UPUNGUFU WA DAWA HOSPITALI YA WILAYA YA KISARAWE NI MWIBA KWA WAKAZI WAKE.

Belinda Habibu

Na: Belinda Habibu

“Kama ningalijua sitapata dawa bora ningeenda tu duka la dawa nikanunue mwenyewe nimeze tu,kuliko kwenda katika hospitali hii halafu hupatiwi tiba halisi”
Hayo ni maneno ya fundi selemala , Noel Daniel Udulele wa kijiji cha Kisarawe na ameongeza hata ukiumwa nini utaambiwa na daktari kanunue dawa .
“Unajua ndugu mwandishi hata panadol unaambiwa ukanunue,panakatisha tamaa.”Alisema fundi huyo.
Aliongeza ni bora kama una hela ukaenda hospitali za binafsi ukajua moja kuliko tunachokipata hapo hospitali ya serikalini.
Mwenyekiti wa kitongoji cha Sanze, Aloyce Mayombo, anasema tuliwahi kuchagua kamati za afya sijui zinafanya nini maana tatizo la kutokuwepo kwa dawa wananchi wanalilalamikia.
Ameongeza ni kweli ukiumwa mfano malaria utaambiwa tu ukanunue dawa nje ya hospitali hiyo katika maduka ya dawa.
Sera ya afya ya mwaka 2007,inasema watoto chini ya miaka mitano,wazee na wasiojiweza watatibiwa bure,ila changamoto ni upungufu wa dawa,vifaa tiba na hata miundo mbinu wakati mwingine haifai.
Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Kisarawe, Yona Maki alisema asilimia 73 ya wanaotibiwa katika hospitali hii wanatoka mkoa wa Dar es salaam,na asilimia 27 wanatoka wilaya hii.
“Ongezeko hili la watu ni kiashiria tosha kuwa matibabu yanayotolewa hospitalini hapa ni mazuri”alisema mkurugenzi huyo.
Mganga mkuu wa hospitali hiyo Mwendo Msengi alisema ni kweli dawa hakuna kama wanavyosema wananchi,tumeelemewa.
Bajeti tunayotakiwa kupewa kutoka serikalini ni shilingi milioni 40,ila mpaka sasa tumepewa milioni 28 tu (July 2012-mwezi march 2013),kwa ajili ya kutibu watu wa kisarawe,na kama tukinunua dawa wiki mbili tu zimekwisha.
“Pamoja na kuhimiza uchangiaji wa huduma za afya,bado kuna changamoto ya makundi ya msamaha kama wazee,watoto,wajawazito na wenye ugonjwa wa kifua kikuu,wanaotakiwa wapate matibabu bure”aliongeza.
Mganga mkuu huyo ameongeza, asilimia 73 ya wakazi wa jiji la Dar es salaam wanatibiwa hapa na bajeti inatoka kwa wakazi wa Kisarawe ambao ni asilimia 27 iliyobaki.Wananchi hufika hapa kwa sababu ya ukaribu,na hatusemi wasije ila kuwe na ongezeko la fungu la kukidhi kuwahudumia wote.
Kutokana na ufinyu wa bajeti,mimi (mganga mkuu),naangalia na wenzangu kipi ni kipaombele tunachoweza kununua kwa hela tuliyonayo.
“Kwetu sisi kipaombele ni dawa za mama wajawazito (wakati wa kujifungua) na wale wanaopata ajali mbalimbali, dripu, dawa za usingizi,antibiotics,nyuzi”,alisema mganga mkuu huyo.
Taarifa inayohusu ombi la kuongezewa bajeti kwa hospitali hiyo, iliyotumwa wizara ya afya na ustawi wa jamii, ,iliyopatikana kwa mganga mkuu wa wilaya inayoonyesha ni wagonjwa 118,411 ,ndio walengwa (wakazi wa Kisarawe),na wengine 80,677 wanatoka mkoa wa Dar es salaam na kutibiwa hapo.
Akizungumzia zaidi upungufu wa dawa, mganga Msengi amesema wakati mwingine tunaweza kupeleka maombi MSD,ukakuta dawa tunazoomba hazipo inabidi kusubiri na huku wagonjwa hawakauki,ndipo hapo utasikia dawa hakuna hospitalini.
Alisema kinachotakiwa kifanyike ni kuwa na uwiano kati ya bajeti na idadi ya watu wanaohudumiwa itapunguza manung’uniko,na nawasihi wananchi kujiunga katika mifuko ya bima ya afya, tatizo hili litapungua,wenzetu walio katika utaratibu huu wamefanikiwa.
Ameongeza, ukimwambia mgonjwa akanunue panadol,dawa mseto za malaria nakadhalika katika maduka ya dawa atapata, kuliko nyuzi za kushonea,dawa ya ganzi (hawezi kuipata), hivyo wananchi wajue tumeelemewa ila tunadhamira nzuri.
Alisema mwaka jana (2012),waganga watano waliacha kazi hapa lakini sababu kuu ikiwa ni kukosa vifaa tiba vya kutosha na kujikuta hawafanyi kazi waliyoisomea na wakati mwingine unaona mgonjwa anakufa, kwa kukosa dawa,ama kifaa tiba fulani huna na kama vingekuwepo angepona.
Uchunguzi uliofanyika katika zahanati,vituo vya afya katika baadhi ya mikoa hapa nchini unaonyesha hali ya hospitali hii na hivyo vinafanana.
Baadhi ya wakazi wa Mererani mwaka jana (2012),nilipozungumza nao,walisema wanalalamikia kituo chao cha afya kukosa dawa, wakati huu unaweza kuzipata na si zote ,wakati mwingine huwezi kuzipata,zahanati ya Mwadui Lohumbo, wananchi wanaotibiwa hapo wanakiri hali kama hiyo,na wale wa kijiji cha Idukilo pia wanalalamikia ukosefu wa dawa.
Pia katika zahanati ya Maganzo,Magalata wilaya ya Kishapu ,Kiegei(Nachingwea), Ifinga (Songea)hali ya ukosefu wa dawa kwa wanaotibiwa hapo ni sawa kama ilivyo Kisarawe.

XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *