Wodi za watoto, wanawake na wanaume tatizo Butiama

Gordon Kalulunga

UKOSEFU wa miundombinu ya kutosha zikiwemo wodi za watoto, wanawake na wanaume katika hospitali ya Butiama mkoani Mara ni kieelezo tosha kuwa lengo la milenia la kupunguza vifo vya wajawazito na watoto chini ya miala mitano kufikia vifo 85 kati ya vizazi hai 100,000 Tanzania haitatekelezeka.

Kaimu mganga mfawidhi wa hospitali hiyo Dr. Joseph Musagafa aliwaambia waandishi wa habari wa masuala ya afya walipotembelea hospitalini hapo kuwa kwa sasa hospitali yake ina upungufu nyumba za watumishi, mawodi ya watoto, wanawake na wanaume.

‘’Nyumba za watumishi tunazo 14 wakati mahitaji ni 20, mawodi hayatoshi ambapo wodi moja ya wanawake, watoto na wanaume ni sawa na chumba kimoja cha mgonjwa staff na vyoo vipo vine wakati mahitaji ni vyoo sita’’ anasema Dr. Musagafa.

Akielezea uhaba wa miundombinu katika hospitali hiyo ya wilaya, alisema kuwa wodi hospitali hiyo ina wodi moja ya wanaume yenye vitanda kumi tu, wodi mbili ya wanawake na wodi mbili za watoto zenye vitanda kumi kila moja ambapo chumba cha wauguzi kinatumika kama chumba cha wagonjwa mahututi.

Alisema anaimba serikali kufika katika hospitali hiyo na kujionea hali halisi ilivyo na kwamba mawodi hayo yakipanuliwa mahitaji sahihi kwa upande wa vitanda vinahitajika 20 kwa kila wodi na visibanane kama ilivyo hivi sasa na kuwe na ukubwa mzuri ya vyumba ili kutenganisha wagonjwa badala ya kuchanganywa kama ilivyo hivi sasa.

‘’Hatuna miundombinu mizuri ya maji na tunategemea maji ya mvua na maji ya kupampu yaliyoelekezwa kwenda nyumbani kwa Mwalimu Nyerere’’ alisema Dr. Musagafa.

Kwa upande wa watumishi katika hospitali hiyo kuna watumishi 90 ambapo madaktari ni wanne wakati angalau wangukuwa madaktari nane na kati yao hao wanne mmoja ni mtawala na mwingine ni anashughulikia masuala ya VVU katika wilaya nzima.

Matabibu wapo 17 na wengine wanaobaki ni wauguzi na watumishi wengine wakiwemo walinzi.

Dr. Musagafa anataja sababu zinazosababisha vifo kwa wajawazito na watoto chini ya miaka mitano katika wilaya hiyo kuwa ni pamoja na upungufu wa damu, kuchelewa kufika hospitalini, kununua dawa madukani kabla ya kupima, kwenda kwa waganga wa jadi, usafiri duni na miundombinu mibovu, uchumi mdogo na ukosefu wa elimu ya afya.

Anakiri kuwa wajawazito wengi wanajifungulia nyumbani kutokana na sababu mbalimbali huku akitolea mfano kuwa umbali ni kikwazo pia ambapo wananchi wanaoishi katika maeneo ya Bugoji, Majila na Bulangi wapo mbali na hospitali.

‘’Wananchi hao wanaishi zaidi ya kilomita 100 hivyo kusafiri kuja hospitali kwa ajili ya kujifungua labda iwe rufaa ya kufanyiwa upasuaji maana jiografia ni mbaya na hakuna usafiri wa uhakika hivyo wengi wanaamua kujifungulia nyumbani’’ anasema Dr. Musagafa.

Kuhusu elimu ya uzazi wa mpango anasema kutokana na mila na desturi za wananchi wa wilaya hiyo hufikiria na kukubali kwa shingo upande kutumia njia za kisasa za uzazi wa mpango angala wakifikisha watoto kuanzia sita.

Alitoa wito kwa wahisani na serikali kutembelea hospitali hiyo ili kuona hali halisi ya miundombinu ili waone umuhimu wa kumuenzi Mwalimu Nyerere kwa vitendo kwa kuhakikisha hospitali hiyo inakuwa na hadhi badala ya kujenga chuo kikuu kinachotarajiwa kujengwa katika wilaya hiyo kama njia ya kumuenzi Mwalimu.

‘’Serikali imuone Mwalimu shujaa, aliyejinyima sana na kuwanyima maendeleo watu wa nyumbani kwao na kunufaisha taifa hivyo inapaswa kujali kutengeneza mazingira mazuri ya huduma za afya na elimu kwa wananchi wa Butiama’’ alisema Dr. Musagafa.

Naye muuguzi kiongozi wa hospitali hiyo Neema Muchunguza alisema kuwa kila mwezi zaidi ya wanawake 100 hujifungulia katika hospitali hiyo hivyo serikali inapaswa kufanyia kazi mapungufu na upanuzi wa miundombinu ya hospitali hiyo ya wilaya.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *