Askari wa Zimamoto Mwanza atafuna stakabadhi kuficha ushahidi

Jamii Africa

ASKARI  wa  kikosi  cha zimamoto    katika  Halmashauri ya Jiji  la Mwanza, Masood  Gadafi amezua  tafrani ofisini  kwake  baada ya kukwidana  na mteja wake na kisha akatafuna  stakabadhi za serikali  kwa lengo la kupoteza ushahidi.

Habari zilizozagaa  jijini hapa zinadai kwamba  licha ya kuidhalilisha  ofisi  ya serikali , askari huyo mwenye cheo cha ‘meja’  bado  hajachukuliwa  hatua  zozote za kinidhamu.
Inadaiwa kuwa tukio hilo lililokusanya umati wa watu wakiwemo wapita njia, lilitokea katika ofisi  za zimamoto  jijini hapa siku ya  Septemba 15 mwaka huu,  kati ya saa 6 na saa saba mchana.
Kwa  sharti la kutotajwa jina  gazetini, inadaiwa  kuwa chanzo cha tafrani hiyo ni ‘uchakachuaji’  unaofanywa na baadhi ya askari wa kikosi cha zimamoto  Jijini hapa.
“ …tafrani hiyo ilitokea  baada ya mteja  mmoja  aliyefamika kwa jina moja la Daniel  kuomba  kupatiwa stakabadhi kwa ajili ya malipo  ya  ‘sticker’ za magari  yake  malori yake mawili  ambayo  yanafanya biashara  katika  wilaya ya Magu” kilidai chanzo cha habari .
Inadaiwa  mteja  wa  askari huyo  alistukia  uhalali wa  stakabadhi  alizokabidhiwa na ndipo  alimkamata  ili  amfikishe  katika  vyombo vya sheria.
“ Pamoja  na kuhoji  uhalali wa zile stakabadhi, mteja  wake alitaka kumkamata  Masood  mara baada ya kubaini kwamba  stakabadhi hizo  zilikuwa  feki. ” inadaiwa.
Habari  zinafafanua kuwa  stakabadhi hizo zilikuwa zimetolewa kwa  ajili ya malipo ya stika za  kughushi (gazeti hili  limepata nakala zae) za malori yenye namba  za  usajili T915AVC  na T394ABV.
Inadaiwa   Masood   kwa kushirikiana na  baadhi ya  wafanyakazi wenzake a kikosi cha zimamoto  Jijini hapa  wamekuwa   wakilalamikiwa  kwamba  wanatoa  sticker  pamoja na  stakabadhi feki  kwa wateja kwa lengo la kujipatia fedha kwa njia  zisizokuwa halali.
Kwa   mujibu wa  habari, askari  huyo  anatumia  vitabu  vilivyoibwa   mwishoni mwa mwaka wa fedha 2010/2011 .
Habari zaidi  zilizothibitishwa  kwa  njia ya simu na Naibu  Kamishna  wa Kikosi cha  Zimamoto  nchini, Maiko   Shija  zinadai  vitabu  hivyo viliibwa katika ofisi ya zimamoto  makao makuu, Jijini Dar es salaam  na kwamba taarifa za upotevu huo  zilitolewa  kupitia  vyombo vya habari.
“ Ni kweli  hilo tukio lipo  lakini ninaomba  uongee na mkuu  wangu wa idara”  alithibitisha Masood huku  akikabidhi simu yake ya mkononi kwa bosi wake  wa idara. ya simu.
Hata hivyo, mkuu  wake  wa idara aliyejitambulishwa kwa jina la  Musa  Kaboni  hakuwa  tayari   kuzungumzia suala hilo  kwa  madai  kuwa  bado  linashughulikiwa  kiofisi.
“ Ni  kweli kwamba  mimi ndiye bosi wake, na ndiye  nilikuwa ninamkaimu  Mkuu  wa kituo cha Zimamoto hapa Jijijini Mwanza; lakini  sina cha kukuambia  zaidi ya  kusema kuwa  linashughulikiwa” alisema  Kaboni  ambaye ni mkuu  wa idara ya utoaji wa stika  zinaohusiana na moto katika magari, nyumba  pamoja na boti  Jijini hapa.
Kwa upande  wake, Mkuu  wa kituo cha Zimamoto  jijini hapa, Julius  Bulambu  alikiri kupokea  taarifa  za kuwepo kwa tukio hilo.
“ Mimi  sikuwepo  wakati tukio hilo linatokea;  aliyekuwa  akikaimu ni  afande  Kaboni. Lakini baada ya kurejea  nilipewa  taarifa ambazo bado ninazifanyia kazi” alidai Bulambu.
Alifafanua kwamba  tayari  ameshachukua hatua, ikiwemo  kumhoji  Masood  na kwamba  bado anasubiri  kupata maelezo ya kutoka kwa  mlalamikaji( mteja  aliyekwidana na  Masood).
Naibu  Kamishna  wa Kikosi  cha  Zimamoto  Makao Makuu  nchini, Maiko Shija,  pia  alikiri  kupokea  taarifa za kuwepo  kwa tukio hilo.
“ Taarifa hizo  ninazo  lakini  wasemaji wakuu  wa  suala hilo ni  uongozi  wa Zimamoto  Jijini  Mwanza  ambao nimeambiwa walishuhudia  wakati  tukio hilo linatokea”  alisema Shija  kwa njia ya simu  na kuongeza kuwa ofisi  yake  inaendelea  kufanya ufuatiliaji.
Kamanda  wa  Polisi  Mkoani hapa, Liberatus  Barlow  alisema  suala hilo bado haljaripotiwa  ofisini kwake.
Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *