Wananchi wamwitaji Wasira kuokoa wajawazito

Gordon Kalulunga

BAADHI ya wananchi wa kijiji cha Kambubu kata ya Nyamang’uta wilaya ya Bunda mkoani Mara wamemuomba waziri wa nchi uratibu wa sera na Bunge Stephen Wasira kuokoa wajawazito katika kijiji cha Kambubu kutokana na kukosa imani na kituo cha afya cha Ikizu maarufu kama Nyamuswa.

Wananchi hao waliwaambia waandishi wa habari waliotembelea katika kijiji hicho kuwa katika kituo cha afya cha Ikizu kumekuwa na manyanyaso makubwa kwa wajawazito huku wakitozwa gharama kubwa za kujifungua.

Kijana Samson James alisema kuwa wanalazimika kwenda katika kituo hicho cha afya kwa ajili ya kupata vipimo tu.

‘’Tunaenda Nyamuswa kwa ajili ya kupata vipimo na dawa huwa tunanunua maduma ya dawa na endapo katika maduka ya dawa kungekuwa na vipimo tusingethubutu kwenda huko’’ alisema Samsoni.

Mwenyekiti wa kitongoji cha Kambubu Warioba Kiharata alisema kuwa ili kupata huduma bora za afya katika kituo cha afya cha Ikizu hasa kwa wajawazito na watoto chini ya miaka mitano kama huna fedha basi ni lazima utambike.

‘’Huduma za afya ni shida na pale Nyamuswa ni za kutambikia, maana ukiwaambia kuwa wakusaidie mkeo anaumwa wanakuuliza kuwa sasa wao wafanyeje!’’ alisema Kiharata.

Alisema kuwa kutokana na hali hiyo, wananchi wamehamasishana kujenga zahanati ya kijiji chao na tayari wamekusanya mchanga na mawe na kwamba hata Mbunge wao Stephen Wasira anayo taarifa hiyo lakini bado hawajaruhusiwa kujenga kwa miaka zaidi ya mitatu sasa.

‘’Wakunga wa jadi wanahitajika sana kuliko huduma za kisasa kwa akina mama, kwa sasa katika kijiji chetu tunasubiri kibali cha kujenga zahanati ambapo wanaotukwamisha ni serikali hawataki kutupa ramani ya kujenga zahanati yetu’’ alisema Mwenyekiti huyo.

Agnes Baraka alisema wajawazito wanaopata huduma bora hospitalini ni wale wenye uwezo wa kifedha na ndiyo maana ambao hawana uwezo huo wanaona ni bora kujifungulia nyumbani au kwa wakunga wa jadi.

‘’Kama miba haiuwa na matatizo unaweza kutozwa Sh.7,500 baada ya kujifungua, mtoto akiumwa mapokezi ni Sh3,000, daftari 300 hapo bado gharama za vipimo na wenye bima ya afya ya jamii(CHF) wanapimwa bure lakini dawa wananunua.

Naye Anna Japhet(35) alisema kuwa wakunga wa jadi wanatoa huduma bure na wale wanaotoza fedha ni Sh. 3,000 tofauti na hospitalini ambako mjamzito analazimika kununua karatasi, gaharama za kitanda, na mafuta ya taa 1,000.

Diwani wa kata hiyo ambaye ni rafiki mkubwa wa Waziri Wasira Kelemba Jonathan Ilubi alikiri kupokea baadhi ya malalamiko ya wananchi wa kata yake lakini alisema kuwa hana mamlaka kutokana na kituo hicho cha afya kuwa nje ya kata yake.

Kuhusu ujenzi wa zahanati katika Kijiji hicho alikiri kuwa anajua nguvu kubwa walyoitumia wananchi lakini hawapati ushirikiano kutoka serikalini licha ya yeye pia kupigania ujenzi wa zahanati hiyo.

‘’Wananchi wamejitolea kwa kiasi kikubwa lakini hakuna utekelezaji kutoka serikalini na Mbunge Wasira anakwamishwa maana alishatoa Shilingi Mil.2 lakini mahitaji kamili ya ujenzi wa zahanati ni Mil.60’’ alisema Diwani Ilubi.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *