Elimu inatakiwa ili kuondoa tatizo la utapiamlo Wilayani Uvinza

Winfrida Bwire

TATIZO la utapiamlo wilaya ya Uvinza limekuwa likishika kasi kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo za ulaji duni wa chakula unaotokana na kula milo michache na yenye upungufu wa viinilishe.

Ili kujua kitakwimu tatizo la lishe wilayani Uvinza kuliendeshwa utafiti maalumu ambao matokeo yake hayakuwa ya kuridhisha.Jumla ya watu 444, kati yao 342 likiwa ni kundi la watu wenye umri wa miaka 5 na zaidi, na 112 ni  watoto waliochini ya miaka 5 lilifanyiwa utafiti.

Kwa kuangalia kadi ya maendeleo ya mtoto kliniki, imebainika kwamba kuwa watoto wenye utapiamlo walikuwa  55 sawa na asilimia 49 na wenye lishe watoto 57 sawa na asilimia 51. Matokeo hayo yanatoa taswira isiyiopendeza kwa taifa la kesho. Ukuaji wa aina hii unaleta kuwa na kundi la watu ambao kufikiri kwa haraka kunakuwa tatizo.

Vilevile takwimu zinaonyesha kuwa watoto wa miaka zaidi ya mitano wenye utapiamlo ni 20 sawa na asilimia 6, wenye lishe ya kutosha  127 sawa na asilimia 37, uzito uliozidi 137 sawa na asilimia 40, na wenye udumavu 43 sawa na asilimia 13.

Kuwapo kwa tatizo kwa watoto wachanga kunaambatana na lishe duni kwa wanawake wanapokuwa waja wazito.

“Kipindi cha mimba kutungwa  ni muhimu kwa mama mjamzito, kula mlo wa uhakika mpaka anpojifungua na mtoto kutimiza miaka miwili ndio tathimini inayoeleza hali halisi ya ubinadamu yaani siku 1000” alisema  bwana  afya  wilaya , Ernest R. Teyumwete

Pia aliongeza kuwa ulaji duni kwa mama mjamzito unapelekea watoto kuwa na uelewa mdogo katika elimu ambao unaunda taifa lisilokuwa na watu wenye uelewa wa haraka kama inavyotokea sasa kwa baadhi ya wanafunzi kuwa wazito darasani.

Asilimia 75 ya kaya wilayani Uvinza wanakula mlo mmoja na upo chini ya viwango hali ambayo hupelekea kuwa na watoto ambao wanauzito pungufu ya umri wao, Salima Salumu ni mtoto mwenye umri wa miaka miwili lakini anauzito wa kilo nane ambao ni sawa na uzito wa mtoto wa miezi saba hadi nane.

Nilipozungumza na mama yake, hakuonekana kukata tama, anaamini kwamba mtoto wake atakua kama wengine walivyokua.

“…..sasa utafanyaje kama uwezo wenyewe ndo huo nilionao Mungu atatusaidia atakua mbona wote wanakua katika hali hiyo…..” alisema mama Salima ambaya hakupenda jina lake kutajwa.

Pamoja na maelezo ya mama huyo hali ya afya ya mtoto hairidhishi pia ni hatari kwa afya ya mtoto hata katika makuzi kama inavyoeleza kauli mbiu ya masuala ya lishe mwaka huu kuwa ‘afya bora ni matokeo ya lishe bora,jali lishe ya mama mjamzito na mtoto kwa maendeleo ya taifa”

Akithibitisha hayo daktari  hospitali ya Nguruka Ndugu Beatrisi Mtesigwa amesema kuwa wazazi wengi hawazingatii lishe kwa watoto hasa waliochini ya umri wa miaka mitano na kwa mama mjamzito hali ambayo ni hatari hata wakati wa kujifungua.

“Mama asipokula vizuri wakati wa ujauzito uhakika wa kujifungua mtoto aliyechini ya uzito ni mkubwa,” alisema daktari Beatrice Mtesigwa

Mzee Mohammed Ally Ruvakule mwenye umri wa miaka 52 akizungumzia sababu za kuwa na uzito wa kilo 54 anasema kuwa shughuli zake za ulinzi zinamalipo ambayo hayatoshelezi mahitaji ya mlo.

“Nimekuwa nikila mara moja kwa siku kutokana na hali yangu kuwa duni, nakula pale ninapopata kitu kidogo kulingana na hali ya uchumi kuwa ngumu, na huwa nakula saa 8-9 mchana ili niweze kustahimili mpaka kesho yake muda kama huu.” Alisema mzee Mohammed

Hali hii inakumba wanafamilia wengi ambao pia hulazimika kuwa na chakula cha pamoja bila kujali rika na umri  wanapokuwa wakila pamoja . unakuta kwa baadhi ya familia watoto wa umri kuanzia miaka2 hadi 10 wanakula katika sahani moja kwa pamoja hali ambayo inapalekea kwa yule mdogo asiyekuwa na bidii ya kula kutotosheka na chakula kilichoandaliwa.

Bado Serikali inaendelea kukabiliana na changamoto ya uelewa mdogo wa wananchi kuhusu masuala ya lishe katika jamii, kuanzia ngazi ya familia. Lishe ikiboreshwa itasaidia kupanga mikakati ya kupambana na utapiamlo mkali hasa kwa watoto waliochini ya umri wa miaka 5 na wajawazito, ilikulinusuru Taifa kutokana na kuwa na kizazi chenye uelewa mdogo na hatimaye kuipunguzia serikali mzigo wa umasikini.

Kama kila mtu atazingatia ushauri wa Mheshimiwa Rais Jakaya Kikwete alioutoa siku ya Uzinduzi wa kampeni  ya lishe kitaifa Mwezi Mei, 2013, mabadiliko makubwa ya lisahe yatapatikana na kulinusuru taifa.

Mkoa wa Kigoma ambao umezindua rasmi kampeni ya lishe ki-mkoa katika wilaya ya Uvinza mnamo tarehe 18 mwezi machi 2014 unastahili kuamka na kuangalia sera ya lishe nchini, kuitafakari na kutafuta njia ya kuitekeleza.

Sera ya lishe ya mwaka 2006 inaelekeza kwa undani nini maana ya lishe kwa kuangalia majumuisho ya hatua mbali mbali tokea chakula kinapoliwa na jinsi  miili yetu inavyochukua virutubisho na kuvitumia katika kumpatia mlaji afya bora.

Kwa maana hiyo, kuwepo kwa chakula kinachotosheleza mahitaji ya lishe kuanzia mtu binafsi, kaya hadi taifa ni muhimu kwa afya na maendeleo ya jamii. Chakula cha kutosha kitapatikana kama kuna uhakika wa chakula katika ngazi zote kuanzia kaya hadi taifa.

Kwasababu lishe limekuwa tatizo kwa akina mama wengi kutozingatia ulaji wa watoto wao hasa waliochini ya umri wa miaka mitano hivyo kupelekea watoto wao kuwa na afya mbaya inayoweza kushambuliwa na magonjwa kiurahisi kupoteza maisha kutokana na utapiamlo ni vyema kuwepo na kampeni maalumu zinazozingatia uvunjaji wa tamaduni zinazosababisha upungufu wa chakula na mwenendo wa lishe.

Utapiamlo ni hali mbaya ya lishe inayosababishwa na mambo mbali mbali ikiwa ni pamoja na ulaji usiofaa. Utapiamlo unaweza kusababishwa na kula mlo ulio na virutubisho vichache au vingi kulingana na mahitaji. Kula mlo wenye virutubisho vichache visivyokidhi mahitaji huleta upungufu mlo; wakati mlo wenye virutubisho vilivyozidi mahitaji huleta kiribatumbo.

Kwa kuangalia kilimo na shughuli zinazofanywa na watu wa Uvinza upo uwezekano wa kuondoa tatizo la utapiamlo na kiriba tumbo kama elimu sawasawa itatolewa kuhusu kilimo na chakula stahiki kwa mwili wa mama mjamzito na mtoto wake.

2 Comments
  • Nimeiona doc.yako ya lishe.mimi ni afisa lishe wilaya kasulu na nimeshiriki katika uzinduzi wa lishe mkoa kigoma hapo uvinza.Document yako haionyeshi waythrough,ingawa umeonyesha matatizo ya wanajamii.ukizingatia kwamba maisha ya watu wa uvinza ni duni na wanakaya wengi hawawezi kupata walau milo mitatu kwa siku.nini kifanyike?,mimi naona kupitia TAsaF awamu ya pili watu wajengewe uwezo wa kujitegemea,hususani akina mama wajawazito,maana ndipo udumavu unapoanzia.

  • James Ngalaba unachokisema ni sawa, mimi pia ni mdau wa lishe (Nutritionist).
    Wewe kama Afisa Lishe ya wilaya ya kasulu hali ikoje wilayani kwako? Ni mikakati gani uliyoanza kuitekeleza kutatua matatizo ya kilishe yanayokumba wilaya yako na wilaya jirani kama Buhigwe?
    Mwandishi kazungumzia suala la Elimu ya Lishe itolewe zaidi, kitu ambacho ni sahihi.
    My take: Tuwashirikishe pia wadau mbalimbali wasaidie kukuza uchumi + elimu ya lishe wananchi watakayokuwa wamepata+utekelezaji wake =Taifa lenye Afya njema. Asante.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *