Mwenyekiti wa CCM mkoani Shinyanga acharuka

Jamii Africa

Na  Juma Ng’oko, Mwanza

MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika mkoa wa Shinyanga, Hamisi Mgeja amesema mbunge wa Kahama, James Lembeli (CCM) hana hekima na pia uelewa wake ni mdogo kuhusu vipengere vya katiba ya Chama hicho tawala.

Mgeja ametoa kauli hiyo kwa njia ya simu, ikiwa imepita siku moja tangu Lembeli alipowaambia Waandishi wa habari Jijini Dar es salaam Aprili 26 mwaka huu kwamba bado kuna viongozi wa CCM wakiwemo wa ngazi ya mkoa wa Shinyanga ambao wanapaswa kujivua gamba kutokana kile alichodai kuwa ni mawakala wa mafisadi wakubwa nchini.

“Mimi sipendi kuzua  malumbano yasiyo ya lazima na ambayo hayana tija kwa chama; ingawa sijui kama huyu mwanachama mwenzangu anazungumza maneno kama hayo akiwa kama Katibu Mwenezi wa Chama Cha Mapinduzi  au kama nani!” alihoji Mgeja wakati alipohojiwa na Fikra Pevu kwa njia ya simu.

Kwa mujibu wa Mgeja, CCM siyo kampuni na kwamba si kila mwanachama ndani ya chama hicho anapaswa kuzungumza  masuala ya chama kupitia vyombo vya habari.

“CCM siyo kampuni, bali ni chama ambacho kina  wasemaji wake kwa mujibu wa katiba ya nchi bhwana! …inawezekana huyu jamaa yetu (Lembeli) haifahamu vizuri katiba ya chama ndiyo maana inafikia hatua ya kuzungumza bila utaratibu” alidai Mgeja .

Alifafanua kwamba Katiba ya CCM imeainisha majukumu, wajibu wa kiongozi pamoja na njia za kuzungumzia  masuala yanayohusu chama hicho.

Mwenyekiti huyo alidai kauli iliyotolewa na Lembeli kwamba ni vema kamati ya siasa  ya mkoa  wa Shinyaga  ijivue gamba haina maslahi kwa chama wala taifa, kwa vile ni mtazamo hafifu alionao  mheshimiwa Lembeli.

Akizungumizia shutuma kwamba uongozi wa CCM mkoa wa Shinyanga ndio umesababisha baadhi ya majimbo yachukuliwe na vyama vya upinzani katika uchaguzi mkuu uliopita, Mgeja  alidai kuwa  wenye haki ya kuibua  hoja hiyo ni wajumbe wa kamati za siasa za wilaya mkoani humo.

Alidai kuwa katika kikao cha tathmini ya uchaguzi kilichofanyika hivi karibuni mkoani humo  hakuna wilaya hata moja iliyotoa hoja ya aina hiyo.

Aliendelea kusisitiza kuwa mbunge ni mtu mdogo sana ambaye hapaswi kujadili mstakabali wa chama hicho.

“…mimi ni kiongozi wa kimkoa, yeye kama mbunge ni mdogo sana ambaye kutoa kauli hiyo ni sawa na  kuchezea sharubu” alisisitiza mwenyekiti huyo huku akiahidi kuitisha kikao na waandishi wa habari ili aweze kutoa ufafanuzi kuhusiana na shutuma zinazomkabili.

Hata hivyo, Mgeja hakuwa tayari kutaja  kwamba ni  wapi atakutana na waandishi wa habari ili aweze kupata fursa ya kujibu tuhuma zinazomkabili.

Aprili 26 mwaka huu, Lembeli akiwa Jijini Dar es salaam alisema kuwa CCM ukiwemo uongozi wa chama hicho mkoani Shinyanga  wanapaswa kujiuzulu  kwa madai kwamba kimejaa mawakala wa mafisadi.

Alisema kamati ya siasa ya mkoa wa Shinganga inayoongozwa na Hamisi Mgeja, nayo inapaswa kujivua gamba kwa sababu kimeshindwa kutimiza wajibu wake.

Kwa  mujibu wa Lembeli, Mgeja pamoja na wajumbe  wa kamati ya siasa  wamechangia baadhi ya majimbo  kutwaliwa na wabunge  kupitia vyama vya upinzani mkoani humo.

Alidai kwamba hali hiyi imesababisha  wananchi  wasiwe na imani  na chama pamoja na serikali yao.

Mbunge huyo alisema ushahidi uko wazi kuwa mkoa wa Shinyanga ndio uliokuwa ngome kuu ya Chama Cha Mapinduzi,  sasa umegeuka kimbilio la vyama vya upinzani ambapo vyama hivyo vimefanikiwa kuvuna kura za kishindo  katika nafasi za ubunge  wakati wa uchaguzi mkuu  uliofanyika Oktoba 31 mwaka jana.

Aliyataja majimbo yanayowakilishwa na wabunge  kutoka vyama vya upinzani mkoani Shinyanga  kuwa ni jimbo la  Bariadi Mashariki, Maswa mashariki, Maswa Magharibi, Bukombe pamoja na jimbo la  Meatu.

Lembeli  alisema kupotea kwa majimbo hayo kumesababishwa na  ufisadi uliopo miongoni mwa  viongozi wa CCM mkoani Shinyanga.

1 Comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *