Sauti za wadau kuhusu nini kifanyike kuzuia Maambukizi ya Virusi vya UKIMWI

Belinda Habibu

Vijana watarajiwa wa kike wenye umri wa miaka 12-15,katika wilaya ya Ushirombo mkoani Geita wanajihusisha na masuala ya ngono.

Sababu ya kiuchumi imetajwa kuwa ndio moja ya chanzo cha suala hili miongoni mwao ili wapate kipato cha kujikimu katika mahitaji mbalimbali ya kila siku kama kununua mafuta,nauli za shule na hata chakula cha nyumbani.

Mwandishi wa habari za jinsi na utawala bora Joas Kaijage kutoka mkoani Kagera alisema hayo wakati wa mahojiano na blog hii jijini Mwanza.
Ameongeza kuwa katika wilaya hii vijana wasichana wa umri huo hulipwa sh. 5000 kwa tendo la ngono kama watataka mwanaume anayejamiana naye avae kondomu na kama laa basi atalipwa sh. 10,000.

“Wengi huchagua kujamiana bila kuvaa kondomu ili walipwe hela nyingi ya sh. 10,000 na hii ni hatari kwa wao kupata maambukizi”alisema Kaijage.

Muaandaaji wa vipindi vya ukimwi kutoka mkoa wa Kilimanjaro Halima Kassimu amesema sababu kuu ya kuwepo kwa maambukizi ya ugonjwa huu kwa vijana ni tamaa ya mali na pesa,na kuanzisha mahusiano na mtu ambaye hadumu naye kwa muda mrefu.

Ameongeza sababu nyingine ni kuwa na wapenzi wengi, kufanya uasherati na ngono kwa rika tofauti matumizi madogo ya kinga,ukeketaji kwa vijana wa kike na jando kwa wanaume wakitumia kifaa kimoja kwa watu wengi.
Akizungumzia madhara kwa wanawake anasema wanaweza kufa na kuacha familia ambayo nayo inakuwa ipo hatari katika kupata maambukizi ya ukimwi kwa kuwa inaachwa ikiwa haina msimamo hasa wa kiuchumi.
“Mfano mama akifariki kwa ugonjwa wa ukimwi,akaacha mabinti watatu,na msimamo wa familia hiyo hauweleweki kinachofuata na wao wanaweza kujiingiza katika biashara ya ngono na wanaweza kuambukizwa.”alisema Halima.
Kwa upande wa vijana madhara wanazoweza kuyapata ni pamoja kwa taifa tunapoteza nguvu kazi,
Akizungumzia nini kifanyike amesema lazima kuondoa mfumo dume wa kuona mwanamke ni kitu cha matumizi,kama kurithi wajane,ulaghai wa mapenzi,kukeketwa, ubakwaji,kurithi wajane na suala la kupima liwe pande zote mbili,si kwa wanawake wawapo wajawazito.
Kwa upande wa vijana waache tamaa za kupata mali haraka bali wajikite na shule kwa waliokuwa masomoni,wafanye kazi kwa bidiii na kuzingatia elimu ya kujikinga na maambukizi ya ukimwi.

Mwanaharakati wa kupambana na ugonjwa wa ukimwi (Kilimanjaro AIDS Control) Exaud Malya alisema vijana hasa wakike wanapata maambukizi ya ugonjwa huu kwa sababu ya tamaa ya kuwa na vitu vya gharama,kama nguo nzuri,kujirusha kumbi za starehe.

“Wale walio vyuoni kwa kuwa maisha yao ni ya kujitegemea wakiishiwa hela huanza kufanya biashara ya ngono”alisema Malya.

Akizungumzia sababu nyingine alisema ni umaskini, hivyo vijana wa kike na wanawake kujiingiza katika biashara ya ngono kwa kumtegemea mwanaume kama ‘source of income’ ili waweze kupata pesa ya kujikimu binafsi na familia zao kuanzia mijini hadi vijijini.

Sababu za kimaumbile, mila na desturi zinazomfanya mwanamke awe chini ya mwanaume mfano anaweza kuolewa na mwanaume asiyemtaka wa kupima kuwa ana hali gani ni kwa sababu tu baba anahitaji mahari.

Sababu nyingine ni ukeketaji matumizi ya kifaa kinatumika zaidi na mtu mmoja,na hata wakati wa kujamiana sehemu ile iliyokatwa inaweza kuchanika na kumfanya apate maambukizi kwa urahisi kwa kuwa virusi vya ukimwi vipo zaidi katika maji maji ya sehemu za siri na damu.

Ameongeza kulikuwa na utafiti uliofanyika mwaka 2006 akiwa na Kilimanjaro Reproductive Health Program, waliokuwa wanafuatilia kwa nini wanandoa mmoja ana ukimwi na mwingine hana.

“Tulichokigundua, wanawake walikuwa wanafanya ngono isiyo salama kama kwa kutotumia kondom, kinyume na maumbile (hapa idadi ni kubwa) ili walipwe juu zaidi na wakitumia kondom basi hulipwa kidogo.”aliongeza mwanaharakati huyo.

Aliendelea kusema utafiti kama huo ulifanyika kwa mikoa ya Moshi na Arusha,walikuta wanawake wanajiuza kwa sh.500 kwa mwanaume mmoja kwa sababu walikuwa wengi sokoni hivyo kujikuta ili waongeze kipato cha sh. 10,000 na zaidi, walilazimika kutembea na wanaume 15 kwa siku.

Alizungumzia sababu ya maambukizi kwa vijana wa kiume kuwa kuanzia miaka 18 na kuendelea anasema wao huona fahari kuwa na mahusiano na vijana wasichana wengi mara leo huyu kesho huyu,na hata wengine kutembea na wanawake umri sawa na mama zao wenye kipato ili waweze kufanya matanuzi.

Aliongeza sababu nyingine kwao ni kutokuwa na woga wa kufanya ngono na kuongezewa mshawasha wa kufanya mapenzi kwa kuangalia picha za ‘pono’ katika ‘internet’.

Madhara ni makubwa nguvu kazi ya taifa inapungua Ukimwi ni janga la taifa ilionyesha umri kati ya 17-60 wanakufa,taifa linakuwa na wagonjwa wengi na gharama kwa serikali kwa kuwa inatumia fedha nyingi kununa dawa za kurefusha maisha,magonjwa nyemelezi hivyo kubaki taifa maskini.
Madhara mengine,ni ongezeka la watoto yatima,watoto wa mitaani na wanaoishi mazingira magumu.

Akizungumzia nini kifanyike alisema elimu ya ujasiliamali itolewe kwa wanawake na vijana ili wajitegemee badala yakutegemea ngono kuwa kimbilio la kujikimu kimaisha.

Ameongeza elimu ya ukimwi iendelee kutolewa kwani wengi wanaona ni kawaida,kwa upande wa wanaotumia dawa za kurefusha maisha watumie kwa usahihi na wasiambukize wengine tutaweza kupunguza ongezeko la idadi ya waathirika.

Kwa upande wake kijana anayejishughulisha na ‘ubeshi’(kuvamia mgodi na kuchota mchanga kutafuta almasi Mwadui, Frank Mpulule wa kijiji cha Mwadui Lohumbo anasema sababu kuu ya maambukizi kwa vijana kama yeye hasa wasichana, ni kutojua jinsi ya kujikinga kwa kuwa hakuna elimu ya aina yoyote inayotolewa kwao.

Aliongeza kingine ni maisha magumu ya kijijini kwao hakuna mzunguko wa hela huwezi fanya chochote hivyo wanawake na wasichana hutembea na huyu na yule tena hawataki utumie kondom.

“Kijiji hiki ni miongoni mwa vijiji vinane vinavyozunguka mgodi wa almasi wa Williamson Diamond,hivyo wanakuja watu wengi hapa hujui huyu katokea wapi na ni mzima ama laa” alisema Frank.

Mwandishi wa habari za afya ya uzazi Mariam Mngumbaru alisema sababu ya maambukizi kwa vijana zipo za aina nyingi kwanza ya kiuchumi, umaskini na kukosa malezi bora kutoka kwa wazazi.

“Nikiwa nafanya kazi yangu katika kijiji cha Kiegei Nachingwea,wasichana wadogo wa kike wa darasa la nne(shule imehifadhiwa),walikuwa wanatembea na vijana,baba zao kwa umri,na hata wa rika zao ili wapate kipato cha kusaidia familia”alisema Mariam.

Aliongeza eneo hili kuna machimbo,elimu ya matumizi ya kondom haipo kabisa kwa kuwa wasichana hawa hawafahamu jinsi zinavyotumika.
Alisema alichokiona pia ni malezi mabovu ya wazazi, hawawajibiki katika nafasi zao za kuhakikisha wanaleta pato la familia na mabinti kuonekana walishaji na hawaulizwi umepata wapi.

Edward Haule ni mwandishi wa habari kutoka mkoa wa Iringa, alisema sababu ya maambukizi kwa vijana na wanawake hazitofautiani sana zipo za kiuchumi,fahari na uwelewa mdogo wa elimu ya maambukizi ya virusi vya UKIMWI.

Alisema wanawake wengi hufanya ngono kama kitega uchumi kutokana na familia nyingi kuwa duni kwa kipato,na kwa wakati mwingine kuwa mzazi mmoja.

Ameongeza mara nyingi wanaume wenye hela huweka dau kubwa kama hutaki kutumia kondom na dau dogo ikitumika,kutokana na hali ya kiuchumi bila kufikiria njaa ya mbali,hujitumbukiza katika mtego wa dau kubwa.

Aliongeza kwa upande wa vijana,huona fahari kutembea na wasichana wengi bila kujua msichana huyu ana wapenzi wangapi,na wapo wengine wanaodiriki kuchukua akina mama poa(rika hata za mama zao) kwa aajili ya kulelewa bila kufahamu mama huyo anamtandao kiasi gani.

Akichambua juu ya sababu za kuwepo kwa maambukizi ya virusi vya ukimwi, mkuu wa wilaya ya Kasulu Zainab Kwikwega amebainisha kuwa, tabia ya vijana kufanya ngono zisizo salama kabla na baada ya kuoa au kuoelewa ni moja ya vyanzo vikubwa vya kuendelea kuwepo kwa UKIMWI hapa nchini.

2 Comments
  • tuna safari ndefu kuundoa ugonjwa huu hatari wa ukimwi,  kinachotakiwa ni maamuzi na utashi binafsi.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *