Wajawazito zaidi ya 200 wapita salama mikononi mwa Nyagawa!

Frank Leonard

MAIMUNA Nyagawa (59), maarufu kwa jina la Mama Zamda ni Mkunga wa jadi anayeishi katika kijiji cha Mdandu, wilayani Wangingombe mkoani Njombe; kazi yake ni kuwasaidia wajawazito kujifungua.

Katika kijiji hicho ndipo yalipokuwepo Makao Makuu ya Wilaya ya Njombe, wakati huo wa mkoloni ikijulikana kwa jina la Nyamuyuya.

Makao Makuu ya Wilaya mpya ya Wanging’ombe yamewekwa kwa muda katika kijiji hiki kilichopo kilomita 30 kutoka Njombe mjini.

Kutoka katika ofisi ya muda ya Mkuu wa Wilaya hii hadi kwa mkunga huyo wa jadi ni mwendo wa takribani kilomita moja. Nyumba yake iko kandokando ya barabara kuu iendayo Njombe.

“Nilianza kazi hii mwaka 1974 kwa kutumia uzoefu nilioupata kutokana na kutembelea wanawake wajawazito wakati wakijifungua katika zahanati ya kijiji,” anasema na kuongeza kwamba kazi hiyo huifanya nyumbani kwake na katika zahanati hiyo.

nyagawa

PICHA: Mkunga wa Jadi Maimuna Nyagawa akiwa na mtoto ambaye mama yake alizaa kutokana na huduma yake

Alianza kuizoea kazi hiyo na jina lake likaanza kukua siku hadi siku kutokana na kuipenda na kuifanya ipasavyo.

Nyagawa anasema mwaka 1984, yeye pamoja na wakunga wengine kutoka katika vitongoji sita vya kijiji hicho, walipewa mafunzo ya njia bora za kuwahudumia wanawake wajawazito.

Pamoja na mafunzo, walipewa vifaa vya kazi ikiwemo begi maalumu ya kuhifadhiwa dawa na vifaa muhimu vya kujifungulia, mzani na taulo.

“Ujuzi uliongezeka na nikawa naachiwa funguo za zahanati pindi muuguzi katika kituo chetu anapokuwa safari au likizo ili wajawazito wanaofika wasikose huduma,” anasema.

Hata hivyo anasema katika kuweka mazingira ya tahadhari, kazi ya kupokea wajawazito na kuwahudumia katika zahanati hiyo alikuwa akiifanya kwa kumshirikisha Mganga Mstaafu anayeishi kijijini hapo, Julius Ngakonda.

Tangu wakati huo mpaka sasa, Mama Zamda anasema amewawezesha wajawazito zaidi ya 200 wakiwemo watoto wake kujifungua salama.

“Katika kipindi chote hicho hakuna mzazi au mtoto aliyefariki kwa kupitia kazi ya mikono yangu, lakini mnafahamu jinsi wanavyopoteza maisha mikononi mwa wauguzi katika vituo vya kutolea huduma,” anasema.

Kwa jinsi anavyoipenda kazi hiyo, anasema anacho kitabu ambacho amekuwa akikitumia kuhifadhi kumbukumbu za wajawazito wote anaowahudumia.

Anasema huduma hiyo amekuwa akiitoa bila malipo yoyote japokuwa wapo baadhi yao wamekuwa wakimpa fedha kidogo kama shukrani kwa kazi yake.

Pamoja na kuwahudumia bure, wanawake hao wamekuwa wakilazimika kununua vifaa vya kujifungulia wakati wakipata huduma yake. Vifaa hivyo ni pamoja na mpira wa kujifungulia, beseni, taulo, nguo na mafuta ya mtoto.

vifaa

PICHA: Maimuna Nyagawa akionesha baadhi ya vifaa anavyotumia kufanyia kazi ya ukunga

Kati ya mwaka 2009 na 2012, Janeth Mtavangu (26), alijifungua watoto wawili kwa msaada wa Mama Zamda. Alifika katika kituo cha huduma kijijini hapo na kukuta hakuna muhudumu. Ndipo alipoitwa Nyagawa na kutoa msaada wake wakati akijifungua.

 “Alinizalisha vizuri watoto wangu wote wawili. Watoto wanaendela vizuri. Vitu vyote nilivyotakiwa kununua, nilinunua na vilitumika kama ilivyokusudiwa,” anasema.

Katika maeneo mengi hapa nchini, huduma ya wakunga wa jadi inatolewa bure, wanawake wajawazito wanaipata bila kulipia, hiyo inaifanya huduma iwe ya kuvutia. 

Hata hivyo anasema mpango wa serikali wa kujenga zahanati katika kila kijiji umesaidia kupunguza ukubwa wa matatizo yanayowasibu wanawake wajawazito kabla, wakati na baada ya kujifungua.

“Maendeleo hayo yamefanya mwaka juzi serikali ituzuie wakunga wa jadi kuzalisha, hata hivyo zoezi hilo limekuwa gumu kwani wajawazito wengi wanakuja na kutuomba tufanye kazi hii” anasema.

mteja

PICHA: Maimuna Nyagawa akiwa na mjamzito anayesubiri kujifungua

Kaimu Mganga Mkuu wa Halmashauri ya wilaya ya Njombe, Dk Conrad Ugonile anasema kwa kipindi kirefu wakunga wa jadi wamekuwa tegemeo katika afya ya uzazi.

Anasema majukumu yao yanaanza kupunguzwa kwa kuzingatia miongozo ya serikali inayowazuia kuzalisha pamoja na kwamba wametambuliwa na baadhi yao kupewa mafunzo.

“Wanachotakiwa kufanya ni kuwasindikiza wanawake wajawazito wanaokwenda kwao kwenye vituo vya kutolea huduma,” anasema.

Dk Ugonile anasema uamuzi huo umezingatia ongezeko la vituo vya kutolea huduma ambalo limepunguza wanawake kuzaa wakiwa majumbani.

Hata hivyo taarifa kutoka kwa watoa huduma za afya wa vijiji zinaonesha kwamba bado kuna wajawazito wanaoendelea kupata huduma kwa wakunga wa jadi kwasababu mbalimbali ikiwemo ya vijiji vyao kutokuwa na vituo vya huduma au wakunga wenye ujuzi.

Taarifa ya Dk Ugonile inaonesha kwamba vijiji 50 kati ya vijiji 145 vya halmashauri ya wilaya ya Njombe na wanging’ombe havina vituo vya kutolea huduma.

Hali hiyo imeifanya Tanzania kuwa moja kati ya nchi zenye kasi ndogo ya kufikia malengo ya ya Maendeleo ya Millennia (MDGs), lengo namba tano la kupunguza vifo vya wanawake wajawazito.

Kwa mujibu wa Makamu wa Rais, Dk Mohamed Gharib Bilal idadi ya vifo vitokanavyo na uzazi nchini, vimepungua kwa asilimia 50 ukilinganisha na mwaka 2009 ambapo takwimu zinaonesha wajawazito 500 walipoteza maisha ambapo  mwaka 2010, vifo hivyo vilipungua na kufikia 250.

Akifungua Mkutano wa Afya ya Mama, mjini Arusha mapema mwaka huu, Makamu wa Rais, Dkt. Mohamed Gharib Bilal anasema lengo ni kupunguza vifo hivyo na kufikia 193 ifikapo mwaka 2015.

Anasema Serikali itajitahidi kuhakikisha lengo hilo linafikiwa ili kuzuia matatizo mbalimbali yanayochangia vifo vya wanawake wajwazito wakati wa kujifungua.

Taarifa ya Shirika la Watoto Duniani (UNICEF) inaeleza kwamba wajawazito wanakufa kutokana na matatizo mbalimbali yanayojitokeza kabla, wakati na baada ya kujifungua. 

Sehemu ya vifo hivyo haviripotiwi kwasababu wanawake wa vijijini wanaendelea kujifungulia majumbani kwa msaada wa ndugu au wakunga wa jadi.

Zipo dalili mbalimbali za hatari wanazokuwa nazo wanawake wajawaito zinazosababisha vifo kwa baadhi yao.

Dalili hizo ni pamoja na kutokwa na damu ukeni, homa kali, kichwa kuuma sana, kutokuona vizuri, na maumivu makali chini ya tumbo. Dalili hizi zote zinaweza kutambuliwa na mtoa huduma aliyepata mafunzo.

Nyagawa anakubali kwamba, ingawa hajakutana na changamoto kubwa katika utoaji wake huduma, hajawezeshwa kikamilifu kuzijua dalili hizo na kumsaidia mwanamke kukabiliana nazo.

“Wakati mwingine, ninapoitwa katika mazingira ya dharula nimekuwa nikitoa huduma bila kuchukua tahadhari. Na jambo lingine ni kwamba sikuwa nikiuliza kama mama mjamzito ninayemuhudumia ana maambukizi ya virusi vya UKIMWI. Wakati mwingine ni ndugu zangu ninaowahudumia, nikilenga kuwasaidia. Lakini tumefundishwa kwamba watoto wanaweza kupata maambukizi ya VVU wakati wa kujifungua,” anasema.

1 Comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *