Mzimu wa Balalli waibuka ‘twitter’ – Salamu kutoka kuzimu?

Jamii Africa

Katika hali ambayo inaonesha kuweza kuja kulitetemesha taifa kupita kiasi mtu anayejiita “Daudi Balali” ameanza kuzungumza kupitia mtandao wa Twitter akijaribu kuwaamsha Watanzania kuwa taarifa za kifo chake zilikuwa za uongo na kuwa huko aliko yu mzima salama salimini. Daudi Balali “huyo” alianza kuandika kwenye mtandao huo wa intaneti ambao umekuwa maarufu duniani kwa kuweza kutoa taarifa za watu mbali kwa haraka zaidi na kwa maneno machache zaidi.

Balali alianza kuandika mwezi Disemba tarehe 6 mwaka jana kwa maneno  machache tu akisema kuwa “Its time to go home” yaani “Wakati wa kwenda nyumbani umefika”. Kwa maneno hayo machache mtu huyo ajiitaye Balali alianza pole pole kudokeza kuwa taarifa ambazo serikali ilizitoa kuwa “amefia” Marekani hazikuwa na ukweli wowote na kuwa ilikuwa ni sehemu ya njama za kimataifa za kumnyamazisha kufuatia kuibuliwa kwa wizi mkubwa katika Benki Kuu ya Tanzania wakati yeye alipokuwa Gavana wa Benki Kuu.

Daudi Balali alikuwa ni Gavana wa Benki Kuu baada ya kuletwa nchini na aliyekuwa Rais wa Tanzania Bw. Benjamin Mkapa kuwa Mshauri wa Rais pale Ikulu. Baada ya muda mfupi Ikulu Balali alipewa nafasi ya kusimamia taasisi kubwa kabisa ya fedha nchini ambayo ina wajibu wa kusimamia uchumi wa Tanzania yaani Benki Kuu. Ilikuwa ni chini ya Gavana Balali wizi wa aina mbalimbali ukihusisha magenge ya kimataifa ya mitandao ya kihalifu ambayo yalikuwa yanafanya kazi nchini kwa kushirikiana na wanasiasa, wataalamu na wana usalama mbalimbali.

Katika ya kashfa zote kubwa ambayo ilionekana kutishia usalama wa nchi na utawala ulio madarakani ni ile inayojulikana kama Kashfa ya EPA. Wakati wa Gavana Balali makampuni mbalimbali nchini yaliwasilisha Benki Kuu hati za kujitambulisha kuwa yamepewa haki ya kisheria ya kufuatilia madeni ya makampuni ya nje ambayo yalikuwa yanaidai Benki Kuu ya Tanzania kutokana na sababu mbalimbali za kiuchumi. Makampuni hayo ya Kitanzania yalipatiwa taarifa za ndani ya madeni hayo na watu kutoka ndani ya Benki na yakafanikiwa kukusanya baadhi ya wanasiasa na wafanyabiashara nchini ambao waliunda kwa haraka haraka makampuni feki ya kudai madeni hayo kwa “niaba” ya makampuni ya kigeni.

Katika hali ambayo ilishtua Kampuni ya Kimataifa ya Ukaguzi wa Fedha ya Deloitte and Touche ambayo iligundua kutokupatana kwa taarifa mbalimbali za makampuni hayo. Kampuni hiyo iliandika taarifa yake kwa Gavana kuelezea kutokupatana huko na kushangazwa ni jinsi gani watu wa Benki kuu walishindwa kuona tofauti hizo. Hata hivyo katika hali ya kushangaza kampuni ya Deloitte and Touche iliondolewa kufanya kazi hiyo.

Hata hivyo siri ilikuwa tayari wazi. Makampuni 22 yalijipeleka Benki Kuu na kuwasilisha vielelezo mbalimbali vya ulaghai na watu wa Benki Kuu wakiwa na akili timamu na wenye elimu ya juu kabisa wakawapatia kiasi cha dola milioni 133 kwa urahisi kabisa. Waliochukua fedha hizo wakazibadilisha huku wengine wakizihamisha nchini. Kampuni maarufu kati ya hizo 22 ni kampuni ya Kagoda Agriculture Limited ambayo peke yake ilichotewa zaidi ya dola milioni 40 kutoka Benki Kuu!

Kuibuliwa kwa kashfa hiyo ambako kulipigiwa kelele vikali na viongozi wa upinzani Tanzania kulielekea kutishia watawala ambao walijitahidi kutafuta namba ya kukabiliana kwani ukweli ulikuwa ni mgumu kuukana. Kwamba, kuna fedha zilichotwa Benki Kuu hakukuwa na shaka; kwamba makampuni yaliyochotewa fedha hizo yalikuwa ni feki hakukuwa na shaka; kwamba kulikuwa na njama ya hali ya juu kufanikisha hilo bila kushukiwa na vyombo vya usalama nalo halikuwa na shaka. Serikali ikajikuta iko kwenye matatizo.

Lakini kilichounganisha vitu vyote ilikuwa ni taarifa iliyotolewa na kundi lisilojulikana ambalo kwa mara ya kwanza liliwachorea Watanzania picha ya mtandao wa uhalifu wa kiuchumi (economic criminal ring) ambao unafanya kazi Tanzania. Taarifa hiyo ilionesha kuwa mtandao huo unahusisha wafanyabiashara kadhaa wa Kitanzania pamoja na watendaji wa ngazi za juu serikalini ambapo kinara alikuwa ni Gavana wa Benki Kuu Bw. Daud Balali. Taarifa hizo zilidakwa na wapinzani na Dr. Wilbrod Slaa wakati huo akiwa Mbunge wa Karatu alihoji juu ya taarifa hizo katika Bunge ambapo mwanzoni aliyekuwa Spika Bw. Samwel Sitta alijaribu kupuuzia kuwa ni taarifa za “mtandaoni”.

Hata hivyo, madhara yalikuwa yamekwisha fanyika. Pamoja na juhudi zote za serikali kujaribu kupuuzia na kuonesha kuwa siyo jambo kubwa ilikuwa vigumu kuwashawishi Watanzania kuwa madai ya wapinzani na Watanzania wengine yalikuwa ni ya “kisiasa” tu na ya “kutafuta umaarufu”. Hatimaye, Gavana Balali aliitwa Dodoma ambako alikutana na viongozi mbalimbali. Hiyo ilikuwa ni baada ya kufanya mkutano na waandishi wa habari ambapo alikanusha kabisa kuhusika na wizi huo na kudai kuwa kilichokuwa kinaelekezwa kwake ni njama za “wafanyabiashara” ambao hawakufurahia alivyokuwa anasimamia Benki Kuu.

Alipotoka Dodoma kwa ndege ya Serikali Balali “alitoweka” nchini. Siku chache baadaye taarifa zikatangazwa kuwa amepelekwa Marekani kwa matibabu japo siku ya kuondoka na namna alivyoondoka hakuna ambaye alikuwa tayari. Na huo ndio ulikuwa mwisho wa Balali kuonekana Tanzania. Taarifa zikaanza kutokea kila baada ya siku chache juu ya maendeleo ya “hali” yake huku nchi ya Marekani ikitoa ofa kwa serikali ya Tanzania kuwa kama wanamtaka Balali ingeweza kumsaidia kumleta nchini. Serikali haikuwaomba Marekani kufanya hivyo.

Kama wiki moja hivi kabla ya “kifo” chake taarifa za mpango wa geresha ya kifo zilivuja kutoka vyanzo vya ndani sana ambavyo vilidokeza kuwa Balali alikuwa atangazwe kuwa amekufa kwa “ule ugonjwa” na atazikwa huko huko “Marekani”. Na kweli siku chache baadaye taarifa kuwa Balali amefariki dunia zilitangazwa na kama ilivyokua kwenye mambo mengine taarifa hizo hazikukubaliana. Serikali ya Tanzania ilitangaza kuwa Gav. Balali ambaye alikuwa analipiwa matibabu na serikali alikuwa amefia kwenye “hospitali moja huko Boston” japo taarifa zilizotolewa kwenye “msiba” huko Washington DC zilidai kuwa amefariki katika hospitali ya Chuo Kikuu cha Georgetown ambako alisomea miaka kama arobaini iliyopita.

Katika hali ambayo ilitarajiwa (na kinyume na desturi ya misiba mingi ya Watanzania) mwili wa Balali haukuoneshwa kuagwa na hakuna mtu yeyote wa nje (asiye mwana familia) ambaye amewahi kuonesha aidha Balali akiwa mgonjwa hospitali au mwili wake ukiwa unaagwa. Na kinyume na kawaida nyingi za Watanzania wanaofariki nje ya nchi mwili wa Balali haukurudishwa nchini kwa mazishi. Taarifa nyingine ambazo zimekuja miaka karibu miwili tangu taarifa za kifo cha Balali zitolewe zimedokeza kuwa Balali aliruhusiwa kutoka hospitalini na kwa miezi mitatu alikuwa akiugulia nyumbani. Hizo nazo zilikinzana na taarifa za serikali kuwa Balali alikuwa ameugulia hospitali hadi mauti yalipomkuta.

Hivyo, kuibuka kwa “Balali” kunaelekea kuibua mjadala mwingine kabisa kama kweli alikufa kama ilivyotangazwa au alitoweshwa na kufichwa mahali akiahidi ukimya. Maandishi ya Balali wa mtandao wa “twitter” yanaonesha kuwa kama kweli ndiye Balali wa BoT basi huko aliko amechoshwa. Dalili ya hali ya kutokukubali (defiance) ya Balali wa twitter inatukumbusha jinsi alivyojitokeza hadharani kuzungumza na waandishi wa habari mwishoni  mwa juma la pili la mwezi Julai 2007 akikanusha vikali madai kuwa alihusika na wizi wa EPA.

Baadhi ya watu wanaamini kuwa ilikuwa ni maneno yake yale ya hadharani ambayo yaliwashtua wahusika mbalimbali kuwa Balali hakuwa tayari kubebeshwa zigo la Kagoda na kama wangemuachilia kwa hakika angemwaga ugali, kumwaga mboga, kuvunja masufuria na kuchoma jiko!

Maandishi ya Balali wa twitter yanaonesha kuwa ni mtu ambaye anaamini amedhulumiwa haki yake ya kusema ukweli na kuwa huko aliko anajuta kuondoka Tanzania katika mazingira ya alivyoondoka.  Akiandika siku ile ya kwanza ya Disemba 6, 2011 Balali wa twitter anaandika “I didn’t die, I’m not dead” kwamba “sikufa, niko hai”. Baadaye aliandika “I miss home” na kuwa “the Big 6 and the Architect said I died” akimaanisha kwamba anatamani kurudi nyumbanio na kuwa Vigogo 6 pamoja na “Mtaalamu” ndio waliosema kuwa amekufa. Aliongeza pia kudai kuwa hakukuwa na jinsi yoyote ya yeye kwenda kinyume na weledi wa fani yake na kuisaliti nchi ambayo anaipenda kutoka moyoni.

Hata hivyo akidokeza kwa mbali kile kinachowezekana kuwa ni sababu ya yeye kutokea hadharani sasa Balali wa twitter anasema “they ripped me off” akimaanisha kwamba hao watu waliomsababishia kukubali kuondoka nchini wamemuingiza mjini.  Akiwaita watu hao “wao” anasema wanauwezo wa kuchagua rais, kutafuta fedha na kuzitumia na kutangaza watu kuwa wamekufa.  Balali wa twitter amedai kuwa kama atakufa sasa kabla ya lengo lake kutimia bado siri aliyo nayo itawafikia wananchi. Inasadikiwa kuwa wapo watu wachache sana ambao Balali huyo amewafuata na kuwapa sehemu ya taarifa aliyonayo kwa masharti kuwa wakae nazo na wazitoe tu kama atashindwa kufika nyumbani katika muda aliouweka.

Balali huyo amedai kuwa hao waliomsababishia atoweke nchini waliamini kuwa hana madhara yoyote kwao na kuwa wanajua kwamba yuko hai japo hawajui yuko mahali gani. Katika maandishi yake ametuhumu vyombo vya habari kuwa navyo vinatumika kiufisadi kuanzia ngazi ya chini hadi ngazi ya juu kabisa.

Balali huyo amedai kuwa ameandaa mpango wa kina ambao anaufuata wa kuweza kulipua mambo yote ambayo bado yamewakalia wananchi kama kivuli. Ameahidi kufunua gharama halisi ya Minara Miwili ya Benki Kuu, Jinsi Benki Kuu inavyofanya kazi, EPA, Magavana “halisi” wa Benki Kuu, Mkataba wa Rada na mambo mengine kem kem. “Nina mpango wangu kamili ambao ni lazima niufuate na hivyo sina haja ya kuharakishwa kufanya lolote; nitaamua mwenyewe nifanye nini na vipi” amedai Balali huyo wa twitter na hivyo kufanya wahusika mbalimbali kuanza kuwa na matumbo moto hasa kama itathibitka kuwa ni kweli anayezungumza ni Balali aliyewahi kuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania.

Akionekana kuwa anatekeleza mpango wake Balali huyo wa twitter alianza kuhesabu siku zilizobakia hadi mpango wake huo kutimizwa. Tarehe 9 Disemba (Siku ya Uhuru) alitangaza kuwa zimebakia siku 308 hadi tukio fulani ambalo amelidhamiria litatokea. Haijulikani kama ni siku ambayo yeye mwenyewe atajitokeza hadharani au siku ambayo nyaraka mbalimbali zinazohusiana nay eye zitawekwa hadharani.  Siku 308 tangu Disemba 9, 2011 ni tarehe 12 Oktoba, 2012.

Vyovyote vile ilivyo, wazo kwamba suala la Ballali halikufikia mwisho unaoeleweka linaacha uwezekano mkubwa wa watu wa aina mbalimbali kuweza kujitokeza na kufanya lolote wakijua tundu kubwa lililoachwa wazi na serikali baada ya kuonekana kushindwa kabisa kujua la kufanya juu ya Ballali. Lakini kinachotisha zaidi ni swali lisiloepukika "vipi kama ni kweli huyu ni Ballali"?

Niandikie: [email protected]

77 Comments
    • MIMI niljua kwamba huyu jamaa yupo kwa sababu ilikuwa haingii akilini kwamba mtu kama Balali afe harafu selikari ishindwe hata kutuonyesha picha za mazishi yake?

  • Hii ni noma. Natamani jamaa angejitokeza hata sasa hivi ili umma wa Watanzania waweze kufanya maamuzi magumu. Zaidi sana natamani wale wote watakaotajwa na huyu Balali wa Twitter pindi akijitikeza tuwanyonge kwa mikono yetu wenyewe bila ya hata kutumia kitanzi. Ukweli utajulikana tuu. Mi mwenyewe ni kati ya wale wasioamini juu ya kifo cha Bw. Balal. Lakini hakuna marefu yasiyokuwa na Ncha.

  • Mtu yoyote anaweza kujisajili kwenye hizi web kama Balali,kwa hiyo watanzania wenzangu msibabaike na hizi taarifa si za kweli

    • Ingia Twitter afu m follow jamaa, then utajua je ni kweli ama uongo, maana anayo andika yanaleta maana ati.

  • itakua aibu kubwa sana kuliko ya jamaa waliodanganya umma kuhusu kuupandisha mwenge kileleni!!!!!!!!?

  • hivi umeona wapi mtanzania mwenye asili ya kiafrica akifa huchumwa moto hivi wabongo hamjaliona hili huyu balali naami yuko hai anakula kuku hawaii , aligeuzwa chambo

  • Ndio maana hamna maendeleo kwa kushabikia fikra potofu. Acheni hizo, Balali alikwisha kufa. Wabongo bwana, fitina tupu.

    • WEWEW ACHA UTOTO MPAKA UNAFIKIA UMRI ULIO NAO ULISHAONA WAPI MTU ANAKWENDA MSIBANI KWA KADI?
      AU NA WEWEW NI MMOJA WAO?

    • Yeah..nadhani huyu Ballali wa twitter amechoshwa na mzigo alio twishwa ambao hakika asipo sema basi anahisi hata akifa ki-kweli basi ameondoka na zigo hilo la dhambi za hujuma kubwa kabisa dhidi ya m-Tanzania fukara wa kupindukia, so dawa ya hawa jamaa ni mwaga mambo hadharani, nchi hii hakika kuiondoa kwenye genge la hawa waranguzi, njia pekee ni kufunguka tuu, sema, then waachie kazi wa-Tanzania waamue, hakika sasa wa-Tanzania si wavivu wa kufikiria kama ilivosemekana siku chache zilizo pita, hakika huyu Ballali wa twitter anaweza walau kuuonyesha umma kuwa yeye ni mzalendo, na kwetu atakuwa shujaa wa taifa hili siku za usoni kama akijitokeza……kata hiyo minyororo na ufunguke, na hakika babu yako wa kwanza alizikwa Tz hii, hivo utaendelea kuwa mzalendo popote pale ulipo…wewe funguka tuu,

    • Wewe usiwe kibaraka wa ufisadi, hata kama mwana familia ya kifisadi kaa pembeni kama huna jipya acha kujipendekeza wewe una maendeleo gani acha matusi Balali yupo tutakugombea usilete wehuu hapa alaaa!

      • dah sasa huyo jamaa ane sema kafa atupe ushahidi wa kutosha kama alisha wahi kwenda kwenye mazishi labda, ama ushahidi wowote utakao ridhisha jamii unajua unapo toa habari ambazo hazina uwakika katika jamii yenye watu wa hadhi tofauti unatakiwa kujipanga sanaaa we truesay umekuwa falsesay with no facts

        • ee mwenyezi MUNGU utuhurumie; utuwezeshe tuone anguko kuu la watu wasio na akili ya kufikiria kama ndugu yetuTRUESAY. Huyu na wenzake wa CCM. Nani aliliona kaburi laBALALI?

    • Maendeleo hayawezi kuja wakati tuna watu wenye mawazo finyu kama wewe. Una ushahidi gani kuwa huyo siyo Daudi Balali aliyekuwa BOT. Ushahidi kuwa ni yeye upo tena mwingi. Tunasema hakufa sababu mazishi wala maiti yake haikuonekana na hakuna mtu yeyote aliyeenda kumzika kutoka Tz. wewe kama sio fitna kitu gani kinachokufanya useme kuwa kafa?

  • Mmmm ni vigumu kujua kwa uhakika kama ndio Gavana wa Zamani,lakini TZ lolote lawezekkana.Maelezo yaliotolewa na serikali hayakuridhisha wengi.

  • hivi mtu kama gavana wa benk kuu si cheo kidogo iweje afariki kusiwe hata na kiongozi aliye wakilisha nchi hata makamu wa raisi au waziri mkuu akifa mtu yeyote maarufu viongozi wanawakilisha serekali iweje kwa balali hapa kuna zengwe ila hakuna lenye mwanzo lisilo na mwisho

  • hapa tulichezewa akili zetu kabisa huyu mtu hajafa wala nini yupo tu anatumia pesa zetu maana serikali lazima imgaramie ili mambo yao yaende. Mungu angeshuka dk 1 tu.

  • Balali yupo hajafa kilikuwa ni kiini macho cha serikali ili wasiaibike lakini mungu yupo na chadema wapo dk slaa oyeeeeeeeeeee peopleziiiiiii power

  • habari hii ni ya kweli, Wa tz tusiwe wagumu wa kuamini, tumwombe Mungu atufikishe salama hapo oct 2012

  • Inawezekana jamaa yuko huko misituni america kama yule mzungu wa australia aliweza kuishi chini ya ardhi miaka kibao huku akila watoto wake huku majirani wakijua anaishi peke yake ndo ashindwe belali original

  • possible kuwa huyu mtu yu hai,tumwombe mungu tu siku ya mageuzi na hasira za watanzania yaja.
    mungu ibariki africa,mungu ibariki tanzania.

  • Watanzania tuache bla bla tufanye kazi. tumezidi mno kuchonga hatuko serious! ndio twadai maisha bora, yatakujaje bila ya kufanya kazi? tumekalia uzushi tu! Mungu atusaidie!

  • Kama ni kweli yupo basi kitaeleweka baada ya hizo siku 308 kuisha na itawasaidia wanaharakati kuwa no hoja za kushambulia utawala wetu wa kifisadi

  • Aisee kadri siku zinavyokwenda naziona ISHARA ZA SHARI hivi BALALI,BALALI yeye huyoo auu?
    mungu amlete ili tuujue ulimwengu ulivyo maana kuna mambo mengi sana yamefichwa fichwa tu

    • Imagine kuwa siku hiyo imefika, na siri nyingi zimefichuka na wahusika wamejulikana..NINI KITATOKEA? Jibu ni : “Hakuna la maana”.

      Watanzania tumejengewa roho ya upole, uzubaifu, umbumbumbu.. Sana sana hakuna kitu cha maana kitatokea na hakuna hatua yoyote yenye manufaa itakayochukuliwa zaidi ya kelele nyingi tu na maneno mengi tu yasiokuwa na vitendo vya kutokomeza ujinga huu wa watu wachache ktk jamii uliojaa ktk kila sekta ya serikali ya Tanzania…kuanzia polisi mpaka ofisi kubwa kabisa ya juu zaidi ktk serikali.. Hiyo kesi itasimamiwa na chombo gani ambacho hakiko kwenye system hiyo? Mahakama (you kidding me??), Usalama wa taifa (you kidding me??), bunge la Tz (you kidding me??)… Halafu kuna bwana mmoja hapo juu kasema kuwa the so-called Balali akishaijulisha umma kuhusu hao Balali then watawanyonga kwa mikono mitupu (you kidding me too??) .. Wewe mwananchi mnyonge unaetembea kwa miguu, utamfikiaje huyo aliyeshikilia mabilioni ili umnyonge?? Cha maana mnyonge anachoweza kufanya ni kujitolea kukusanyika na kujitolea kufa either kwa kuuliwa na hao mafisadi au kujiua ili sauti isikike kimataifa kuwa kuna unyanyasaji wa kibinadamu unafanyika ili mje kusaidiwa.. LAKINI NI MTANZANIA YUPI NINAYEMFAHAMU MIMI ANAEWEZA KWENDA MSTARI WA MBELE NA KUONGOZA KUNDI LA WAFIA-JAMII?? Courage hiyo haipo Tanzania, mpaka zama hizo zitakapofika ndipo Tanzania itaweza kutokana na hali hii iliyopo, hali ya watu wachache kabisa kuchota fedha na kuchezea kwa kuzificha nje ya nchi, huku watanzania wakiendelea kutaabika nchi kwao.

    • kiukwel kuna uwezekano mkubwa jamaa yu hai na ni ukwel usiopingika kuwa kuna uwezekano hata baadhi ya viongozi serikalini wanajua sehemu alipo jamaa huyu.Tusubiri tuone.

  • kumjua kama huyu balali au sie ni kazi rahisi ambayo ni lazima serikali iingilie kati, ni Kazi ya Twitter na FBI kutwambia kama ndie, they just have to track him then expose him, hata mimi na wewe tunaweza kuingia twitter mmoja akajifanya Kikwete mwengine Slaa kwa kusudio la kuupotosha umma, Sio kila ukionacho net ukajua ni ukweli vyengine ni uzushi!

    mimi siwezi kukubali moja kwa moja kama yeye ndie au sie ila kama kweli anataka tujue kama yupo hai hivi aliona tabu gani kutengeza video akajirekodi na kuiweka Youtube na akatumia id yake ya twitter kutuonesha link ya Video yake? Lazima tujiulize,,, mi naona ni uzushi tu!

  • haya mambo jamaan hawa wahusika wanajua ukweli ukiangalia mazingira ambayo serikali ilitangazai umma kuwa amefariki ni mazingira ambayo hayaridhishi kwani kwa cheo alichopewa ni lazima mwakilishi wa nchi angeenda kwenye mazishi,suala la kuchoma maiti yake kwani jamaa alikuwa baniani???

    Ukweli utajulikana tu iwe uzushi au ukweli mungu pekee atatufungua macho…..ww na mimi hatuna uhakika tusubirie tu. Je,ww unayeamini kuwa amekufa una uwezo wa kuthibitisha??? Na ww unayesema hajafa una uwezo wa kuthibitisha??? Tumeibiwa kwa muda mrefu ila mungu atasimamia na juhudi zetu zitaleta haki katika jamii yetu

      • Da we umenena Wabongo tunahitaji kutoka Giningi. du yote yanawezekana coz hawa wakuu bwana mmmmhhhhh wanaweza lolote unapotezwa fasta tu ishu kibao ziko pending kazi kulala tu mjengoni hawana jipya we ned to change the whole system ilianza na sisi

  • Mungu Mkubwa, namwombea Balali huyu awe hai mpaka hizo siku zitimie atupatie uwazi wa haya mambo manake mimi binafsi sikuwahi kuamini kama alikufa kweli ila ndo hivyo mi wa chini sina cha kufanya.

    Mungu tuinue waTanzania kwasababu kuna watu wataumbuka na hata kupoteza nafasi zao ati!!

    Kwanini sisi lakini kwanini Tanzania tunaonewa hivi jamaniii

  • kuna abali zimetapakaa kwamba uyo jamaa ‘balali, yuko anjuani. kule majeshi yetu yalipokuwa katika kuleta kile kinachoitwa utawala bora.kuwa yuko katika ngome ya vijana wetu waliosalia ni kweli ?nipeni habali mimi sielewi nachanganyikiwa.

  • watanzania tuache mambo ambayo yanatupotezea muda wetu wa kutafuta maendeleo yetu

  • Balali yuko hai hajafa. Hata viherehere waliojifanya wakipewa nauli watamleta balali kutoka marekari walishabusu ardhi(kuuwawa), hapa nakaa kinywa nilee watoto kwa mchuzi wa kujitizama.

  • Jamani mi naona tusubiri hizo cku 308 then tuone kitakchotokea ila kwa sasa tujiulize hizi nguvu zinazotumika kwenye chaguzi ndogo alafu madaktari, wauguzi na walimu hawana mishahara mizuri tutafika kweli?

  • mimi nakaa pembeni, nikimshukuru mwenyezi MUNGU kwa kunionyesha haya, na sasa namuomba tena aniongezee uhai ili niweze kuona menginge mengi katika hali ya neema katika nchi yetu, ikiwezekana hata ujio wake tena kwa Tanzania

  • watnzania wanapendepa kujua ukweli bt wakiujua huishia kuongea na kulaumu bila kuchukua hatua yoyote kwa kisingizio cha kutovunja amani,kuna haja gani yakuvumilia unyonyaji kwa kisingizio cha amani

  • mungu hamfichi watu wanafiki, nafikiri ni mda wakujua uovu wa viongozi wetu, kw kuficha ukweli juu ya kifo cha BALALI.
    ingekua busara kama angejitokeza kipindi hiki kigumu, cha mawazo mengi juu ya kifo chake.

  • kama Tanzania ina Kingmakers na Pesa ya nchi (walipa kodi)iko mikononi mwa watu na wanajulikana na hakuna Mkuu,wala watendaji wakuu wanachosema na naona kamawabunge wanaogopa kupagusa(kwa mtazamo wangu).Anaweza kuwa yeye lakini atakuwa hatarini sisi wachungaji yatupasa kuomba si kwa ajili yake tu, bali hatima ya Tanzania pia.laiti angepatiana ndugu wa karibu kuusaidia hili utata ungeisha,hata hivyo Mungu Mwema,hakuna marefu………….

  • najiuliza kwa nn anasubiri oktoba? anafanya uchunguzi? kama kweli,, kwa nn asiendelee kukaa kimya basi mpaka hiyo oktoba ifike!! akafie mbali,,, kwa nchi tena marekani??? asiombe hifadhi basi?? asieleze imekuwaje kuwaje?? nae mwizi tuu na mzandiki, laghai na mfitini.. hatumuhitaji maana hana jipya!! si yeye wala waliomtndea hayo wananeemeka,,, tena akirudi nae ahukumiwe na wenzake wote… bora afe sasa kuliko kusubiritutakaposhika dola

  • ni aibu kama jamaa kweli yupo,tumlilie mungu atatuonyesha mambo makubwa na magumu tusio yajua

  • Inaonekana kama akijitokeza hadharani, atasema yote halafu afe (kwa njia yoyote ile hata suicide) siku ya kukumbuka kifo cha Mwalimu Nyerere, OCT 14th, ili iwe siku ya kukumbukwa maana hatutaacha kuadhimisha Nyerere day. May be ndo lengo lake kama ni Balali wa BOT

  • Mwisho wa viongozi wetu utakuwa ni aibu kuu.Mungu tusaidie kila kitu kiwe hadharani

  • NIME JAAA SHAUKU KIASI GANI ONCE THE WHO IS CALLED REAL BALALI EXPOSED NA NDIO ITAKUWA KILIO KWAO WEZI WOTE NA CCM NA HII INAMAANISHA CCM WOTE NI WEZI ZAIDI SANA VIONGOZI WALIOOKO MADARAKANI KUANZIA JK MWENYEWE KATU HATONUSURIKA LAKINI

    LAKINI SEHEMU YA USA IKO WAPI KATIKA HILI
    SEHEMU YA JK IKO WAPI UA NDO HAJUI KAMA DOWANS ALAFU IKIJULIKANA ITAKUWAJE

  • God is able, at the end of the day the truth will be known! for sure i come 2 prove that good leader is born not made! selfishness leaders of these days are the source of all evils in our beautiful country which is exploited by few people!

  • Haya baba kazi bado ipo ngonga izo siku ziishe tuone mambo na jins nchi itakavyosambaratika

  • Kila mwenye akili na uwepo wa Mungu nafsini mwake anatambua wapi nchi hii na watu wake wanaelekea.kila kitu kipo wazi hakuna lilijificha tangu cku wametangaza kuwa ni marehem.hata mie nikifa ninahakika mjumbe wa nyumba kumi ataona jeneza na mahali nimezikwa.

  • ukweli juu ya jambo hili uko wazi, Balali ni mzima na Dunia inajua hivyo,,, ila kwa sababu ya ufisadi kutawala dunia hii ndo maana watanzania tumechezewa akili kwa kiasi hicho…

    Hata hivyo ushahidi ulishaanza kuonyesha wa ukweli huu na muda si mrefu mambo haya yatajidhihirisha kwa watu wote

  • Nafikiri kuna haja ya kufahamu familia ya Balali(mke na watoto) wapo wapi?au Jamaa alikuwa single?
    Wanaweza kutupasha habari japo za juju

  • unajua tanzania kama kweli ili swala kuna watu wa kujitolea kulifanyia uchunguzi inawezekana sanaaaa tena sanaa kitu ambacho me naweza sema ni mwamba hii mitandao ya kijamii ukiamua kumsaka mtu uanampata vizuri sanaa kwa sababu hii mitandao inatuweka open sanaa bila sisi wenyewe kujifahamu ukiamua kumtafuta huyu mtu anapost tweets zake kutokea wapi ukiunganisha na searchengine mengine kama google map na mengine ambayo yanaweza kuwepo namimi mwenyewe nisiyajue tunaweza kuakikisha kuwa huyu ni yeye ama si yeye.

  • Hivi inawezekana kweli ?mbona haiingii akilini,mtu aliyezikwa ,tena ndugu zake wameshuhudia (last respect)halafu leo aanze kututumia jumbe mbalimbali kwenye twita!aaa…sidhani kama yaweza kuwa hivyo.Hebu tujiulize ”kuzimu kuna internet?”Kama kweli ni yeye anatuandikia,basi atakuwa hajafa,lkn je yule aliyelazwa kwenye jeneza alikuwa nani?Du!kidogo hizi habari zinachanganya,hebu na wengine waseme,hayo ni mawazo yangu mimi.

  • kwanzia mwanzo wa mazungumzo sijaona mtu aliye chukua hatua zakupata habari zaid kutoka ktk familia yake au ndugu ,rafik ivi namaneno yetu yote hayo hakuna hatua!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!! tutaonekana wajinga bado tupo gining token huko mi nshatoka nahatua nisha chukua

  • Tobaaaaaa!! zimebakia wiki tatu tu tokea leo ili Balali amwage mambo hadharani. Eeeh Mungu kama ni kweli ebu nijaalie uzima nije kushuhudia huyu jamaa atakuwa na taarifa gani

  • Mwanakijiji hii habari imeandikwa miezi kadhaa iliopita na sasa nimeisoma kwa mara ya kwanza. Zimebaki siku 20 kufikia tarehe 12 October 2012.

    Endelea kufuatilia kujua kama uwezekano wa kufanyika chochote kitu kuhusiana na Balali huyu wa Twitter, Eidha tupate taarifa ya kufanikiwa au kutofanikiwa kwa mtu huyu na ikiwa hajafanikiwa alikumbana na matatizo gani, ama anahitaji nini ili aweze kufanikiwa.

    Naweka siku hii kwenye kumbukumbu zangu ili siku hio niwe makini mtandaoni na kwenye vyombo vya habari vya ndani na nje huko aliko. Kila la Kheri kwa huyo Balali wa Twitter anaedhamiria mema Tanzania na vizazi vyake.

  • Leo ndio siku yenyewe hakuna taarifa yoyote kumhusu huyu mtu anaeitwa balali wa twitter. Kama zilikua stori za uzushi iondoe habari hii kabla ya masaa 48 yajayo. Naona mnawababaisha watanzania kwa kuwapa taarifa za uchochezi siku zote.

  • ijapokuwa muda umepita, but research shows that, balali is alive. I have even my friend who was there USA where barial took place, but could not be able to participate.
    he might be even here in Tz now. in tz every thing is possible

    • THE TRUTH can never be changed by any cost if he is alive or not it will be known.My GOD show Us the way

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *