Huduma ya simu bure kwa wahudumu wa afya na madaktari nchini itawafikia walengwa vijijini?

Mariam Mkumbaru

Mawasiliano ya simu ni njia moja wapo ya kupunguza vifo vya wajawazito na watoto chini ya umri wa miaka mitano na wagonjwa wengi, lakini katika zahanati na vituo vya afya sehemu za vijijini hakuna mawasiliano ya simu ambayo yanayoweza kurahisisha kupata gali la kubeba mgonjwa kumpeleka katika kituo cha au hospitali ya wilaya.

Nimepata fulsa ya kutembelea zaidi ya zahanati saba na kituo cha afya sehemu mbalimbali za hapa nchini, lakini cha kushangaza maeneo hayo niliyofika hakuna mawasilino ya simu za mkononi, kitu kinacho changia ongezeko la vifo vya wajawazito.

Hivi karibuni Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dk. Seif Rashid amezindua huduma ya bure ya upigaji wa simu kwa wahudumu wa afya na madaktari nchini, kwa kushirikiana na kampuni moja ya simu za mkononi na Switchboard.

Lengo ni kurahisisha huduma za afya katika maeneo mbalimbali, lakini je? walengwa wenyewe kama  wahudumu wa afya, madaktari na waganga vijijini wataifikia huduma hiyo ipasavyo na kuwasaidia kufanyakazi kwa ufanisi na kutoa huduma bora kwa jamii? au watanufaika kwa wale walioko mjini na wale wa vijijini watabaki kusikia kwa wenziwao wanaishi sehemu yenye mawasiliano ya simu?

Nimefika katika zahanati ya ifinga katika kijiji cha ifinga kata ya Matumbi wilaya ya Songe mkoa wa Ruvuma, ni takribani kilometa 219 kutoka songea mjini mpaka ifinga.

Kutoka barabara kuu ya kwenda songea mjini mpaka ifinga ni kilometa 48, ukipanda pikipiki kuelekea ifinga ukifika kilometa 20 ndio mwisho wa kupata mawasiliano ya simu ya mkononi, kuanzia hapo mpaka unafika ifinga kilometa 28 hakuna tena mawasiliano ya simu ya mkononi.

Tulipofika katika kilometa 20 kutoka barabara kubwa ya kwenda songea mjini kuna sehemu inaitwa kona kali, juu ya kilima na kuna kona kali kweli, hapo naambiwa na mwenyeji wangu mganga wa zahanati ya Ifinga Tobias Millinga ndio mwisho wa mawasiliano.

Nilishangaa sana kusikia hilo lakini ndio ukweli wa mambo kwamba ndio mwisho wa mawasiliano niwapigie ndugu zangu, bosi wangu na marafiki maana baada ya hapo hakunua tena mawasiliano mpaka nitakapo rudi mjini.

Bila ya kusita nilichukua simu na kuongea na ndugu zangu na bosi wangu kwamba hapa nilipofika ndio mwisho wa kupiga simu na kupokea simu, hutonipata tena mpaka nitakapo maliza kazi ya kufanya utafiti wa afya ya uzazi kwa wiki moja nikiwa huko ifinga.

Nilipomaliza kuwasilina na ndugu na bosi wangu safari ya kwenda ifinga ikaanza tena, tulifika Ifinga saa 1:30 ya usiku tukiwa hoi, naingia ndani kwa mwenyeji wangu Mganga Tobias Millinga anatoa simu naangali hakuna mawasiliano.

"Mawasiliano ni ndoto  za alinacha hapa ifinga tumeomba tuwekewe hata simu ya upepo ili tuweze kupiga simu katika kituo cha afya madaba ambapo ni kilometa 87 kutoka ifinga ili watuletee gali la kubeba mgonjwa lakini wapi mpaka sasa imekuwa hadithi tuu, Mbunge watu Jenista Mhagama alipokuja katika kampeni mwaka 2010 alisema nitawaletea wataalamu wapime wapi utafungwa mtambo wa mawasiliano lakini toka alivyopata kula mpaka sasa hajaonekana ifinga, sie ni wamwisho tuu kwa kila tuu,"alisema John Ndunguru

Millinga alisema kuwa mwaka jana wajawazito wawili wamepoteza maisha kwa sababu ya kutokwa na damu nyingi wakati wa kujifungua, hakuna  mawasiliano ya kupiga simu katika kituo cha afya madaba ili walete gali la kubeba wagonjwa, mpaka kuchukua pikipiki mpaka kufika madaba wajawazito walifariki njiani maana njia nayo ni mbovu.

Hata madawa yakiisha inakuwa ngumu kuagiza kwa sababu hakuna mawasiliano ya simu za mkononi, inakuchukua muda wa wiki moja hadi mbili kwenda mjini kuchukua dawa kipindi ambapo zimeisha, kwa sababu huwezi kuagiza uletewe kwa kukosa mawasiliano inakubidi uondoke kwenda mjini na kuacha zahanati haina dawa hata moja.

Kwa sasa ifinga inawakazi wapata 32,00 kwa mujibu wa sensa ya mwaka jana na mahitaji yao makubwa ni mawasiliano ya simu na barabara, kwani yatasaidia kupunguza vifo vya wajawazito na watoto ifinga.

Kwa upande wa wilaya ya Nachingwea mkoa wa Lindi, nako hali ndio mbaya zaidi katika suala zima la mawasiliano kwa sababu kakribani vijiji saba hakuna mawasiliano ya simu ya mkononi.

Nikielekea katika kijiji cha Kiegei kata ya Kiegei  ni zaidi ya kilometa 120 kutoka Nachingwea mjini, nako hali ni hivyo hivyo hakuna mawasiliano ya simu na kila kijiji kuna zahanati na kituo cha afya kimoja.

Napanda pikapu kuelekea katika kijiji cha Kiegei, lakini njiani napita vijiji sita ambavyo vyote vina zahanati, inanilazimu kushuka na kwenda kuongea na wahudumu wa afya, mama mkunga na mganga kama wapo na kuangalia mazingira yalivyo na upatikanaji wa huduma kwa mjamzito na mtoto.

Nafika katika kijiji cha Mtua nashuka na kwenda katika zahanati ya kijijini hapo nakutana na mhudumu wa afya anayeitwa Hajira Salumu anamika 12 katika kutua huduma za mama na mtoto toka ameanza kazi hiyo, aliniambia mtua kuna wakazi 7,680 wote wanategemea zahanti hiyo lakini hakuna mawasiliano ya simu.

Nimetoka mtua nakwenda kijiji cha Chimbendenga nakutana na Baby Msangi, mhudumu wa afya anahudumia zaidi ya wakazi 5,000 lakin hakuna mawasilino ya simu.

Pia nafika katika kijiji cha Mbondo kata ya Mbondo Tarafa ya Kilimarondo nakutana na mhudumu wa afya Khadija Chuachua, anasema anatoa huduma zaidi ya wakazi 3,000 lakini hakuna mawasilino ya simu ikitokea mjamzito ameshindwa kujifungua tunampakiza katika pikipiki na kumpeleka kilimarondo kituo cha afya ni zaidi ya kilometa 30.

Nafika kijiji cha Nahimba nakutana na mhudumu wa afya Bona Makwinya anatoa huduma kwa wakazi wapatao 1,325 lakini hakuna wasiliano ya simu, anatoa huduma hiyo kwa muda wa miaka mitatu bila ya kuwa na msaidizi katika zahanati hiyo yeye anawazalisha wajawazito, anapima watoto, anatibia wagonjwa wa aina zote kwa wakazi hao.

Kilimarondo ndio kituo cha afya hapa nakutana na Sharifa ng'ombo ni mama mkunga, kuna gali la kubeba wagonjwa lakini halitumiki kama lilivyoletwa kwa sababu vijiji vyote vyenye zahanati hakuna mawasiliano ya simu ya mkononi, ni ngumu sana kumpigia dereva kumwambia wahisha gali kuna mgonjwa, gali linapaki tuu nje ya kituo cha afya kila siku.

Matekwe kuna zahanati na kutana na Lidia Ulio ni mhudumu wa afya anahudumua wakazi 2,548, aliyeanza kazi mwaka 1986 katika zahanati ya lihonji mpakani mwa wilaya ya Liwale, mpaka sasa anamika 20 katika kazi ya kuwazalisha wajawazito lakini mara zote hutumia simu yake ya mkononi kama tochi ya kumsaidia mjamzito usiku wakati wa kujifungua, kwa sababu hakuna umeme wa jua na hakuna mawasiliano ya simu.

"Mwaka jana nilimzalisha mjamzito mmoja baada ya mtoto kutoka vema kondo la nyuma la uzazi liligoma kutoka, simu ninayo lakini huku hakuna mawasiliano ya simu ambayo yangeniwezesha kupiga simu katika kituo cha afya ili walete gali la wagonjwa wamchukue mjamzito huyo, ikabidi ipakizwe kwenye pikipiki mpaka kituo cha afya kilimarondo ambako ni takribani kilometa 20 kutoka Matekwe," alisema Lidia.

Safari yangu imefika mwisho kwa kufika katika zahanati ya Kiegei nakutana na mhudumu wa afya Asimini Omari anatoa huduma kwa wakazi 17,500 hakuna mawasiliano ya simu, mwaka jana wajawazito wawili wamepoteza maisha kwa sababu ya kupakizwa katika pikipiki zaidi ya kilometa 25 ili kuwahi kusafishwa baada ya mimba kuharibika na zahanati ya kiegei haina kifaa cha kumsafisha mjamzito mimba ikiharibika.

Swali la msingi la kujiuliza hayo mawasiliano yaliyozinduliwa hivi karibuni na Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, yataweza kuzaa matunda na kupunguza vifo vya wajawazito na watoto waliozaliwa chini ya wiki nne na watoto wa chini ya miaka mitano, sio tuu kwa wajawazito lakini pia kwa wagonjwa wa aina nyingine na kuleta ufanisi katika kutoa huduma za afya nchini?

Asilimia 75 hadi 80 ya watanzania wanaishi vijijini na huko ndio kuna zahanati na vituo vya afya lakini hakuna mawasiliano ya simu za mkononi, je huduma hiyo ya kupiga simu bure katika hospitali ili kurahisisha huduma ya afya itafanikiwa?

Maoni yangu wafunge minara ya simu au kuweka hata simu za upepo ili kurahisisha upatikanaji na ufanisi wa kutoa huduma za afya pale inapotokea tatizo la haraka mganga au mhudumu wa afya aweze kupiga simu katika kituo cha afya au hospitali kupata msaada wa gali au mtaalamu wa kumsaidia mgonjwa asipoteze maisha, lakini sehemu nilizokwenda wajawazito ndio wanaoathirika sana kwa kukosa huduma bora wakati wa kujifungua na baada ya kujifungua kama atapatwa na tatizo la uzazi.

1 Comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *