Bwawa la Zumbi limeifanya Nyaminywiri kuwa ‘Selou’ ndogo

Stella Mwaikusa

Kijiji cha Nyaminywiri kinapatikana katika kata ya kipugira wilayani Rufiji katika mkoa wa Pwani, ni umbali wa kilomita 30 kutoka hifadhi za  mbuga za wanyama za Selou  ni mwendo wa nusu saa kuufikia mji wa kibiashara na sehemu wanayofikia watalii wanaotembelea mbuga za Selou mji wa Mloka.

Wakazi wa kijiji hiki wanajishughulisha na kilimo cha Mpunga, mahindi, mbogamboga na Kilimo cha korosho zao kuu la biashara kwa wakazi hao, blla kusahau biashara ya samaki kutokana na kijiji hiki kuzungukwa na maji ya mto Rufiji na Bwawa kubwa la Zumbi ambalo ndio linakifanya kijiji hiki kuwa Selou ndogo.

zumbi1

Bwawa la Zumbi lina historia ndefu katika kijiji cha Nyaminwiri kwani wenyeji wanasema kila kijana anayetaka kazi ya uvuvi basi huanza kujifunzia katika Bwawa hilo, hii ni kutokana na wingi wa samaki wanaopatikana humo ambapo kijana yeyote hujisikia faraja baada ya kuanza kazi na kupata mafanikio yaani kupata samaki wa kutosha

Unapofika katika bwawa hili huwezi kuamini kama kuna kiumbe hai anaishi humo kwani maji yake ni tulivu na yana rangi ambayo ni vigumu kuielezea hii ni kutokana na rangi kuonekana tofauti kila unapojaribu kusogea karibu au mbali.

Nilipotaka kujua ukimya wa bwawa lile mwenyeji wangu alinijibu kwamba hiyo ni ishara ya kuonyesha  kuwa bwawa hilo lina kina kirefu na kukiri kwamba hata wao huvua wakiwa kwenye mitumbwi kutokana na ukweli kwamba bwawa hilo lina chatu wakubwa na mamba ambao ni wakubwa kuliko mamba wote wanaopatikana duniani. 

Ndani ya bwawa hili] wanapatikana samaki wa aina mbalimbali kama vile Kumba,kasa, panga panga, kitoga na  Kambale wote wakipatikana kwa misimu tofauti kwa mfano mwezi  wa oktoba samaki aina ya kumba ndio wanaopatikana kwa wingi na wenyeji wanasema samaki wanaopatikana katika bwawa hilo  ni watamu kuliko wale wa mto rufiji.

Pamoja na kupatikana kwa aina hizo za samaki bwawa hili lina mamba wakubwa  wanaokadiriwa kufikia urefu wa futi 16 na Chatu wakubwa ambao wamekuwa wakionekana mara moja moja lakini hawajahi kuleta madhara.

“Huu ni wakati mzuri wa wataalam wa maji kuja kuchunguza  bwawa hili kwani humu ndani kuna mamba wakubwa ambao tunaamini hawapatikani kokote duniani.” anaeleza askari wa kulinda mazingira ya hifadhi ya kijiji (village game scout) Sultan Omary Mtulya, ambaye hulinda doria katika bwawa la zumbi na maeneo yanayozunguka bwawa hilo ili kuhakikisha mazingira yote yanakuwa salama.

zumbi2

Upande wa pili wa bwawa hilo ambako kuna msitu mkubwa wanapatikana wanyama wa aina mbalimbali kama Simba, Chui, Tembo,Swala Nyati, nguruwepori na nyani ambao hufika kwenye bwawa kwa ajili ya kunywa maji na mara nyingi wanyama hao hufika jioni.

Kaimu mwenyekiti wa kijiji cha Nyaminywiri Yusufu Magenge anasema  tayari wameshazungumza na wanakijiji wa Nyaminwiri na  vijijii vingine vya Kipo na Kipugira ambako bwawa hili linapatikana.

Anasema wamepanga namna ya kujenga mazingira mazuri ya bwawa hili ili kulifanya liwe na hadhi ya kitalii kwani pamoja na mamba wakubwa wanaopatikana humo lakini maeneo yanayozunguka bwawa hilo yana wanyama wa aina nyingi ambayo yanalifanya bwawa hilo kuwa kivutio.

“Mwaka juzi kijiji cha Nyaminwiri kilipata tuzo ya utunzaji wa mazingira yanayozunguka bwawa na tukapata shilingi150,000 hali inayoonyesha kuwa tukiamua kulitengeneza eneo hili kuwa la kitalii inawezekana”, anafafanua  Magenge.

Wavuvi wa samaki katika bwawa hilo nao wanalizungumzia kwa namna tofauti kwani pamoja na kuwepo kwa mamba na chatu katika bwawa hilo wanasema hilo si tatizo kwao kwani mamba hawawasumbui na mara nyingi wamekuwa wakipishana nao japo wakati mwingine huchana nyavu zao pale wanaponasa kwenye mitego ya samaki, lakini wanasema inapotokea hali hiyo basi hushona nyavu zao na kuendelea na kazi.

Pamoja na pilika za kupishana na mamba wakubwa katika bwawa la zumbi wavuvi wanasema wingi wa samaki waliopo katika bwawa hilo huwasahaulisha machungu yao na kujikuta wakifikiria zaidi faida wanayoipata kutokana na kuuza samaki  na kuendesha maisha yao ya kila siku.

“Huwa navua mpaka samaki mia 400 kwa siku na kila ninapovua nina uhakika wa kuwauza kwani tuna wateja kutoka maeneo mbalimbali.” anaeleza Amiri Omary Kuyawa ambaye ameanza kuvua kwenye bwawa hilo tangu mwaka 2006.

Anasema maeneo ambayo hutegemea samaki kutoka katika bwawa la zumbi ni kibiti,ikwiriri na wengine huku wateja wengine wakitokea Dar es salaam.

Anasema ng’ambo ya bwawa hilo ambako kuna msitu ni mapumziko ya wavuvi wengi kutokana na kivuli kizuri cha msitu huo pamoja na matunda pori kama makoche na mabungo yanayopatikana huko.

Anasema mara nyingi wanaenda kwenye msitu huo muda wa mchana kwani muda huo wanyama  kama Tembo, Simba na chui  wanakuwa bado hawajashuka kunywa maji.

Omary Kuyawa anakiri kupungua kwa samaki kutokana  na watu wengi kutoka maeneo mbalimbali kama utete na Ikwiriri kufanya kazi  ya uvuvi katika bwawa hili  lakini pamoja na hali hiyo  anasema kila mtu anapata riziki yake.

Kutokana na kuongezeka kwa wavuvi katika bwawa hilo viongozi wa kijiji pamoja na walinzi wa bwawa hilo wameweka utaratibu wa kuvua kwa sasa wavuvi wanapewa ruhusa ya kuvua mwezi wa tisa, kutoka mwezi wa saba mpaka mwezi wa pili ili kutoa nafasi ya samaki  kuzaliana na kuhakikisha samaki hawaishi katika bwawa hilo.

Mlinzi wa bwawa na mazingira yanayozunguka bwawa hilo Rashid Bakari  anasema wapo wavuvi wanaokiuka taratibu walizojiwekea na inapotokea hivyo nyavu za wavuvi hao huchukuliwa na kuchomwa moto, anasema  mhalifu analipa faini ya shilingii 20,000 katika serikali ya kijiji.

“Si wavuvi tu wapo baadhi ya watu kutoka kijijini huingia kwenye msitu unaozunguka bwawa na kukata miti na wengine huchoma moto kwa sababu zao wanazozijua hao ni lazima tuwakamate, anasisitiza bwana Mgawa.

Bwawa la Zumbi linapatikana katika vijiji vitatu,  Kipo, Kipugira na Nyaminywiri.

2 Comments
  • Niliishia katikati baada ya kuona kimya kimezidi, nia yangu ilikuwa kufika ng'ambo  ambako mamba wanaotea jua lakini nikachemka na kumwambia mwendesha mtumbwi anirudishe haraka!

     

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *