Je, Wajua kuwa tabia zako zaweza kukukosesha fursa?

Lady ViVa

Jamii yenye staha ni ile yenye mpangilio, yenye kuheshimu wengine, na inayojishindia heshima kutoka kwa wengine. Kwa vile tabia njema katika jamii ni kitu cha muhimu, basi tujue kuwa vivyo hivyo tabia njema ni muhimu sehemu nyingine nje ya nyumbani ikiwemo sehemu za kazi na maeneo mengine tunamohusiana na watu wengine. Ni uungwana na wajibu kuheshimiana na kuthamini maoni, imani na desturi au tamaduni za wengine.

TABIA NJEMA NA ITIFAKI.

Sehemu ya kwanza: Je, Wajua kuwa tabia zako zaweza kukukosesha fursa?

Utangulizi

Mpendwa msomaji, ni mara ngapi umekaa ukajiuliza swali hili: “Je tabia zangu ni kikwazo kwa wengine?”Jibu laweza kuwa NDIO au HAPANA. Nimeona nikushirikishe mambo haya kwa vile ninaona kuna umuhimu wa kujua ni mambo gani hatuna budi kuyachunguza tena upya ili kama inabidi, tujirekebishe kabla hayajatugharimu.

Kwa kuanzia na kwa kifupi, tabia ni kanuni zilizo rasmi au zisizo rasmi zinazojengwa kupitia malezi au makuzi. Tunafunzwa tabia njema nyumbani; mfano, namna ya kuheshimu wakubwa, kuishi na majirani, kuwajali wengine, kushirikiana na wengine, namna ya kula chakula kwa adabu, staha katika mavazi na mwenendo, n.k. Shuleni wanafunzi hujifunza nidhamu kama namna ya kuwa na adabu na tabia njema. Kadhalika vyuoni na kazini vijana na watu wazima huendelea kujifunza namna ya kushirikiana na kuhusiana na watu wengine kikazi na hata kibiashara. Hii ni pamoja na kutii kanuni na taratibu za sehemu za kazi. Tabia njema sehemu za kazi zinahusisha kanuni na taratibu ambazo mtu hupaswa kujifunza na kuzingatia kila mara. Tunapozungumzia tabia njema, hatuna budi kuzingatia utamaduni na hata imani za kidini za wahusika.

Binadamu tunajifuza na kuziishi tabia hizi kama namna ya kuhakikisha uwepo wa amani, staha na maelewano miongoni mwa wanajamii. Mathalani, nyumbani watu huishi kwa kufuata taratibu ambazo huwekwa na wakuu wa familia ili kuwafundisha wanafamilia tabia na desturi nzuri zinazofanya maisha ya nyumbani yawe ya raha na kuheshimiana. Wazazi au walezi wasipofundisha watoto tabia au desturi zinazofaa, watoto watakuwa bila kujua lipi jema au lipi linakera. Watoto wakikua na kuanza kuchanganyika na wengine, wataonekana wamekosa malezi au wanaweza kuonekana kero kwa wengine kwa vile wanaenda kinyume na matarajio ya wengine katika maeneo mbalimbali. Kumbuka, mtoto umleavyo ndivyo akuavyo na asiyefunzwa na mamaye hufunzwa na ulimwengu!

Jamii yenye staha ni ile yenye mpangilio, yenye kuheshimu wengine, na inayojishindia heshima kutoka kwa wengine. Kwa vile tabia njema katika jamii ni kitu cha muhimu, basi tujue kuwa vivyo hivyo tabia njema ni muhimu sehemu nyingine nje ya nyumbani ikiwemo sehemu za kazi na maeneo mengine tunamohusiana na watu wengine. Ni uungwana na wajibu kuheshimiana na kuthamini maoni, imani na desturi au tamaduni za wengine.

manners

Kwa mfano, wakati wewe unaamini kuwa kuketi  juu ya kiti na kula na kijiko ni desturi na tabia njema, ujue kuna wengine wanaona kuketi juu ya mkeka na kula kwa mkono ni desturi na tabia njema. Zote ni sawa kwa sababu tabia hizo zinatokana na utamaduni na  kawaida za watu mbalimbali na watu wahusika wanaamini hivyo. Kwa kifupi, tabia njema na zinazokubalika ndio mzingi wa kuwa na mahusiano mazunri na watu wengine. Ukiwa unawakera watu kutoka na tabia au vijitabia vyako, ujue utapata hasara siku moja. Kabla hatujachambua tabia hizo na vijitabia vyenye kukera, ni vizuri tuzijue kanuni muhimu zinazojenga mahusiano mazuri.

Kanuni za mahusiano

Tabia inahusika sana katika kujenga au kuharibu mahusiano. Watu wanakua na mahusiano na wengine kijamii na hata kikazi. Uhusiano bora sharti uwe na vitu vifuatavyo:

Kujiheshimu

Ili uheshimiwe lazima wewe mwenyeweujiheshimu. Kadhailika, huwezi kuheshimu wengine kama wewe mwenyewe huna hata chembe ya kujiheshimu.

Kuheshimiana

Ili uhusiano wowote ule udumu, haina budi kuwepo na heshima pande zote.

Kujali na kuhurumia wengine

Uhusiano utaweza kudumu kama pande zote zitajali na kuhurumiana. Hata kama ni biashara lazima kuwepo na hali ya kujali wateja na kuwafikiria unapofanya mambo yako. Usiangalie kuwatoa au kupata kitu toka kwao tu au kutengeneza faida kwa gharama yoyote ile. Wajali wateja wao, ufanye biashara ya halali na kama ni faida basi itokane na kujibidisha kwako pia. Uhakikishe ubora wa bidhaa unazouza au huduma unayotoa. Usipokuwa na moyo wa kujali hutafanikiwa kudumu katika uhusiano wowote.

Ushirikiano

Kufanya jambo pamoja mkiwa na lengo la pamoja kutafanya uhusiano udumu. Ndio maana siku hizi tunasikia sana kuhusu kufanya kazi au shughuli kama timu.

Kuaminiana

Pale watu wanapofanya jambo kama timu, kunakuwepo na kuaminiana japo tunasikia kuna wanachanma wa timi hurubuniwa na kuhongwa kuihujumu timu. Imani hujengwa, haiwezi kulazimishwa au kudaiwa na inajengwa kwa kuzoeana na kujionea matendo na maneno vyote vikiashiria mhusika anaweza kuaminika ama la. Huwezi kujifanya kuwa unaamini, imani inakuja pale ambapo mtu anaridhika na neno au matendo ya mtu. Tunajifunza kuamini sisi wenyewe kwa namna tunavyoona wale tunaowaamini wanavyofanya au yale wanayoyasema.

Kujituma na kujitoa

Katika jambo lolote fanaka inatokana na jinsi wahusika wanavyojitoa na kujituma utekelezaji badala ya kuongea maneno matupu bila vitendo.

Swali: Je mpendwa msomaji, unadhani ni tabia gani zinakera na unaona zinahitaji kurekebishwa? Angalia pale ulipo – nyumbani, kazini, barabarani, mikutanoni, kwenye tafrija, nk.

Niandikie au post hapa kwenye mjadala [COMMENT]

Itaendelea………………… Endelea kufuatilia kolamu hii

3 Comments
  • Ndio ndugu muhariri nimekuelewa, ila liko hili la utofauti wa asili za tamaduni (cultural diversity), kama ulapo umeketi mezani kwa kijiko na kula huku umeketi chini kwa mikono,wote huwa sawa kutokana na uasili wa tamaduni binafsi,ila huwa tofauti kulingana na tamaduni ya mwenzake.

    Mahusiano yapo kwa kila ngazi ya maisha kwa mawasiliano tofauti tofauti,hususani enzi zetu za sayansi na teknolojia, tumelirahisisha hili la mawasiliano, hususani kwa mitandao ya kijamii, ndio wengi tunatofauti wa kimaadili kutokana na makuzi tuliopitia.

    Vipi mtu kuweka bayana yalio ya haki kwa jamii fulani eidha inayo nyanyasika/nyanyaswa na mtu/watu/jamii fulani, ila kwa kufanya hivyo huonekana kuwa na tabia mbovu kwa wachache wenye ajenda na kunufaika nanyi isivyo halali. Mfano, wakoloni na wapigania uhuru, wazalendo na mafisadi, ila sanasana picha inapatikana kwa mkoloni na mpigania uhuru, tuje mpaka ukoloni mambo leo na waupingao!

    • Asante John kwa mchango wako kuntu.

      Mawasiliano yapo tofauti tofauti na kwa muktadha tofauti pia.Suala la cultural diversity nalo lipo na  ni muhimu kulizingatia unapohusiana na mtu kutoka background tofauti na yako.Ukionacho kibaya kwako chaweza kuwa kinakubalika kwa mwingine.Hata hivyo kuna common denominator nayo ni swali hili- " JE KITENDO CHANGU/MWENENDO WANGU UNAUDHI WENGINE"?

       

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *