Polisi watuhumiwa kupiga walinzi wa kampuni; wakidhani majambazi

Jamii Africa

WALINZI  wawili wa kampuni ya Cob Web Security Ltd  wamelazwa katika Hospitali Teule ya Wilaya ya Sengerema Mkoani  hapa, huku mmoja  wao akiwa mahututi baada ya kupigwa na askari Polisi  akidhaniwa kuwa jambazi.

Chanzo cha habari kutoka hospitalini hapo kimemtonya mwandshi wa habari hizi  kwa sharti la kutotajwa jina gazetini kwamba walinzi hao  walijeruhiwa usiku wa kuamkia Mei 31 mwaka huu, wakati wakiwa kazini  katika mtaa wa Misheni mjini  humo.

Walinzi hao wametajwa kuwa Zunya Kaswahili  pamoja na Paul Damas, wote wakazi wa mjini Sengerema.

Habari hizo ambazo pia zimethibitishwa na mmoja wa walinzi hao zinadai   wamelazwa katika wodi namba mbili(wanaume) kutokana na majereha  pamoja na maumivu makali mwilini.

Inadaiwa kwamba walinzi hao walijeruhiwa kufuatia tukio la ujambazi  katika mtaa wa Misheni ambapo mali kadhaa ziliporwa madukani.

” Kwa kweli  hali ya Zunya siyo nzuri kwa sababu mbali na kujeruhiwa na majambazi, pia alipigwa na askari polisi waliofika eneo la tukio baada ya kupokea taarifa za ujambazi” kilidai chanzo cha habari.

Inadaiwa kwamba katika malindo tofauti walinzi hao walipigwa  hadi   Zunya alivuliwa sare  kabla  kuachwa  huku akiwa amepoteza  fahamu .

” Askari  walipofika eneo la tukio  walimkuta Zunya akiwa amelala chini na ndipo walipoanza kumpiga wakidhani kuwa ni miongoni mwa majambazi  yaliyokimbia” alisema mmoja wa walinzi hao  kwa njia ya simu, Paul  Damas wakati akiendelea kupatiwa matibabu.

Alisema  yeye  amepoteza simu yake ya mkononi  na kuongeza kuwa wakati wa purukushani  baina yao na majambazi, mlinzi mwenzao mmoja  alifanikiwa kutoroka wakati akwa na bunduki .

Alifafanua pia kwamba  majmbazi hayo  yalifanikiwa  kupora simu  kwenye duka linalomilikiwa na Simon Chai.

Majeruhi huyo alisema tukio hilo lilitokea majira ya saa 7 usiku na kwamba hadi anakimbizwa hospitali hakuna mtu yeyote ambayo alikuwa ametiwa mbaroni  kuhusiana na ujambazi huo.

Alifafanua  kuwa amejeruhiwa  kwa mapanga kichwani na kwamba hali yake ilikuwa ikiendelea vizuri.

” Zunya  amejeruhiwa vibaya  shingoni, hasa  kwenye mishipa  ya damu” alisema mmoja  wa wahudumu waliokuwa zamu, kwa  sharti la kutotajwa jina kwa vile siyo msemaji wa hospitali hiyo.

Hadi  tunakwenda mitamboni, Meneja  wa Cob Web  Security  Ltd, Tumain Mahinduka  pamoja na Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani hapa, Simon Sirro, hawakupatikana kwa njia ya simu ili waweze kutoa ufafanuzi juu  ya tukio hilo.

Simu  ya Sirro  iliita bila kupokelewa ambapo simu ya Mahinduka  haikuwa hewani.

Na. Juma Ng’oko (Mwanza)

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *