Katavi: Ziara za viongozi kero kwa wanafunzi. Wamsubiri DC kuanzia saa tatu asubuhi, yeye awasili saa saba mchana

Jamii Africa

WALIMU na wanafunzi katika Wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi wamelalamikia tabia ya viongozi wa serikali kuwalazimisha kushiriki shughuli ambazo hata hazihusu maendeleo yao kielimu.

Wakizungumza na FikraPevu kwa sharti la kutotajwa majina yao, walimu na wanafunzi hao wamesema ziara za viongozi wa kiserikali mara nyingi hukwamisha shughuli za kielimu kwa kuwataka washiriki mapokezi na kuvunja vipindi.

Wanafunzi wa Shule ya Msingi Vikonge katika Wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi wakiwa wamekatishwa vipindi vya masomo kwa ajili ya kuhudhuria makabidhiano ya jengo la Ofisi ya Kijiji baina ya taasisi ya Jane Goodall na Serikali Machi 24, 2017.

 

Aidha, wamesema, hata pale wanapovunja vipindi hivyo, vingozi wengi hukawia kuwasili hata kwa saa tano, na wakati mwingine kuahirisha ziara zao, jambo ambalo kwa kiasi kikubwa linavuruga utaratibu wa masomo.

“Kukiwa na ziara tu basi siku nzima inabidi tuvunje vipindi kwa sababu mnaweza kuambiwa viongozi wanakuja saa nne, lakini mtakaa hapo huku wanafunzi wakiimba hadi saa nane mchana, huu si uungwana,” walisema walimu hao.

Mbali na ziara za viongozi wa kimkoa au kiwilaya, watoto wa shule pia huwa nje ya madarasa nyakati za sherehe mbalimbali.

Machi 24, 2017, FikraPevu ilishuhudia wanafunzi katika Shule ya Msingi Vikonge wilayani Tanganyika wakikatiza masomo kwa ajili ya kwenda kushuhudia makakabidhiano ya Ofisi ya Kijiji hicho.

Hili ndilo jengo la Ofisi ya Kijiji cha Vikonge alilokabidhiwa Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika, Salehe Mhando, na taasisi ya Jane Goodall ambayo ililijenga kwa gharama ya Shs. 50 milioni.

 

Ofisi ya Kijiji cha Vikonge iliyojengwa na taasisi ya kimataifa ya Jane Goodall, imegharimu Shs. 50 milioni na siku ya tukio, watoto hao wa shule walifika eneo la tukio kuanzia saa tatu asubuhi.

Kwa mujibu wa taarifa za awali, ilikuwa imepangwa kuwa mgeni rasmi katika shughuli hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika, Saleh Mhando, afike eneo hilo saa tano asubuhi.

Aidha, baada ya viongozi kugundua kuwa wanafunzi walikuwa wakifanya mahojiano ya kawaida na waandishi wa habari, Ofisa Tarafa ya Kabungu akalazimika kuingilia kati na kuwaondoa wanafunzi hao akiwaelekeza kurudi shuleni.

Wakati Ofisa Tarafa huyo anafikia uamuzi wa kuwarejesha madarasani wanafunzi hao, tayari vipindi vya asubuhi kwa siku hiyo vilikuwa vimepita.

Hata hivyo, FikraPevu iliyokuwepo eneo la tukio, ilishuhudia DC huyo akiwasili saa saba mchana ambapo wanafunzi walikuwa wamerejea shuleni.

FikraPevu inafahamu kuwa hao si wanafunzi pekee waliowahi kuathirika na ziara au matukio ya kisiasa na kijamii wilayani Tanganyika na kwingineko nchini, jambo ambalo linakwamisha maendeleo ya elimu.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *