‘Teni pasenti’ kuwaponza watumishi wa Tanroads Kilimanjaro

Jamii Africa

ASILIMIA 10 ya malipo ya rushwa na upendeleo, huenda “ikawatokea puani” watumishi wawili wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), mkoani Kilimanjaro.

Inadaiwa kuwa watumishi hao wamekuwa maarufu kwa kupokea asilimia hiyo, maarufu kama –teni pasenti- bila woga.

Watumishi hao tayari wameanza kuchunguzwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambanana Rushwa (Takukuru) baada ya Ikulu kuagiza kufanyika kwa uchunguzi huo.

Ikiwa uchunguzi utakamilika, wanaweza kushitakiwa mahakamani kwa matumizi mabaya ya madaraka na hata rushwa.

FikraPevu imepewa taarifa kutoka serikalini kwamba baada ya Ikulu kupokea barua ya malalamiko kutoka kwa makandarasi wa Kilimanjaro, iliagiza Takukuru kuanza uchunguzi “mara moja.”

Kuanza kwa uchunguzi huo kunafuatia barua iliyoandikwa na makandarasi wa Mkoa wa Kilimanjaro kwa Rais Dkt. John Magufuli, baada ya kudai kwamba “wameshindwa kusaidiwa na ngazi zingine,” hivyo kuomba kusaidiwa na ofisi namba moja, Ikulu.

FikraPevu imeiona barua iliyoandikwa kwa Rais Magufuli na makandarasi hao wakitaka kuchunguzwa na kuchukuliwa hatua kwa watendaji hao wa Tanroads.

Barua hiyo ya malalamiko inaonesha kuandikwa Februari 28, 2017 na kwamba ilifikishwa Ikulu, Dar es Salaam baada ya siku nane, yaani Machi 6, 2017.

Takukuru wazungumza

Ofisa mmoja kutoka Takukuru, Makao Makuu Dar es Salaam, ameiambia FikraPevu kwamba kweli uchunguzi umeanza na unafanywa na watendaji ambao hawako Kilimanjaro.

“Sina haja kukueleza wanafanya nini na kina nani wanachunguzwa, lakini elewa timu yetu ipo makini huko na kazi zinaendelea,” alisema, huku akisisitiza “usiweke jina langu popote.”

Taarifa zilizopatikana kwa FikraPevu zinadai kuwa watumishi hao wa Tanroads wamekuwa wakitumia nafasi zao, hasa “kuwaminya” makandarasi kwa kuomba rushwa ndipo wapate zabuni.

Malalamiko ya makandarasi wa Kilimanjaro kwa baadhi ya watendaji wa Tanroads, Kilimanjaro yamekuwa yakipazwa mara kwa mara na makandarasi, huku wakieleza kuwepo kwa kampuni mbili tu zinazopewa upendeleo.

FikraPevu haitataja majina ya kampuni hizo kwa sasa kwa kuwa hazikufikiwa mapema. Kazi inaendelea kuzifikia.

Uongozi Tanroads wazungumza

Meneja wa Tanroads Kilimanjaro, Ntije Nkolante, amekiri kuwepo kwa malalamiko hayo, lakini akadai kuwa makandarasi hao siyo wakweli kwani uamuzi wa nani apewe kazi, haufanywi na mtu mmoja wala wawili, ni jopo la wataalam.

“Zipo bodi nne zinazohusika hadi kupatikana kwa mzabuni ambaye anapewa kazi, hivyo siyo rahisi kuchakachua kwa namna yoyote ile,” anaiambia FikraPevu.

Ntije anasema kuna timu ya tathmini, kitengo cha ununuzi, menejimenti na meneja mwenyewe, hivyo siyo rahisi kwa watu wawili kushawishi wengine ili kupendelewa kwa kampuni moja au mbili.

Katika malalamiko ya makandarasi hao, wanaitaja kampuni moja iliyopewa zabuni ya kujenga madaraja eneo la KIA, lakini ilishindwa kutekeleza mradi huo kwa madai ya kutokuwa na uwezo.

Meneja huyo wa mkoa amekiri kampuni hiyo kupewa kandarasi na kushindwa

kutekeleza mradi huo, lakini akaitetea kwamba mradi ambao kampuni hiyo imeshindwa ni mdogo ikilinganishwa na miradi mikubwa iliyotekeleza wilayani Same, Kilimanjaro.

“Ni kweli hiyo kampuni imeshindwa kujenga hayo madaraja kama ilivyoomba na kushinda zabuni, lakini tunashindwa kuelewa ni kwa nini imeshindwa mradi mdogo kama huo, wakati imetekeleza miradi mikubwa wa kujenga karavati kubwa wilayani Same,” Ntije ameiambia FikraPevu.

Tunachokijua

Tanroads Kilimanjaro imekuwa ikilalamikiwa mno kwa madai ya rushwa kwa kazi nyingi za ujenzi wa barabara zinazotolewa kwa kampuni za ndani au nje ya nchi.

Madai haya ya makandarasi yamekuwa yakielezwa “kukomea” ngazi ya mkoa au taifa, bila uchunguzi kufanywa.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *