kupitia magazetini.

“Itakumbukwa kuwa tarehe 9 Februari, 2011 nilimwandikia barua IGP Said Mwema kumtaarifu kuhusu njama za kuondoa maisha yangu na ya viongozi wengine. Kwa kutambua kuwa Jeshi la Polisi la Tanzania daima husisitiza kuletewa ushahidi kwanza ndipo lifanyekazi, nilihakikisha nimeainisha katika barua hiyo kila ushahidi nilioupata au kupewa.

“(Utaratibu huu wa Jeshi la Polisi kusubiri kuletewa ushahidi mezani, kama ambavyo mahakimu wanavyosubiri ushahidi mahakamani, haupo popote pale duniani (ila Tanzania tu) kwani kazi ya msingi ya Polisi si kuletewa, ni kutafuta ushahidi. Polisi wanachohitaji duniani kote ni kupata clue au tetesi tu.

“Hiyo inatosha kufukua ushahidi wote unaohitajika). Pamoja na kujitahidi kuanika kila aina ya ushahidi niliokuwa nao, mambo manne yalijitokeza ambayo yalionyesha wazi kuwa Polisi hawakuwa na dhamira ya dhati ya kupeleleza suala hilo:

(i) Siku chache baada ya kumkabidhi IGP barua hiyo, nilitumiwa timu ya “wapelelezi” ofisini kwangu kuja kuchukua maelezo yangu ya ziada. Timu hiyo ilikuwa inaongozwa na ACP Mkumbo, afisa wa polisi ambaye wiki chache zilizokuwa zimepita alikuwa miongoni mwa askari waliotuhumiwa kupokea rushwa kwa lengo la kumbambikizia madawa ya kulevya mtoto wa Mwenyekiti wa IPP, Reginald Mengi, suala ambalo mpaka leo hii uongozi wa Polisi umeshindwa kulitolea maelezo ya kuridhisha. Kwa msingi huo, nilikuwa nimeletewa mtuhumiwa wa rushwa/ ujambazi kuendesha uchunguzi wa watuhumiwa wengine wa ujambazi! Nikatambua mara moja kuwa zoezi zima lilikuwa la mzaha, tena mzaha mkubwa!

(ii) Wiki chache baada ya barua yangu kuwasilishwa kwa IGP na timu ya ACP Mkumbo “kuanza kazi”, Jeshi la Polisi likachukua hatua ya kuwapongeza na kuwazawadia askari niliowatuhumu kushirikiana na majambazi! Huhitaji kuwa profesa wa falsafa kuelewa kuwa huo ulikuwa ujumbe tosha wa kunipuuza.

(iii) Hivi karibuni tuhuma za askari polisi kujihusisha na vitendo vya ujambazi mkoani Morogoro zilipopamba moto na kuwagusa askari “wale wale” niliowatuhumu kwenye barua yangu, IGP alichukua hatua ya kuwahamishia mikoa mingine!

(iv) ili kunikatisha tamaa kabisa, barua yangu ya “siri” kwa IGP ikavujishwa kwa makusudi kwenye vyombo vya habari na kuchapishwa kama habari ambayo ilikebehi na kukanusha taarifa nzima niliyotoa, sijui kwa faida ya nani! Lakini huu ni mchezo wa kawaida kwa polisi kwani hivi karibuni Mhe. Waziri Samuel Sitta alipohojiwa na ofisa mwandamizi wa Jeshi la Polisi ofisini kwake, wakiwa wawili tu, taarifa ya kikao hicho ikawa magazetini ikikebehi ushahidi aliotoa Sitta! The integrity of the police force leadership is on the line.

Nimeelezea vizuri katika barua yangu kwa IGP kuwa kundi hilo la mauaji lilikuwa limeelekezwa kuniua kwa kutumia sumu, taarifa ambayo kwa karibu mwaka mzima Polisi hawakutaka kuifuatilia kwa sababu wanazozijua wenyewe. Sasa huu msukumo mpya wa Jeshi la Polisi kutaka kujua kama nilipewa sumu au la na kukurupuka kutoa tamko hata kabla ya kunichunguza nilivyo, kunihoji mimi na wasaidizi wangu ofisini na hata kuongea na mabingwa wa Kihindi wanaonifanyia uchunguzi, umetokea wapi?

Aidha napata taabu kuamini kama DCI Manumba na wenzake waliisoma taarifa halisi ya matatibabu yangu au walisoma taarifa “nyingine”, na kama waliisoma taarifa hiyo wenyewe au “walisomewa”! Nasema hivyo kwa kuwa alichokisema DCI Manumba kwa wandishi wa habari hakifanani kabisa na picha iliyo kwenye taarifa halisi ya Apollo ambayo inatamka wazi kuwa kuna kitu kwenye bone marrow kinachochochea hali niliyonayo, kitu ambacho mabingwa wanahangaikia kukidhibiti/ kukiondoa huku vyombo vyetu vya dola vikipelekeshwa na mafisadi kusema bila msingi wa kisayansi na bila aibu: “hakulishwa sumu”, “hakulishwa sumu”!

Nimesoma darasa moja Kitivo cha Sheria Mlimani na DCI Manumba. Baadaye IGP Mwema alikuwa mwanafunzi wangu wa sheria Mlimani. Vigogo hawa wawili wa usalama wa raia nchini hawajanitendea haki, nao wanajua. Wanajua vilevile kuwa sitakaa kimya au kumung’unya maneno come what may pale ambapo haki inakanyagwa.

Tuendelee kuombeana afya na uhai ili kutendeane haki na vilevile tuitendee nchi yetu haki kwa kuvimalizia viporo vinavyokera vya Dowans, EPA, Kagoda n.k. kwa maslahi mapana ya Taifa letu.

Mungu Ibariki Tanzania.

12 Comments
  • POLE SANA DR MWAKYEMBE
    Nakuomba sana uendelee kumtumaini MUNGU katika maisha yako atakulinda na kukushindia katika majaribu unayopitia kumbuka kuwa Mungu ndiye BWANA wa visasi na atapigana kinyume na adui zako na watesi wako watajikwaa na kuanguka

    • suala la ugonjwa wa mwakyembe linahitaji kuepusha hisia binafsi na kuzama ndani zaidi ili kupata jibu sahihi na kisha uamuzi sahihi.

  • suala la ugonjwa wa Dr. Mwakyembe linatakiwa lifanyiwe uchunguzi kwa kina na mambo ya siasa yawekwe kwanza pembeni ili kuweza kupata jibu kamili la ugonjwa wa waziri ili kuweza kuokoa maisha yake kwanza ndo mambo mengine yaendelee.

  • watu wasipende kuongeaongea hovyohovyo bila ya kuwa na uhakika na vitu wanavyoongea lazima uweze kukitetea kitu unachokizungumza na pia uwe na ushahidi thabiti ili hata ukiulizwa maswali juu ya ulichokiongea unayo majibu ya kujitosheleza kutokana na ulichokizungumza

  • NAWAHAKIKISHIENI ANAYEUA KWA UPANGA ATAKUFA KWA UPANGA WALIOHUSIKA NA SWALA LA SUMU KWA MWAKYEMBE NA WANAOENDELEA KUJADILI NAMNA YA KUTOA ROHO ZA WENZAO BADALA YA KUJADILI MAENDELEO WATAONA CHA MOTO KWA KUFANYA HIVYO WANAWASAFISHIA TU WENZAO NJIA YA KUUONA UFALME WA MUNGU NA ROHO NZAO NI MBAYA AFADHALI WAKUSHUSHE MIKUMI UKUTANE NA SIMBA KULIKO KUKUTANA NAO.

  • SIO WANAONGEA OVYO (WAMESOMA UD-CHUO BORA KWA WANASHERIA) ANGALIA MNYIKA, MWAKYEMBE, LISSU, ETC, SO WANAJUA WANACHOKIFANYA. LA KUJIULIZA NI KUWA WANAFANYA KWA NIABA YA NANI? LINGINE TAIFA HILI LINA VIONGOZI, KWANINI WANAKAA KIMYA.

    DR. KASEMA, KAMA KAKOSEA ANGEVULIWA UWAZIRI LA SIVYO POLICE WALIOTAJWA WAONDOLEWE HARAKA SANA, NILITEGEMEA HIVYO. LAKINI WAPIHAKUNA LOLOTE. KIMYAAA MAANA YAKE NINI?? CHAIN NI NDEFU KULIKO TUNAVYOFIKIRI. HAYA NI WAZIRI ANAFANYIWA MZAHA NA TAIFA ZIMA, JE MIMI/WEWE? TUMIA KURA YAKO VIZURI USIWE SEHEMU MZAHA HUU!

  • mambo ni mazito,kutokana na chain kuwa ndefu,hakuna wa kumfunga paka kengele,maisha yote ni ya mashaka matupu,hata presidaa yuko mashakani,uongozi hauna dira,ufumbuzi ni kuuondoa mfumo mzima wa uongozi,tukianzia na kuwa na katiba huru,tume huru ya uchaguzi,ndipo tutapata viongozi huru wenye dira sio hawa.

  • Mambo haya hayahitaji uwe na PHD ili uweze kujua chanzo cha visa hivi ukweli juu ya rasilimali za nchi hii zinagharimu maisha ya mwenzetu ILA ninalojua kwa yeyote aliyehusika ajue UZIMA WA MTU HAUTKANI NA MALI ALIZONAZO BALI KWA NENO LITOKALO KATIKA KINYWA CHA MUNGU wajitathimini wote waone kama uzima wao hutokana na nini?

  • Polisi wetu wanakuaga na taarifa za kiitelegensia kwa vyama vya upinzani pale vinapotaka kuandamana ila inashindwa kufanya uchunguzi kwa mambo muhimu ambayo yanaweza kuatarisha ata usalama wa taifa letu

  • MR.MAKYEMBE, POLE SANA KUU,
    NINACHOSHANGAA MPAKA SASA MZEE MKUBWA NI KITU GANI UNACHOENDELEA KUNG’ANG’ANIA HAPO SISIYEMU NA UTAWALA WAKE,,PAMOJA NA KUA ULISHAJUA KUNA TUHUMA ZA KUTAKA KUKUUA, JE WAONA CHEO CHAKO NI BORA KULIKO UHAI ULIONAO?,,NINA WASIWASI PIA UMESHALILISHWA SUMU YA UONGOZI NA KUJISAHAU KUTUMIKIA NCHI YAKO, UKWELI NI KWAMBA KWA UGONJWA ULIOKUPATA HIVI KARIBUNI UMESHAPUNGUZA MAISHA YAKO ULIYOTAKIWA KUISHIA HAPA CHINI…NINACHOSHAURI KAMA MKEREKETWA NI KUWA, KATIKA BOTI ULIYOPO INAZAMA, NA HUWEZI KUIKOA ISIZAME,,NI BORA UCHUKUE HATUA NA KURUDI UFUKWENI KABLA HAMJAFIKA MBALI..
    NAKUTAKIA MAISHA MEMA..

  • pole baba, ila kwa upande mwingine wewe mwenyewe unachochea hali uliyonayo. coz unajua ndani ya hicho chama chenu mnachofanya kwa nini hutoki? una tu confuse sana. ili uwe unasimamia unachohubiri lazima uwe serious na pia u take action

    • Ni kweli kaka unachosema ndani ya ccm kuna siri nzito na siri hizi haziwezi kufichuka kirahisi WATANZANIA ndio muda muafaka kufichua siri hizi na si kutegemea viongozi wawahamasishe!

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *