Vijana wajawazito wasimulia jinsi wanavyoishi na maambukizi ya virusi vya Ukimwi

Frank Leonard

ASELA Mahanga (18) na Happy Mdalingwa (19), ni wakazi wa kijiji cha Ifunda Kibaoni wilayani Iringa, mkoani Iringa.

Wakati Februari mwaka huu, Asela alikuwa na ujauzito wa miezi minne, Happy  alikuwa na ujauzito wa miezi saba.

Wawili hawa wana hadithi za kweli zinazofanana; kwa maelezo yao wote wana maambukizi ya virusi vya Ukimwi (VVU) na waliamua kuvunja ukimya baada ya kupima.

Walipima kupitia utaratibu wa lazima unaotaka wajawazito pamoja na wenzawao, kushauriwa na kisha kupima ili kama wana maambukizi waanze matibabu yatakayoboresha afya zao na kumuepusha mtoto na maambukizi.

Asela na Happy walisema kwa nyakati tofauti kwamba hawawezi kuzaa tena; wanamuomba Mungu awasaidie wajifungue salama mimba walizonazo.

Katika maelezo yake Asela anasema ana elimu ya darasa la saba aliyopata katika Shule ya Msingi Kibaoni na Happy ana elimu hiyo hiyo aliyopata katika shule hiyo pia.

Asela alimaliza mwaka 2010; baada ya hapo alijiunga na shule ya ufundi Ifunda, kozi iliyomchukuwa mwaka mmoja lakini Happy hakubahatika kuendelea na masomo baada ya hapo.

Asela

Asela

Wakati Asela alianza kufanya ngono mwaka 2011 na mmoja wa vijana wa kijijini hapo, Happy alianza ngono mwaka 2007 akiwa darasa la nne; alipata mimba mwaka 2012 baada ya kufanya ngono na kijana ambaye hakumtaja jina akiwa jijini Dar es Salaam.

Happy alikwenda Dar es Salaam kufanya kazi ya utumishi wa ndani kwa mshahara wa Sh 15,000 kwa mwezi na kurubuniwa na kijana huyo.

Julai mwaka jana Asela alikwenda kuishi na bibi yake katika kijiji cha Nyololo, wilayani Mufindi mkoani Iringa, akiwa huko akakutana na kijana (hakumtaja jina) aliyempa mimba.

“Ilikuwa Oktoba mwaka jana nilipogundua siku kadhaa zimepita bila kuona siku zangu. Januari mwaka huu, mama yangu alinitaka nirudi nyumbani,” anasema.

Baada ya kurudi kijijini kwake Ifunda Kibaoni, alipelekwa katika Zahanati ya Ifunda na baada ya kufanyiwa vipimo ilithibitika ana mimba pamoja na maambukizi ya VVU.

Anasema maambukizi ya VVU hayampi hofu tena baada ya kupewa ushauri kwamba hali hiyo sio mwisho wa maisha yake.

“Mwanaume aliyenipa mimba kaenda Moshi, kwahiyo huduma zote napewa na mama kwasababu sina kazi,” anasema.

Kama ilivyo kwa Happy, Asela hajui kama huduma kwa mjamzito zinatakiwa kutolewa bure kama sera ya afya ya mwaka 2007 inavyoelekeza.

“Zaidi ya dawa, hakuna huduma nyingine nayopewa hospitalini, nasikia pia kuna mashirika yanasaidia lakini mimi binafsi sijawahi kufikiwa na msaada wowote,” anasema.

Anasema akijifungua salama, huyo atakuwa mtoto wake pekee na kwamba hatakubali ushauri utakaomtaka azae tena.

Kwa upande wake, Happy anasema alipotakiwa kurudi kijijini kwao Ifunda kwa ajili ya ujenzi wa makaburi Juni mwaka jana, hakujua kama ana maambukizi ya VVU.

IMG_3988

Happy

“Miezi miwili baadaye bibi alinipeleka hospitalini; nilikuwa natapika na nashindwa kula chakula kwa kiwango nilichozoea,” Happy aliyefiwa na mama yake mzazi mwaka 2007, anasema.

Anasema baada ya kupima katika Zahanati ya Ifunda aligundulika kuwa na maambukizi ya VVU na akashauriwa aende Hospitali ya Mkoa wa Iringa ambako aliingizwa katika utaratibu wa kupata dawa.

“Kila mwezi natakiwa kwenda mara moja, huko napewa dawa kwa ajili yangu na za kumlinda mtoto,” anasema na kutaja aina moja tu ya dawa anayoifahamu kwa jina kuwa ni Septrini.

Anasema kwa kuwa hana mawasiliano na kijana aliyempa mimba hiyo, bibi yake ndiye anayebeba mzigo wa kumuhudumia kwa mahitaji yake mbalimbali.

Mahitaji hayo ni pamoja nauli ya kufuata huduma katika Hospitali ya Mkoa wa Iringa ambayo ni Sh 3,000 kila mwezi, chakula na mavazi.

“Akiwa hana hela, bibi, hulazimika kukopa ili nipate huduma; fedha anazokopa huwa tunazirudisha kwa kwa kufanya kazi ya vibarua katika mashamba ya watu,” anasema.

Anasema alifanya ngono akiwa na umri mdogo kwa ushawishi wa mama yake mdogo aliyemepeleka kwa mmoja wa vijana wa kijijini hapo na kumlazimisha alale naye.

“Nilikuwa na miaka 14 tu, mama yangu mdogo alinipeleka nyumbani kwa kijana huyo; ilikuwa saa mbili usiku, alinilazimisha nilale hapo,” anasema.

Anasema bibi yake hakujua kama kalala nje ya nyumbani na alipomsimulia ndipo mama yake huyo mdogo alipotokomea na mpaka leo hajulikani alipo.

Malengo ya Maendeleo ya Millenia kuhusu mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi ifikapo mwaka 2015 yanapania kuhakikisha kwamba maambukizi ya ugonjwa huu yanapungua maradufu. Hadi sasa kuna dalili za mafanikio kutokana na jitihada zinazofanywa na wadau mbali mbali katika mapambano dhidi ya Ukimwi.

Takwimu za Umoja wa Matifa zinaonesha kwamba, katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, kumekuwepo na ongezeko kubwa la udhibiti na huduma kwa wagonjwa wa Ukimwi sehemu mbali mbali za dunia, mafanikio ambayo yamewezesha walau kurefusha maisha ya wagonjwa wa Ukimwi.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon, katika ujumbe wake kwa maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani inayoadhimishwa Desemba Mosi ya kila mwaka kwamba, kuna haja ya kuendeleza juhudi za kudhibiti maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto sanjari na kuwawezesha wajawazito kupata dawa za kurefusha maisha.

Ki- Moon anazitaka nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa kuondoa tabia ya unyanyapaa na ananukuliwa na vyombo mbalimbali vya habari akisema zipo sheria na sera zinazojikita katika hofu na mashaka, zisizo zingatia ukweli wa kisayansi na kusababisha ongezeko la maambukizi ya VVU.

Anasema ipo haja jamii ikaendelea kupata habari za uhakika kuhusu Ukimwi, kupima na kupata matibabu ya magonjwa nyemelezi kama sehemu ya utekelezaji wa haki ya msingi ya tiba kama sehemu ya mchakato wa mapambano dhidi ya Ukimwi.

“Kila mtu akitekeleza wajibu na dhamana yake, kuna uwezekano mkubwa kwa Jumuiya ya Kimataifa kuwa na kizazi ambacho hakina virusi vya Ukimwi ifikapo mwaka 2015. Kila mdau ajifunge kibwebwe kuhakikisha kuwa anaendeleza mafanikio yaliyokwisha kupatikana hadi sasa,” anasema.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *